Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuwa mchangiaji wa kwanza kwa hoja muhimu iliyo mbele yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake kwa kazi nzuri wanayoifanya kuisimamia sekta hii muhimu na kwa maana hiyo, sitamung’unya maneno, ninaunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 84 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri, kuna jedwali linaloonesha marejesho ya asilimia 30 kwa Halmashauri. Nimefuatilia pale nikagundua katika Mkoa wa Kagera, Wilaya ya Misenyi hatujarejeshewa fedha. Kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri na wataalam wake watusaidie kwa sababu tulishawasilisha maombi yetu ya kurejeshewa asilimia 30 kama tunavyostahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia kusema kwamba katika kitabu cha utekelezaji wa miradi ya Wizara ya Ardhi pamoja na Shirika la Nyumba katika ukurasa wa 25 wamebainisha pale kwamba Mutukula Commercial Complex Center ule mradi umeshakamilika kama walivyoonyesha kwenye kitabu, lakini mimi kwa macho yangu hivi karibuni nilitembelea lile jengo, kwa kweli halijakamilka. Niliwauliza wenzangu baada ya kuona hapa leo hii kwamba imekamilika, lakini Mwenyekiti wa Halmashauri ya Misenyi amenihakikishia akasema bado. Kwa hiyo, nadhani limekamilika tu kwenye vitabu, lakini kwa hali halisi, bado. Nawaomba wahusika walifanyie kazi ili jengo hilo likamilike.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii pia kupongeza Shirika la Nyumba la Taifa kwa kazi nzuri wanayoifanya. Pale Mutukula wamenunua eneo na wamepima viwanja 22. Ni jambo jema kwamba sasa Mutukula itapendeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwakaribishe waungane nami na waungane na Wanamisenyi katika jitihada za kujenga mji wa kisasa wa Bunazi unaofanana na miji ya Ulaya. Mji huu tumejipanga kuujenga na niwakaribishe Shirika la Nyumba washirikiane na sisi. Mpango wetu tulionao, tutaanzia Mutukula, tutajenga Bunazi, tutaenda Kyaka na kwa kweli utaratibu tunaotaka kutumia, siyo kutoa ramani za kujenga nyumba tu, tutakupa kiwanja lakini pia tutakupa na ramani ya nyumba ya namna gani uijenge sehemu ipi. Tunataka tujenge mji wa kisasa unaofanana fanana na miji ya Ulaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawakaribisha Shirika la Nyumba waungane nami katika kutekeleza lengo hilo na kwa kweli Mheshimiwa Lwakatare, Mbunge wa Bukoba Mjini, naomba nimwahidi kwamba ndani ya miaka mitano ijayo Mji wa Bunazi utafunika Mji wa Bukoba, siyo kwa nia mbaya ni kwa sababu ya masuala ya maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo changamoto ya upungufu wa wataalam wa ardhi, namwomba Mheshimiwa Waziri na wataalam wake, watusaidie kutupa wataalam wa ardhi pale Halmashauri ya Misenyi ili tunapopanga mipango yetu, iweze kutekelezwa kwa haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa tisa wa kitabu cha orodha ya migogoro alichotoa Mheshimiwa Waziri, naomba tu niongeze katika vijiji vilivyotajwa mle ni vijiji vya Kakunyu na Bugango pamoja na Byeju, lakini kijiji cha Nkerenge sijakiona pale, naomba kiongezwe. Pia katika Kata ya Mabale, hii ni Kata mpya, kuna mgogoro pia kati ya ranchi ya Mabale na vijiji vya Kenyana na Kibeo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa jitihada ambazo amezifanya kumaliza mgogoro wa Kakunyu. Namuomba pia Mheshimiwa Waziri wa Ardhi na yeye afuatilie kwa karibu mgogoro huu umalizike; na bahati nzuri Mheshimiwa Waziri Lukuvi utendaji wako mzuri unaouonyesha umechangiwa na kupata bahati ya kuwa DC wa Bukoba wakati fulani. Sasa Wanamisenyi tunatambua unaifahamu vizuri Misenyi, utusaidie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili mgogoro huu uweze kumalizika, jambo muhimu ni kuwa watu wote wanaohusika wafanye kazi kwa uadilifu kwa sababu bila kutanguliza uadilifu mbele, hakuna kitakachopatikana. Ipo migogoro mingine kwa mfano Hifadhi ya Msitu wa Miziro kuna mgogoro kati ya hifadhi na vijiji; vile vile katika Kata ya Buyango, Kijiji cha Kikono kuna mgogoro kati ya kijiji pamoja na Msitu wa Miziro na Kata ya Bugandika kuna mgogoro katika Kitongoji cha Ishozi na hifadhi ya jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo, naunga mkono hoja.