Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kwanza kukushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi. Pia nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kwa jinsi anavyofanya kazi kubwa ya kulitumikia Taifa letu na hususani katika kukemea yale yote ambayo yanakinzana na matakwa ya Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia nafasi hii kumpongeza sana mpendwa ndugu yetu Mheshimiwa William Lukuvi kwa kazi kubwa aliyofanya kule Mbulu. Nampongeza sana namwombea kwa Watanzania wote na kazi anayofanya kwa nchi yetu ni kubwa kwa dakika hii ya sasa na jinsi ambavyo ardhi ni eneo lenye matatizo makubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kwanza kuiasa Serikali, mara nyingi tumepata matatizo mengi hasa yale yanayotokea baada ya wananchi kujenga, wananchi wanapimiwa na Maafisa wa Serikali katika maeneo ya hifadhi na maeneo ambayo hayafai kwa makazi, baadaye Serikali inaenda kubomoa bila hata fidia. Naiomba Serikali ianze kuainisha maeneo yote ambayo hayafai kwa matumizi mbalimbali ya wananchi wetu yakiwemo yale ya mikondo ya maji na yale ambayo ni hatarishi kwa maisha yao ili kuepuka hasara kubwa na matatizo mbalimbali yanayotokea baadaye. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kuwataka watu wa barabara na wale wengine wote wanaotumia ardhi, kwa sababu mara nyingi sana tumekuwa na tatizo la kubomoa majengo baada ya wananchi kujenga na wanapata madhara makubwa hasa ya kiuchumi. Kwa hiyo, ningeiomba Serikali iainishe hata yale ya barabara. Tumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais alipokuwa Waziri wa barabara aliweka alama X kwenye mtandao wa barabara zote nchini na kwa hivyo nyumba nyingi hazikujengwa hadi sasa na zile zilizokuwepo zinaendelea kuchoka lakini pia ione umuhimu wa kufidia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kuongelea eneo hili la fidia, wananchi wengi wanapata hali siyo nzuri kutokana na kwamba baada ya mtu kujenga anabomolewa jengo, madhara ni makubwa sana na kwa hivyo niitake Serikali iwe inaangalia madhara makubwa yanayompata Mtanzania wakati wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni eneo la Watumishi wa Serikali. Wote tunafahamu kuwa wale waliojenga kwenye mikondo ya maji na waliojenga kwenye barabara walipimiwa na watumishi wa Serikali ambao ni wataalam, haijalishi ni mtaalam wa aina gani lakini alienda kumpimia yule mtu. Leo hii tunapofika hatua ya kwenda kubomoa yale majengo bila fidia bila hali ya kuangalia ni kwa namna gani mwananchi yule anadhurika, hatuwatendei Watanzania haki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, watendaji wengine wamegawa plot mara mbili kwa Mtanzania mmoja, hali inayoleta migogoro mikubwa kati ya mtu na mtu au taasisi na taasisi. Naomba Serikali iangalie ni kwa namna gani inajitahidi kuona athari za namna hizi zinachukuliwa hatua za kimsingi na zile za mpango mzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia kuwepo na mpango kabambe wa wananchi kupata hati miliki. Hati miliki itaondoa mgogoro mkubwa wa ardhi kwa asilimia kubwa nchini. Iwezekane basi hata namna ya wananchi na Serikali yao kuingia ubia, zipi gharama za Serikali na ipi gharama ya mwananchi ili apate hatimiliki katika ardhi anayomiliki sasa. Kumekuwa na tatizo kubwa la kesi nyingi za ardhi kubadilishwa kutoka kesi ya ardhi kwenda kuwa kesi ya jinai kwa ajili ya uelewa mdogo wa wananchi. Naiomba Serikali itafute njia mbadala ya kuondoa tatizo hili kwa kutenga fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya Wizara hii ilipowasilishwa imekuwa ni bajeti ndogo kuliko tulivyotarajia. Tulitarajia tungekuwa na mpango kabambe wa wananchi kupata hatimiliki, lakini kwa ubia wa gharama kati ya Serikali na wao ili kuwezesha wananchi kumiliki ardhi yao na kuondoa migogoro mikubwa inayotokea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Serikali inabidi kukemea hii hali ya rushwa kwenye Mabaraza ya Ardhi. Maana siyo kwamba Wapinzani wakizungumza mambo yote ni ya uongo, mengine ni ya ukweli lazima tutazame na tuone tunafanyaje wakati inapobidi. Serikali isione tu kwamba hali ya kuachia vyombo vya kiutendaji ni hali ya kawaida, inaendesha inavyotaka, inaendesha kwa mfumo huu wa kidikteta, inaendesha kwa mfumo wa rushwa na wakati huo huo wananchi wanaumia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niitake Serikali kutazama upya watumishi wote au watendaji wote wa Mabaraza ya Ardhi na matendo yao na kuona ni namna gani wale ambao hawafai kabisa na wanatumia madaraka yao vibaya wanaondolewa kwenye system ya utendaji wa chombo hiki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika hali hii wananchi wengi wanashindwa kutetea haki yao kutokana na uelewa mdogo wa kisheria. Uelewa wa kutetea haki yao na pale wanapotaka kutetea haki yao wananchi wengi hawana uwezo na kwa hivyo wanashindwa kutetea haki yao lakini hali hii inasababisha madhara makubwa kwa wananchi kukosa haki yao na hatimaye kubaki na hali ya sintofahamu na kupoteza haki yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naitaka Wizara iwe na mpango kabambe wa kuona maeneo yenye matatizo ya ardhi au migogoro ya ardhi, basi wanafanyiwa utaratibu wa kuanzishiwa Mabaraza ya Ardhi yakiwemo yale ya Wilaya kwa ajili ya kupunguza umbali mkubwa na gharama kubwa wanayopata wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wengi wana kipato kidogo, hawawezi kuweka Wakili, hawawezi kwenda kwenye Mahakama ambayo iko mbali na makazi yao na kwa hivyo hawana uwezo wa kutetea haki yao ya kimsingi na wanaacha inapotea bure. Kama itawezekana pia kuwe na utetezi wa Wanasheria wa Halmashauri kutetea kesi zinazoingiliana na zile za Halmashauri na Halmashauri nyingine au kijiji na kijiji kingine kwa ajili ya utatuzi wa kero hizi na migogoro hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, kwa sababu muda huu ni mdogo, nimwombe Mheshimiwa Waziri alituahidi kule Mbulu kuanzishwa kwa Baraza la Ardhi Wilayani Mbulu. Namwomba sana katika bajeti hii haionekani, lakini sisi tayari tumetimiza wajibu wetu tutamwandikia barua Wabunge wote wa Majimbo mawili, Baraza hilo kwa mwaka huu lazima liwepo awe na majibu wakati wa kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, nimtakie kazi njema Mheshimiwa Lukuvi, niwatakie Watanzania wote utashi mwema wa kuiona nchi yetu inakwenda vizuri na niwashukuru sana kwa jinsi ambavyo Baraza letu la Mawaziri linafanya vizuri sana na wanajitahidi, kukejeliwa ni jambo la kawaida, tunaongezewa speed, tuwe na speed kali sana. Ahsanteni sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, kukejeliwa ni kuongezewa mwendo wa safari, nawashukuru sana.