Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Awali ya yote, nianze kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Njombe Mjini kwa kunipa kura nyingi ili niwe mwakilishi wao. Kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu, nitafanya kila linalowezekana niwawakilishe vema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa sikupata nafasi ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais basi na mimi nichukue nafasi kumpongeza sana, hotuba yake ilikuwa nzuri na kweli imetoa mwongozo na mwanga jinsi nchi yetu inavyoweza kwenda.
Pia nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa uteuzi wa Mawaziri, niwaombe wawe na amani, wafanye kazi kwa bidii wawatumikie Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijikita sasa kwenye Mpango, niseme mpango ni mzuri lakini nina mambo machache ya kusema. Watu wa Kanda ya Kati wanasema reli ya standard gauge lakini sisi wa Mkoa wa Njombe na Mbeya tuna reli tayari pale ya standard gauge ya TAZARA lakini malori bado yapo barabarani. Tukiacha hilo, kwenye Mpango tunasema kuna upembuzi yakinifu wa kujenga reli kutoka Mtwara - Mbamba Bay zaidi ya kilomita 800, sikatai, ni vizuri kwa maana ya kwamba ni kufungua mikoa iliyopo pembezoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kutoka Makambako - Liganga ni kilomita 200, hivi shida iko wapi? Hivi kipi ni rahisi, k ujenga reli kutoka Makambako - Liganga ambako chuma ndiko kipo au kuanza kufanya upembuzi wa kilomita 800 za reli mpya ya Mtwara – Mabamba Bay? Nashauri tufanye kile cha rahisi na pafupi chuma kitoke Liganga ili tufanye maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Njombe ndiyo unategemewa kuwa Mji Mkuu wa machimbo haya ya Kusini mwa Mkoa wa Njombe. Ndiyo mji utakaopokea wageni wengi, ndiyo mji ambao utatoa huduma lakini mji huu hauna maji. Kinachosikitisha zaidi katika Mji wa Njombe, mito miwili mikubwa imekatiza katikati ya mji. Niombe Serikali na nimuombe kaka yangu Mheshimiwa Lwenge, ameshaniahidi tutaenda Njombe tukaone ni namna gani sasa Mji wa Njombe utapata maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vyote vya Jimbo la Njombe Kusini au Mjini havina maji. Wananchi walichanga fedha wakiahidiwa kwamba kutakuwa na mradi wa Benki ya Dunia kusaidia ujenzi wa mradi wa maji. Fedha zao zimekaa huko Serikalini lakini maji hakuna. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri ameshaniahidi basi niamini hilo litaenda kutekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile suala la afya, tunakwenda kujenga uchumi wananchi hawana afya itasaidia nini? Pale Njombe sisi tuna hospitali ambayo mara inageuzwa Hospitali ya Mkoa, mara Hospitali ya Rufaa ya Mkoa lakini ukifika huwezi kujua kama umefika hospitali kwa jinsi ilivyochakaa. Utajiuliza hivi hapa ilitokea vita au kulitokea nini, lakini ukiingia ndani utaona watu wamelala, ni wodi. Hali ya hospitali ni mbaya sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Serikali ione nini tufanye katika hospitali ile. Hospitali ile imerithiwa kutoka kwenye Kampuni ya TANWAT ikakabidhiwa Serikali kwa maana ya Halmashauri ya Wilaya, Halmashauri zimekuwa zikiongezeka mpaka sasa ziko tano bado zinatumia hospitali ile ile na sasa inakuwa Hospitali ya Mkoa bado ni ile ile, eneo lenyewe la hospitali halizidi heka mbili.
Kwa kuwa mkoa umeshapewa eneo katika kijiji cha Mkodechi kwa ajili ya kujenga Hospitali ya Mkoa ambapo wameshafanya uthamini, wameshalipa fidia na wameshaweka mipaka, niombe Serikali itafute fedha tujenge hospitali hii. Tukijenga Hospitali ya Mkoa wa Njombe maana yake itasaidia sasa wananchi wa Njombe kwa maana ya mkoa pamoja na hao wawekezaji wanaokuja kwenye migodi hii kupata huduma ya afya na kuendelea na uzalishaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu. Niipongeze sana Serikali kwa hatua iliyochukua, changamoto zipo sikatai. Ni muhimu unapoanza jambo upambane na changamoto ili kusudi ujipange vizuri zaidi. Naomba sana Serikali ijitahidi changamoto hizi iziangalie kwa haraka. Wengi wamesema hapa lipo tatizo la walimu, maslahi yao yaangaliwe vizuri, wana madai, wamekwenda likizo hawalipwi, wanapandishwa vyeo nyongeza zao hawapewi, niombe sana suala hili lipewe kipaumbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo tatizo ambalo kwangu naliona ni kubwa, tatizo la elimu kwa watoto wa kike. Tatizo hili ni la kitaalam kidogo na ni tatizo linalotokana na makuzi ya mtoto wa kike. Mtoto wa kike katika makuzi yake anafika mahali haudhurii shule kwa sababu ya kukosa zana za kujisitiri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tena tuna bahati sana Waziri wa Elimu ni mama, Naibu Waziri wa Elimu ni mama, Makamu wa Rais ni mama na Waziri wa Afya ni mama, naomba tulione hili. Watoto hawa wa kike hawahitaji hata zaidi ya shilingi 10,000 kwa mwaka ili wajisitiri. Hawawezi kuhudhuria shule kwa sababu hali zao siyo nzuri. Haudhurii shule kwa zaidi ya siku 30 ata-perform vipi vizuri, mbona haiwezekani! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona taasisi nyingi za kina mama hazizungumzii habari ya watoto wa kike tuwasitiri namna gani ili wahudhurie shule. Taasisi zote zinazunguka zunguka tu pembeni zinafanya vitu vingine visivyo vya msingi. Naomba sana suala hili liangaliwe, Serikali ione namna gani itafanya kusaidia watoto wa kike wahudhurie shule siku zote za masomo ili kusudi waweze kupata elimu vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la umeme. Nashukuru sana Profesa Muhongo amefika Jimboni kwangu na tumejaribu kuona vyanzo vya umeme na ameniahidi kwamba Jimbo langu litapata umeme. Tatizo ninaloliona kama nchi kwa suala la umeme ni nguzo. Sisi Njombe tunazalisha nguzo nyingi sana, Serikali ifike mahali ifanye maamuzi kwa kuwawezesha wafanyabiashara wa Njombe wawe na mitambo ya kusindika nguzo zile. Kwa sababu nguzo hizi na umeme tunaoenda kusambaza nchi nzima ni mwingi sana, tunahitaji nguzo nyingi sana na Njombe sisi tuna uwezo wa kutoa hizo nguzo zote zikapatikana, lakini nani awezeshe wale wananchi ili waweze kuwa na mitambo ya kusindika zile nguzo?
Kwa hiyo, Wizara ya Nishati na Madini kwa namna itakavyowezekana iwawezeshe wananchi wenye nia ya kufanya shughuli hiyo ya kusindika nguzo ili wazalishe nguzo nyingi zaidi. Tunaagiza nguzo South Africa, Zimbabwe na Kenya, tena ni hadithi ya kusikitisha unaambiwa nguzo zimetoka Njombe zimepelekwa Kenya zimenunuliwa na mkandarasi zinarudishwa Mara na wakati Njombe sisi nguzo pale zimebaki hazina mnunuzi. Kwa hiyo, niombe sana suala hili lishughulikiwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni elimu ya ufundi, hivi tujiulize… (Makofi)
MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa kwa mchango wako mzuri.