Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Na mimi naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, ameitendea haki Wizara hii tangu Serikali ya Awamu ya Nne na hii ya Tano. Vilevile nampongeza Dkt. Yamungu Kayandabila, nadhani hii ni hotuba ya kwanza ambayo tumekuja humu ndani tukiwa very comprehensive; ina information za kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nampongeza na Naibu Waziri Mheshimiwa Dkt. Angeline Mabula, naye naamini kwamba ameitendea haki nafasi ya wanawake katika uongozi. Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara yako, kwa kweli lazima tuwatendee haki; na kama ambavyo Mheshimiwa Rais anasema tumuombee dua, naamini Watanzania wote watakubaliana na mimi kwamba dua hizo pia tuzielekeze katika Wizara yako.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, Wizara yake inapambana na mapapa wakubwa wa ardhi, lakini tumeona anavyothubutu na kuchukua maamuzi ambayo yana tija kwa wananchi walio wengi. Mimi binafsi napenda nimpongeze kwa kutupatia Halmashauri ya Lushoto Baraza la Ardhi, hiki kilikuwa ni kilio cha miaka mingi na tunaposema Baraza la Ardhi wote tunafahamu kwamba wanaoathirika zaidi na masuala ya ardhi ni akinamama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani wanawake kule Lushoto hasa wale wajane ilikuwa ni lazima wasafiri kwenda mpaka Korogwe wakati mwingine anaambiwa aje na mashahidi wasiopungua sita, sasa yeye ni mjane anaambiwa leta mashahidi, awasafirishe, wakati mwingine awalaze. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri amesikia kilio chetu kwa haraka sana na amechukua hatua na ofisi ile imefunguliwa rasmi Mei 13, tunamshukuru sana na naamini dua hizi za wajane pia zitaelekea kwake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye hii orodha ya mashamba na migogoro ya matumizi bora ya ardhi, katika Wilaya ya Lushoto ameainisha maeneo mawili. Kuna shamba namba 902/3 lakini pia kuna eneo la Kijiji cha Shumenywelo pamoja na shamba la misitu ya hifadhi la Shume. Mgogoro ule ni wa siku nyingi, namwomba sana afike Lushoto akatatue mgogoro huu, umechukua muda mrefu sana na naamini kwa kasi hii ambayo ameanza nayo na ambayo naamini kwamba sio nguvu ya soda atafika maeneo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunalo tatizo la shamba la Mnazi, Mnazi Sisal Estate, lilikuwa chini ya mamlaka ya mkonge. Kama yalivyo mashamba mengine yote na lenyewe limebinafsishwa. Shamba hili lina ukubwa wa takriban hekari 6,000 na ndani yake yapo mashamba matatu. Amepewa mwekezaji mmoja kutoka nchi jirani ya Kenya. Wakati anakabidhiwa shamba hili, amekabidhiwa hekari 1,500 zenye mkonge. Hivi ninavyozungumza hapa, hekari ambazo zina mkonge ni 45 tu. Kwa hiyo, kadri muda unavyozidi kwenda ndiyo anavyozidi kushusha uzalishaji. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, shamba hili tulirudishe kwenye miliki ya Serikali halafu tutalitafutia uwekezaji mwingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, shamba hili pia lina migogoro na vijiji vinavyolizunguka, kipo Kijiji cha Kwemng’ongo na Kijiji cha Kwemkazu. Hawa kuna wakati fulani mwekezaji huyu aliwapa hekari 750, lakini baadaye amewanyang’anya kwa hiyo, naomba sana suala hili tulifanyie kazi kwa sababu ardhi hii imekaa haina kazi yoyote na Wilaya ya Lushoto kwa ujumla ina matatizo ya ardhi na hii ndiyo ardhi pekee ambayo tunaweza tukaipata kubwa ya kuweza kutusaidia katika masuala mazima ya uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo Wilaya ya Lushoto maeneo mengi sana yanamilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania. Kwa ukweli wanayamiliki kihalali, lakini yapo baadhi ya maeneo ya Taasisi haswa shule pamoja na vituo vya afya yapo katika maeneo haya. Nimwombe Mheshimiwa Waziri kwamba, kwa busara anaweza akatukutanisha nao ili angalau yale maeneo ambayo yanatumiwa na umma waweze kuyatoa kwenye hati zao ambazo wanazimiliki kwa mujibu wa taratibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni suala zima la land bank, kwamba Halmashauri zetu nyingi hazina hifadhi ya ardhi na huko kwenye Halmashauri wanatoa ardhi hovyo hovyo hasa kwa watu ambao wanakuja mara nyingi kwa kigezo cha uwekezaji. Sasa niombe Wizara kupitia sera ije na sera mahsusi ambayo inazitaka Halmashauri zetu zitenge maeneo mahsusi kwa ajili ya uwekezaji, kwamba yawepo tu, yawekwe kama hifadhi ya ardhi kwa ajili ya uwekezaji wa siku za usoni. Kama ambavyo juzi Mheshimiwa Mbowe alikuwa anazungumzia suala la hekta 11,000 – zile kwenye suala la uwekezaji wa ardhi ni chache sana. Kwa hiyo, nataka niseme kwamba ni lazima kuwe na sera madhubuti ambayo inalizungumzia suala hili ili tunapo zungumza kwamba tunataka maendeleo tuwe na ardhi, watu na siasa safi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siasa safi hapa ni good policy. Policy ambazo ni nzuri za kuweza kuwa na matumizi bora ya ardhi ili iweze kuleta tija kwa wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo, naomba nikushukuru sana na niwapongeze pia timu ambayo inamsaidia Mheshimiwa Waziri, tunawatakia kazi njema na ufanisi mwema. Ahsanteni sana.