Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi kuchangia asubuhi hii. Mimi nianze kwa kuwashukuru na kuwapongeza Wizara ya Nishati na Madini kwa kazi nzuri wanayoifanya, maana unapotaka mambo yapelekwe kwako au yasogezwe kwenye eneo lako vilevile lazima utambue kazi ambayo imefanyika. Kazi kubwa imefanyika na inaridhisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa kusema hivyo sina maana kwamba tumemaliza, bado tuna kazi za kufanya na tunaendelea nao. Lakini nalinganisha na miaka nyuma ambapo umeme ulikuwa unakatika mara kwa mara, kila mahali giza, sasa hivi hali hiyo haipo tumeweza kupambana nayo na tumekabiliana nayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi mbalimbali inayoendelea, tunaona miradi mingi, tumepata gesi ya Mtwara, kutoka na gesi hiyo tumefungua miradi mikubwa ya kufua umeme pale Kinyerezi ambayo ikikamilika tutapiga hatua kubwa sana katika kuwa na umeme wa kutosha na mzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna miradi mingine, kwa mfano ile njia kubwa ya umeme kutoka Iringa kwenda Shinyanga ambayo ikikamilika ni kama backbone, ina-cross kuanzia Iringa kwenda Shinyanga, itakuwa ni chanzo cha kupeleka umeme mikoa mengine ambayo imezungukwa mikoa hiyo, ambao ni umeme mkubwa KV 400. Hili ni jambo la kujisifia na kuishukuru Wizara ya Nishati na Madini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niisemee REA. REA kazi yao vilevile ni nzuri sana, vijiji vingi nchi nzima vimepata umeme. Mimi najiuliza ingekuwa hakuna REA tungekuwa wapi? Kazi ya REA ni nzuri, nawashukuru na kuwapongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema pamoja na kazi nzuri bado tuna kazi kubwa ya kufanya. Pale Kagera Mkoa mzima kuna tatizo la umeme kubwa sana. Hata leo ninavyoongea hivi sasa hivi hakuna umeme umezimika, jana hivyo hivyo, juzi hivyo hivyo, kila siku, mwaka mzima; wanazima umeme asubuhi unarudi jioni au haurudi kabisa, tatizo ni kwamba hatuko kwenye Gridi ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme wa Kagera unatokea Uganda, tunanunua Uganda hivi leo Uganda wanashida kubwa ya umeme, umeme ni pungufu. Kwa hiyo, wanakata umeme, Kagera tuko gizani muda mwingi sana. Kwa hiyo niombe Kagera iunganishwe kwenye Gridi ya Taifa. Nafahamu umesogea kama si Geita basi ni Chato wa Gridi umefika umeme. Kazi ifanyike kwa jitihada kubwa ufike mpaka Bukoba, mpaka Karagwe, mpaka Ngara kote tupate umeme wa Grid ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna mradi mwingine pale Rusumo wa umeme wa kuzalisha megawatts 80. Mradi huu umeanza kwa ushirikiano wa nchi tatu, Rwanda, Uganda na Tanzania, lakini kasi yake si kubwa hairidhishi. Kasi iongezwe kusudi mradi huu ukamilike tupate umeme huo. Umeme huo ukipatikana ni mwingi, megawatts 80 kwa Kagera tutapata megawatts 27 utatosha mahitaji yetu na utatusaidia kwa shughuli mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimezungumzia miradi ya REA. Pale kwangu Bukoba Vijijini kwanza nishukuru vijiji vimepata umeme baadhi, lakini siyo vyote. Kuna vijiji vingi havijapata umeme, Kata nzima ya Kibirizi haina umeme. Kijiji cha Kibirizi chenyewe, Omubweya na Kamuli havina umeme. Kata nzima ya Rukoma haina umeme, Rukoma yenyewe, Nsheshe na kwingineko hakuna umeme. Kata ya Kikomelo umeme haujakanyaga. Niombe sana vijiji na kata hizi zipelekewe umeme na kwenye Ilani ya CCM ya uchaguzi ya mwaka jana kata hizi zimetajwa kwamba kutapelekwa umeme kwenye awamu hii ya mwaka 2015/2020. Niombe kazi ifanyike na umeme usogee Kata ya Kibirizi, Kata ya Lukoma na Kikomelo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hata vile vijiji vingine ambavyo umefika, jambo ambalo nafikiri REA hawakulifanyia kazi vizuri, vijiji vya Bukoba ni vikubwa sana, vikubwa kweli kweli; unakuta kijiji kina kaya 400 wamepeleka umeme kaya 15, 20 au 10. Ni kweli kwenye kijiji umeme umefika lakini wananchi hawajapata umeme kama inavyostahili. Niombe sana kwamba jitihada ziendelee kwenye REA III, vijiji hivi viongezewe mgao au kazi isogee ndani zaidi kwenye vijiji ambako tayari wamefika lakini hawajafika maeneo mengi ya kutosha na vitongoji vingine ambavyo havijafikiwa nako vifikiwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nimalizie kusema kwamba, umeme huo tunapoupeleka vijijini bado kuna mapungufu fulani fulani.Kwa mfano taasisi kama shule za sekondari au zahanati au sehemu kama hizo tunasema wananchi wajiwekee wenyewe ni kazi kubwa sana kufunga umeme kwenye sekondari uwake madarasani, maabara wafunge wiring mle ndani, nyumba za walimu, wananchi hawawezi, Serikali nayo iangalie uwezekano wa kufanya kazi hii yenyewe, iwe ni sehemu ya mradi, wasiishie tu kupeleka umeme kijijini labda kwenye center halafu wakaondoka.
Mheshimwia Mwenyekiti, taasisi kama shule REA yenyewe ifunge umeme mle ndani kwenye taasisi za Serikali; iwe shule, iwe zahanati kusudi matunda ya umeme yaonekane kwa wananchi walio wengi, taasisi zipate umeme, kama ni hospitali ziweze kuboresha huduma pale tuwe na beni za damu (blood bank) na huduma nyingine kutokana na kutokuwa na umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi hii naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.