Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Vicky Paschal Kamata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. VICKY P. KAMATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu. Kwanza kabisa ninamshukuru Mungu kwa afya njema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili nianze kwa kusema kwamba ninaunga hoja hii mkono kwa asilimia mia moja lakini pia ninampongeza sana Profesa Muhongo kwa kurudi tena katika Wizara hii. Imani kubwa aliyokuonyesha Mheshimiwa Rais John Joseph Pombe Magufuli, ni imani kubwa ambayo Watanzania wengi tulioko huko nje pia tunayo kwako pamoja na Naibu wako Dkt. Kalemani. Tuna imani kubwa sana, kwamba kazi itafanyika na matokeo yataonekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasisitiza na narudia tena kusema kwamba Rais amekuamini Profesa Muhongo, amekurudisha kwa sababu anakujua. Tunataka kwenda kwenye uchumi wa kati ambao unategemea viwanda. Mheshimiwa Mwijage, Profesa Mkenda pamoja na Dkt. Meru hawana muujiza wowote ule watakaoweza kuufanya ili Tanzania iwe kweli ya viwanda iwapo ninyi hamtafanya kazi nzuri ya kuhakikisha kwamba umeme wa uhakika unapatikana ili kuwezesha Tanzania ya viwanda iweze kufikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi na Kamati yangu tulienda Arusha, tulitembelea Kiwanda cha kutengeneza transfoma, TANELEC. Kiwanda kile kinafanya kazi nzuri sana, kinatengeneza transfoma zenye obora mkubwa sana. Transfoma zile zinanunuliwa Kenya, Uganda na nchi nyingine lakini sio Tanzania, kwa maana ya kwamba TANESCO hainunui zile transfoma zenye ubora mkubwa. Wananunua transfoma kutoka India, zinakuja hapa zinafika kwa gharama kubwa pengine kuzidi hizi za hapa kwetu na bado hazina ubora wa kutosha, zinalipuka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wajumbe wengi wameeleza kwamba kwenye maeneo yao yametokea matukio ya hatari sana kwa sababu zile transfoma zimekuwa zikilipuka, wanashindwa kununua transfoma kutoka TANELEC. Kamati yangu ilipata uchungu sana baada ya kujionea kazi nzuri ya kiwanda kile, lakini kuna malalamiko na changamoto kubwa wanazokutana nazo. Kamati ilipata uchungu na ilipata hasira sana. Ninaamini kama kamati yangu ingekuwa na mamlaka, ingekuwa na uwezo siku ile ile tungeweza kutumbua majipu fulani fulani.
Lakini tulijiuliza, kama tunaweza kumtumbua Mkurugenzi wa TANESCO tukamuita jipu, tutakuwa tunamuonea kwa sababu tatizo sio Mkurugenzi wa TANESCO, tatizo si Idara ya Manunuzi, tatizo ni Sheria ya Manunuzi. Sasa kama tunazo sheria ambazo zinakuwa kikwazo, sheria ambazo hazitusaidii, tunataka kukimbia sheria zinatufunga miguu tushindwe kwenda tunakoenda, kwa nini hizo sheria zisiletwe haraka tuzifanyie marekebisho ndani ya Bunge hili? Tuifanyie marekebisho hiyo Sheria ya Manunuzi kusudi tuweze kufanya kazi vizuri kwasababu hii Sheria ya Manunuzi imekuwa kichaka, tutakuwa tunawaonea watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikasirika sana siku ile na Mkurugenzi wa TANESCO tukasema kwanza yeye ni Mjumbe wa Bodi inawezekanaje wanunue transformer India zenye ubora mbovu? Lakini tunakuja kujua kumbe si yeye, tatizo ni sheria yetu ambayo tuliipitisha wenyewe humu. Sasa tulete hiyo sheria haraka sana ifanyiwe marekebisho kusudi tuweze kufanya kazi vizuri na TANELEC iweze kuuza transfoma zake hapa hapa Tanzania; na kiwanda chetu kama kweli tunataka Tanzania iwe ya viwanda basi tuanze na viwanda vilivyomo humu kuvipa uwezo wa kuendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ningependa nizungumzie wachimbaji wadogo wa Geita. Mheshimiwa Profesa Muhongo na kaka yangu Dkt. Kalemani; tena Dkt. Kalemani unaona kabisa hali halisi ya watu wako wa Geita maana wewe unatoka Geita, wewe ni Mbunge wa Chato. Maisha ya wananchi wa Geita ni magumu na Serikali imekuwa ikiahidi kila siku kwamba itawapa maeneo ya kuchimba lakini sielewi tatizo ni nini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Profesa Muhongo ulianza vizuri sana kipindi kile, uliwapa matumaini makubwa sana wananchi wa Geita hususani hawa watu ambao wanachimba, walijiunga kwenye vikundi vya SACCOSS mpaka leo vikundi vinakufa kwa sababu hakuna maeneo ya kuchimba. Naamini pale ulipoishia kipindi kile baada ya matatizo yale kutokea, umerudi tena, ni kwa mpango wa Mungu na kwa makusudi mazuri na nia njema ya Rais kwamba uwasaidie wachimbaji wadogo wadogo wa Geita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa taarifa nilizonazo, lile eneo la STAMICO lina-expire Julai, 2016 yaani mwaka huu, tuna mwezi mmoja tu lile eneo lina-expire. Huoni umuhimu Mheshimiwa Waziri wa kuwapatia sasa wananchi hilo eneo la STAMICO ili waweze kugawana SACCOSS zile ziweze kuanza kufanya kazi? Wananchi wa Geita wanategemea uchimbaji, sasa hawafanyi kazi matokeo yake watu wanaanza kufanya vitendo vya uhalifu kwa sababu hawana kazi za kufanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi ninaomba sana kupitia bajeti, nina uhakika bajeti hii itapita kwa sababu ni nzuri na tena kama ulivyosema asilimia 94 ni kwa ajili ya maendeleo, kwahiyo ninaamini kabisa Geita itapewa kipaumbele.
