Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunisimamisha tena hapa nikichangia Wizara hii ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nataka niendelee kuwaasa ndugu zangu wa Kambi yetu hii ya Upinzani, hii Serikali tuendelee kuishauri wale kule tusiwape miongozo wala taarifa, wale ni washangiliaji tuwaache waendelee kushangilia. Sisi tuendelee kuishauri Serikali pengine Mwenyezi Mungu anaweza akawajalia wakaweza kuyasikia na wakayafanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema kama ifuatavyo. Kwanza sijaelewa Watanzania tuna matatizo gani? Mwenyezi Mungu atupe nini tufike mahali tuseme Alhamdulillah tumepata tutoke hapa twende mbele? Kwetu sisi madini dhambi, mifugo hatari, kila kitu hatari! Nchi za wenzetu ardhi ni maliasili muhimu sana kwa maendeleo ya mwanadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ardhi ni rasilimali kubwa sana ingeweza kututoa hapa tulipo lakini ardhi hii sisi tunaifanyia nini na kwa nini tunaingia kwenye matatizo ya umaskini wakati ardhi tunayo? Inawezekana kwa sababu ya wingi wetu wa ardhi unatufanya tusijue thamani ya hiyo ardhi. Kwa sababu nchi za wenzetu kuwa na angalau heka 10 tu wewe ni tajiri, unakopesheka, taasisi zote za fedha wanakukopesha lakini ni Mtanzania gani anamiliki ardhi inayomsaidia? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tumefika hapa? Tunatengeneza sera ambazo naona hazina maandalizi. Nitoe mfano pale kwenye Jimbo langu la Liwale, tulipata mwekezaji akajenga shule ya Kiislamu nzuri tu, lakini kupata usajili wa shule hiyo leo ni mwaka wa tano kwa sababu hawana hati miliki. Wakienda kwenye Ofisi ya Ardhi wanaambiwa kijiji ulichojenga hakijaingia kwenye mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa hiyo huwezi kupata hati miliki, tunakwenda wapi? Mtu unaandaa mradi, unakwenda kijijini unatafuta ardhi, wanakijiji wanakupa ardhi, unajenga shule ama zahanati, umeshamaliza sasa unatafuta usajili ukifika Ofisi za Ardhi unaambiwa hicho kijiji hakijapimwa, hakiko kwenye mpango bora wa ardhi, kwa hiyo hatuwezi kukupa hati, hao ni Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii Wizara ya Ardhi naweza kusema ni kama Wizara mtambuka. Kuna Sera za Wizara kibao zimeingia hapa, mkanganyiko ni mkubwa, hatuelewi tunakwenda wapi. Kuna Sera ya Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mifugo, Wizara ya Madini na Wizara inayoshughulika na Misitu, hawa watu wote wanavurugana tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano mwingine, pale kwenye Jimbo langu walikuja hawa jamaa wa TFS, watu wa misitu, wamewapimia watu mpaka kwenye nyumba zao, kwa sababu maskini wale hawajui utaratibu ukoje, walikuja pale wakadanganywa, wakapima mpaka unakosa hata mahali pa kuchimba choo, ukitoka kidogo unaambiwa hapa ni kibao cha TFS. Hapa ndiyo mchanganyiko sasa wa makazi na misitu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu kitu kinachonishangaza hizi taasisi ni za Serikali. Hivi inawezekanaje taasisi ya Serikali inakwenda kijijini inawadanganya wananchi, wanaingia mkenge baada ya miaka miwili, mitatu ukienda kuuliza unaambiwa ni ninyi wenyewe wanakijiji ndiyo mlipitisha hii. Tulipitisha hatukujua hilo na ninyi ni taasisi ya Serikali mlitakiwa mtoe elimu. Sasa inafika mahali wananchi wanakosa mahali hata pa kukata kuni, wanaambiwa Mwenyekiti wenu wa Kijiji ndiyo alisaini lakini alijua hilo? Ndiyo hapo unapopata mkanganyiko kwamba jamani hii Serikali tunakwenda wapi, kwa nini hii neema ya ardhi isiwe ndiyo neema kwetu iwe ni majanga? Kitu gani ambacho tunaweza tukakipata tukakiona kwamba hiki kwetu ni neema? Namwomba Mheshimiwa Waziri ashirikiane na Mawaziri wenzake waangalie hizi sera, hii mikanganyiko inatoka wapi? Wananchi wetu hawa kwa nini tuwadhulumu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee katika upande huo huo wa ardhi. Kule kwangu nimewahamasisha vijana wameunda vikundi vya ufugaji na vya kilimo, lakini wale watu wakiandika andiko watafute wafadhili wanatakiwa wapate hati, mfadhili huyo watampataje? Matokeo yake vijana wale wamekwama, hawana wanachofanya, wakija mjini mnawafukuza, sasa wafanye nini, nani mwenye jukumu la kupima hii ardhi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwenye viwanja. Liwale bei ya kiwanja ni ghali sana. Nimekwenda nikamuuliza Mkurugenzi kwa nini hii hali ipo hivi? Akaniambia mimi sina wapimaji, nawachukua Nachingwea. Kwa hiyo, nikiwachukua Nachingwea wanakuja hapa nawalipia hoteli na kadhalika, kwa hiyo gharama ya kupima viwanja ipo juu, watu wanashindwa kumudu kununua viwanja. Sasa hili jukumu la kupima viwanja ni la nani? Hivi unawezaje ku-hire wapimaji kutoka sehemu nyingine kwenda sehemu nyingine halafu unakuja kwa mwananchi unamwambia bwana gharama ya kiwanja imekuwa kubwa kwa sababu tuna-hire wapimaji kutoka maeneo mengine, Mheshimiwa Waziri hili ni tatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu zote wananchi wetu wako mbele ya maendeleo kuliko Serikali na ndiyo hapo mgogoro unaanza. Mtu anakaa pale kesho na kesho kutwa unamhamisha eti panataka kujengwa hospitali sijui amekaa kwenye makazi yasiyo bora sijui pamefanyaje, mlikuwa wapi? Huyu mtu anaweka nguzo ya kwanza mpaka anamaliza tofali la mwisho anahamia mlikuwa wapi? Ndugu zangu, namtakia kila la kheri Waziri mwenye dhamana, lakini nataka tu nimtahadharishe kwamba uwepo wa ardhi nyingi Tanzania imeonekana hatuithamini, kama tungekuwa tunathamini ardhi leo tusingekuwa hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye majengo kujengwa chini ya kiwango. Naamini Shirika la National Housing lina Wahandisi wengi wa kutosha inafikaje mtu unajenga jengo linakuwa chini ya kiwango, hii ni rushwa! Mkandarasi kuipata hiyo tenda anatumia zaidi ya nusu ya fedha aliyotenda. Hivi ni injinia gani atakwenda kumsimamia yule mkandarasi kumwambia hili jengo umejenga chini ya kiwango wakati tayari ameshachukua hela kutoka kwake, anaupata wapi ujasiri wa kumkemea?