Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami nitoe mchango wangu katika Wizara hii ya Ardhi. Kwa sababu kama alivyosema Mwalimu Nyerere, ili tuendelee tunahitaji vitu vinne na ardhi ikiwa ni mojawapo. Siasa safi tunayo ya ujamaa na kujitegemea, watu tunao, uongozi bora tunao unaotokana na Chama cha Mapinduzi na sera zake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maendeleo ni mchakato, hayawezi kuja siku moja kama wenzetu wanavyotaka. Hatukuwepo mwaka 1961 wakati tunapata uhuru, lakini Tanzania ya mwaka 1961 siyo Tanzania ya sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wenzetu wanaosema kwamba hakuna dira; dira ni Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Tena katika utangulizi tu, imezungumza Wazi kabisa nataka pale kunukuu aya ya 6(b) inasema: “kuongeza kasi ya kupima ardhi yao na kuwapatia hatimiliki za kimila ambazo watazitumia kama dhamana ya kuwawezesha kupata mikopo na kuendeleza shughuli zao za kilimo, uvuvi na ufugaji.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mtu akisema kwamba hatuna vision, achukue Ilani ya Chama cha Mapinduzi, hii hapa, kila kitu kimo humu ndani. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe mchango wangu sasa katika Wizara hii ya Ardhi. Ardhi kama tulivyosema, ndiyo rasilimali muhimu sana kwa Taifa lolote lile ikiwemo Tanzania; ardhi na vitu vyake vinavyopatikana katika ardhi. Inawezekana tumepotoka. Kwa mfano tu, inapogundulika mafuta au madini sehemu yoyote ya ardhi, fidia pale kwa Mtanzania ambaye anaimiliki au kijiji atapewa tu labda kama ana migomba, minazi au nyumba yake, lakini mali ile yote ya pale iliyogundulika chini ya ardhi tunaimilikisha kwa wageni. Mtanzania yule anabaki maskini kwa kisingizio cha uwekezaji au tunasema tutapata mrabaha ambao ni mdogo mno.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa ushauri katika hili ili kuendeleza kuwaneemesha Watanzania na kutengeneza matajiri wazawa wa Kitanzania ama kwa kumiliki Serikali au kijiji au yule mwenye ardhi pale, popote pale inapogundulika rasilimali hiyo, basi tutengeneze sheria ije kwamba yule ambaye yupo pale apate hata asilimia fulani katika umiliki ule ili utajiri ule uendelee kubaki kwa Watanzania badala ya sasa kubaki na mashimo na michanga isiyokuwa na faida na mrabaha mdogo ambao tunapata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni kuhusu migogoro ya ardhi. Tena Mheshimiwa Waziri nafikiri labda amepitiwa katika hili. Katika kitabu chake sijaona migogoro yoyote ya ardhi katika Wilaya yangu ya Morogoro katika Halmashauri ya Morogoro Vijijini na ukizingatia ndiyo tunaongoza kwa mashamba pori yanayomilikiwa na watu wanaojiita wawekezaji, wamekopea tu mapesa, lakini hawayaendelezi. Naomba kama nitaileta tena ile list aingize hiyo migogoro ili tuweze kupatiwa majibu na kuweza kurudishwa kwa wakulima waweze kuyaendeleza baada ya hawa wawekezaji kushindwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala la migogoro ya ardhi kama Mheshimiwa Waziri alipotuambia pale nyuma kwamba wameshaanza kuitatua, kwa mfano, wameanza kule Kilombero na Ifakara, basi kasi hii naomba iongezwe ili tatizo hili liweze kutatuliwa haraka. La sivyo, katika hatari ninayoiona ambayo inakuja mbele yetu, inayohatarisha umoja wetu, mshikamano na amani nchini, basi ni hii migogoro ya ardhi. Wote ni mashahidi, tumeona watu wenyewe, Watanzania sasa hivi wanavyopigana, wanavyouana, kwa hiyo, naomba Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi itolee kauli