Mheshimiwa Muhongo juzi umeenda umekutana na Watanzania wanaoishi Geita, umewapa matumaini na umerudisha imani kubwa, wana imani na wewe na mimi Mbunge wao nasema waendelee kuwa na imani na wewe kwa sababu wewe ni mnyoofu, ni muadilifu na ahadi zako hazipindi pindi. Nina uhakika safari hii maeneo ya wachimbaji wadogo yatapatikana, tukianza na hilo linalo-expire mwezi Julai.
Lakini vilevile Mheshimiwa Muhongo unauwezo wa kwenda kuzungumza na GGM. GGM wamehodhi maeneo makubwa sana. Kuna lile eneo la Nyamasagata, kuna la Semina, kwanini usiongee na GGM wakawagawia haya maeneo, wakawaruhusu basi hata wakachimba kwa sababu wenzetu wa Ghana wamewezaje wachimbaji wadogo na wakubwa kuogelea kwenye bwawa moja bila kuleta madhara yoyote? Ni utaratibu tu uwekwe, hawa wachimbaji wadogo wachimbe na hawa wakubwa pia wachimbe, hawa wadogo kwanza wanachimba kwanza hawana vifaa vikubwa kwa hiyo hawawezi wakachukua dhahabu nyingi ya hawa wawekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, itawasaidia tu kuweza kuendesha maisha yao ya kawaida na kelele pia zitakwisha. Nikuombe Profesa Muhongo na Naibu wako, Katibu Mkuu; sisi tuna imani kubwa sana na ninyi, kwa hiyo ninaamini kabisa, mara baada ya hii bajeti kupita, utafika Geita, utawasaidia wachimbaji wadogo, SACCOSS zitaanza kufanya kazi na Geita itafanana kwamba huu kweli ni mji wa dhahabu maana maisha wanayoishi Watanzania pale kwa kweli hayaridhishi hata kidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijagongewa Kengele pia nipongeze na mimi kidogo umeme wa REA. Kwa kweli kwa Mkoa wetu wa Geita mmejitahidi, tunakwenda vizuri, lakini kuna baadhi ya maeneo ambayo nguzo zimepita muda mrefu sana na mpaka sasa imefikia mahali wananchi wanaanza kupata hasira wanataka kukata zile nyaya kwamba kwa nini umeme umepita umeenda maeneo mengine na sisi tumerukwa, na sisi tuko kwenye kata ambayo ni makao makuu ya kata? Kuna vituo vya afya pale, kuna sekondari pale, kuna shughuli nyingi za maendeleo ziko pale lakini umeme umepita juu. Juzi juzi nilikuwa naongea na Diwani wa Nyaruyeye, kaniambia kweli nimekuwa na kazi kubwa ya kuzuia watu kwenda kuangusha zile nguzo kwa sababu zimepita hapa muda mrefu na sisi hatuna umeme.
Kwa hiyo, ninaamini kabisa baada ya bajeti hii kupita, maeneo ya Nyaruyeye, Nyarugusu na mengineyo yote ambayo bado hayajapatiwa umeme lakini nguzo zimepita basi ule umeme ushuke ili watu wote tuweze kunufaika na huo umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yangu yalikuwa ni hayo machache, narudia tena kupongeza Wizara hii na kuwatakia kila la heri, ahsanteni sana.