Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafsi nami niweze kuchangia hoja hii ya Wizara ya Nishati iliyopo mbele yetu. Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya na baada ya hapo nijielekeze kwenye suala la umeme vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Njombe Mjini tuna masikitiko makubwa sana, wengi wamesifia REA lakini Njombe Mjini tunasikitika kwa sababu hata kijiji kimoja hakijapata umeme wa REA. Utaratibu wanasema Njombe tunatakiwa kupata umeme kutokana na Mkandarasi anayetengeneza umeme kutoka gridi ya Taifa kwenda Songea. Mkandarasi yule anakumbwa na matatizo mengi tu, mara hana fedha, mara nini.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hii hali inaleta sintofahamu sana kwa wananchi wa Jimbo la Njombe Mjini na inasababisha hali ya siasa kuwa ngumu, lakini vilevile morali inapungua sana kwa wananchi wakisikiliza habari ya TANESCO na habari ya REA, wanaingiwa na kasumba kwamba kwa sababu lile Jimbo linaitwa Jimbo la Njombe Mjini na umeme wa REA ni wa vijijini, kwa hiyo Njombe haimo. Kwa hiyo, naomba sasa Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anakuja kufunga hotuba yake atuambie, Njombe tutapata lini umeme wa REA. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana TANESCO na REA kwa kazi nzuri waliyoifanya kwa ajili ya umeme wa kupeleka kwenye kwanda kipya tunachotaka kukijenga pale Lwangu, Kiwanda cha Chai. Naomba sasa Wizara na TANESCO wasaidie, msimamo ambao tumekubaliana kwamba kazi ile inaanza mwezi wa Sita kweli ianze, kwa sababu tumeshapata mwekezaji kwa ajili ya chai, chai ile wakulima wale wameshalima haina kiwanda. Kwa hiyo, naomba sana Kijiji cha Lwangu kipelekewe umeme kutoka Kilocha ili chai ile ianze kusindikwa pale kwenye Kijiji hicho cha Lwangu na wananchi waanze kupata fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumzia kwa Jimbo la Njombe na kwa maana ya Mkoa wa Njombe ni Mchuchuma na Liganga. Kwa kweli Wanamkoa wa Njombe tunasikitika sana kwa sababu Mchuchuma na Liganga ni hadithi ya miaka mingi sana, juzi nimesema na leo narudia, kwamba kwa kweli if we are serious na maendeleo ya nchi hii, Ujerumani imeendelea kwa chuma, chuma ndicho kilichoendeleza nchi, sasa chuma cha Liganga ni hadithi tu miaka yote, chuma Liganga, chuma Liganga.
Mheshimiwa Naibu Spika, wamefanya kazi ya kuchepusha madaraja wakisema madaraja yaliyopo ni madogo, mitambo haitaweza kupitia, madaraja yale safari hii yamesababisha matatizo, maji yamejaa yameshindwa kupita, kisa ni kwamba wamechepusha madaraja ili wapitishe mitambo, hakuna cha mitambo, majani yameota. Wale Waheshimiwa waliokwenda kule kwenye migodi inasemekana kwamba wamegundua kuna madini mengine, wameanza kuchenjua hayo, habari ya chuma wameachana nayo. Sasa tuambiwe na Wizara, Mchuchuma ipo ama haipo! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine cha kusikitisha, Mchuchuma amepewa NDC. Watu wote humu ndani tunajua NDC ilivyo, hivi afya ya NDC ikoje jamani? NDC anaweza akachimba chuma! NDC haiwezi kuchimba chuma leo, uchumi wa NDC uko chini sana. Niwaombe sana Serikali muwe na maamuzi na kama mmesema kwamba Mashirika ya Hifadhi ya Jamii yaingie kwenye biashara inayoajiri watu wengi, migodi ile ya Mchuchuma na Liganga inatarajiwa kuajiri watu 30,000. Hayo Mashirika ya Hifadhi ya Jamii yapelekwe huko wafanye hizo kazi za kuchimba makaa kule Mchuchuma na chuma pale Liganga. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hotuba yake aseme chochote juu ya Mchuchuma na Liganga ili tujue msimamo ukoje.
Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kuhusu TANESCO Njombe. TANESCO Njombe wana shida kubwa sana. Wapo vijana wachapakazi sana pale, wanajitahidi lakini ukatikaji wa umeme kutokana na hali ya hewa ya Njombe, mvua nyingi na miti mingi, mara nyingi sana miti inaangukia nyaya, hawana gari za kutosha, wana gari moja TANESCO Njombe. Wasafiri kilometa 70 upande mwingine wa Jimbo la Lupembe kwenda kuangalia tatizo la umeme, wakitoka huko warudi Jimbo la Njombe Mjini waende mpaka Luponde tena kuangalia umeme, unaweza ukakuta siku mbili Kiwanda kama cha Chai Luponde kinakosa umeme kisa TANESCO hawana gari ya kuwafikia.
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini na wakubwa wa TANESCO watakuwa wanasikia maneno haya. Naomba wawasaidie wale wachapakazi vijana pale Njombe ili wapate gari lingine la kufanya service kwenye lane za umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, liko suala la viwanda. Sisi Njombe tuna viwanda, moja ya kiwanda tulichonacho ni Kiwanda cha Nguzo (TANWAT). TANWAT wameingia kwenye tenda ya kuomba ku-supply nguzo TANESCO, wamekosa. Ni jambo la kusikitisha sana! Masharti ambayo wameweka TANESCO na utaratibu waliouweka unasikitisha sana. Wametoa tenda hii South Africa tena ku-supply nguzo za umeme wakati Njombe kuna nguzo za umeme. Ni kweli inawezekana kiwango ambacho kinatakiwa ni kikubwa sana, ndiyo uwape South Africa shilingi bilioni 60 ku-supply nguzo TANESCO, halafu wazawa wananyimwa kwa kuwalambisha tu unawapa Sao Hill nguzo za shilingi bilioni 24!
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, kwa hili nitakwenda ofisini kwake tukae tuongee tuliangalie. Haiwezekani kabisa, kwa sababu nguzo hizi hawa Makaburu wata-supply kwa miaka mitatu, ina maana viwanda vyetu vile sasa havitakuwa na kazi. Nasi kama Watanzania tunasema tunataka nchi iwe ya viwanda, ni lazima tuanze ku-favour viwanda vya ndani. Kama haiwezekani hiyo, basi hata viwanda haitakaa iwezekane. Maana yake watakuja watu wa viatu, watatengeneza viatu, tutasema viatu vya Tanzania vina udhaifu moja, mbili, tatu, havinunuliwi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana, kama nguzo hizi kiwanda kile kimekaguliwa, ubora wa nguzo umekaguliwa, imeonekana kwamba ubora ni sahihi, kinachodaiwa ni kwamba hawana fedha, basi wangewapa hata kidogo tu ili wajijenge kiuchumi kesho waweze kuwa suppliers wazuri zaidi. Kwa suala la nguzo naomba niseme hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, masuala haya yanayohusiana na suala la madini. Kule katika Jimbo la Njombe Mjini kuna mgodi wa madini katika Kijiji cha Uliwa. Mgodi ule ulisababisha ugomvi sana na wananchi kwa sababu tu leseni zilitolewa kwa watu wawili, wote wafanye utafiti katika eneo moja. Naomba sasa, kama utaratibu ndivyo unavyoruhusu, basi urekebishwe kwamba kama ni leseni inatolewa kwa mtu mmoja na idara hii inayohusika na leseni iwe inatoa kwa utaratibu mzuri ili kusaidia wananchi wale wasiingie kwenye mgogoro.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana, yuko mwekezaji mmoja yuko tayari pale kuchimba yale madini ya copper, basi mwekezaji yule apewe kibali aendelee na kazi kwa sababu anazunguka siku nzima, miaka inakwenda kazi haifanyiki; na wananchi wale hawajapata elimu ya kutosha kwamba je, ni utaratibu gani unatakiwa ufanyike ili waweze kupewa kitu kinachotakiwa, kama ni mrabaha wa kijiji au ni wa Halmashauri au wa nini. Matokeo yake ni kwamba wananchi wale wamesimama pale wanasema mwekezaji haingii na mwekezaji anasema nina leseni; na upande mwingine kuna sehemu kuna mwekezaji mwingine anasema naye ana leseni. Kwa hiyo, naomba sana Wizara isaidie uchimbaji wa yale madini katika Kijiji cha Uliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niseme nashukuru sana na naunga mkono hoja.