hili suala la upimaji wa ardhi na kuwamilikisha ardhi watu wake ili tuweze kuiendeleza tuondoe hili tatizo la migogoro ya ardhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nataka kutoa ushauri katika hili, migogoro mingi hii inasababishwa na viongozi waliopewa mamlaka kubwa lakini ufahamu mdogo wa kisheria, hasa viongozi wa vijiji na Mabaraza ya Ardhi, kwa sababu huko ndiko kuna migogoro mkubwa. Pia linachangiwa na kupewa dhamana kubwa wakati hawana posho wala mshahara, matokeo yake wanajikita kwenye vitendo vya rushwa kwa mtu ambaye anataka ardhi kwa sababu anajua hawa Wenyeviti wa Vijiji au Viongozi wa Vijiji ndio wenye mamlaka, anakwenda kuwanunua wanapata ardhi kiujanja ujanja, baadaye inatuletea matatizo makubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukienda huko vijijini utakuta mwekezaji au mtu yeyote kapata ardhi bila kuwashirikisha wananchi, lakini unakuwa muhtasari upo na sahihi zipo za initial na hati imetolewa mpaka Wizarani kwenye hiyo ardhi. Matokeo yake, hata tukienda Mahakamani, haki hiyo inakuwa hatuipati mpaka labda tumtegemee Rais atengue.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, naomba Wizara ya Ardhi, niliwahi kusema hapa kwamba pale Ngerengere sasa hivi ni Mamlaka ya Mji Mdogo; na sera za ardhi zinasema mjini popote hapahitajiki kuwa na shamba, lakini pale tuna shamba la Serikali ya LMU (Livestock Management Unity). Naomba shamba hili tuwape ardhi mahali pengine nje ya mji, ili shamba hili tuweze kulitumia kwa matumizi ya makazi na huduma za kijamii, lakini pia tuweze kuliendeleza kama ukanda wa viwanda vidogo vidogo ndani ya Halmashauri yetu kwa sababu ndiyo sehemu ambayo ina miundombinu mizuri lakini pia lipo karibu na Dar es Salaam, itakuwa ni rahisi sana kupata wawekezaji kwa ajili ya kuendeleza viwanda, kutimiza azma ya Serikali ya Awamu ya Tano kwenda uchumi wa viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nataka kujielekeza kwenye National Housing Corporation -NHC. Sasa hivi NHC wamejikita sana kwenye miji mikubwa na matokeo yake kutokana na ushindani uliopo, hata nyumba nyingine zinaanza kukosa wapangaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kuna Wilaya mpya, Halmashauri mpya na Mikoa mipya na tuna matatizo makubwa ya miundombinu ya majengo na wateja ni Serikali, wapo wa uhakika! Basi tunaomba kama wangeweza kuja kujielekeza huko kuanza kujenga nyumba kwenye mikoa mipya, Halmashauri mpya na Wilaya mpya ili tuweze kwenda kwa kasi na sisi tuwe na majengo na kuwa na ofisi na tutawalipa pango lao kwa kupitia Halmashauri zetu na Serikali Kuu kwa sababu jukumu hilo linatakiwa ni Serikali kujenga miundombinu. Nina uhakika wateja wa uhakika pale wapo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kujielekeza kwa Mheshimiwa Waziri kumwomba tena kwa mara nyingine aje katika Halmashauri yangu ya Morogoro ili kutatua mgogoro mkubwa wa Mkoa wa Pwani na Morogoro katika Kata ya Magindu Pwani na Kata ya Seregete „B‟ kuhusu mpaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tatizo ni la muda mrefu ambapo wenzetu wa Magindu wanaleta mifugo katika Halmashauri yetu na wanawauzia wawekezaji bila kufuata taratibu, matokeo yake inaleta migogoro mikubwa sana na uhasama kati ya watu ambao ni ndugu. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri aje katika Kata ile ya Kidugaro katika Kijiji cha Seregete hapo Magindu atusuluhishe kwa sababu tumeshakaa muda mrefu wenyewe hatujapata muafaka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.