Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Hassan Selemani Kaunje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. HASSAN S. KAUNJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Lakini kwa utamaduni wa Kitanzania unapofanyiwa jambo jema ni vizuri ukatoa shukrani, na shukrani zangu za dhati, ziende kwa Profesa Muhongo, REA, TANESCO Lindi, lakini vilevile TANESCO zone ya Kusini kwa kushughulikia tatizo la umeme katika kata mbili za Ng‟apa na Tandangongoro ambazo zimepitiwa na bombala gesi lakini umeme ulikuwa haujafika. Wamelitatua tatizo hili na ninawashukuru na kuwapongeza sana kwa juhudi hizo walizozifanya.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ninataka nizungumze especially kwenye suala moja tu la LNG inayoenda kujengwa Lindi. Na ningemuomba Mheshimiwa Waziri anisikilize kwa umakini ninayotaka kuyazungumza kwa sababu, kuna ninayotaka kuyashauri ya msingi sana ambayo anapaswa kuyachukua kuanzia sasa anapoanza safari ya kuelekea katika uwekezaji wa kiwanda hicho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 35 wa hotuba yake ameomba tuidhinishe shilingi milioni 800, anaenda kufanya maandalizi ya uchoraji wa ramani ambayo itaingia katika Mipango Miji katika Manispaa ya Lindi ya kiwanda hiki anachotaka kujenga, lakini vilevile maandalizi ya uwanja wa ndege wa Lindi kwa ajili ya programu inayokuja. Sasa wakati anayafanya haya nimuombe Mheshimiwa Waziri aende sambamba na kulipa fidia kwa wakazi ambao wanaoondoka katika eneo ambalo litaguswa na mradi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nimuombe Mheshimiwa Waziri afanye yafuatayo katika eneo hilo, anaenda kuandaa mchoro wa kiwanda, ila eneo la Lindi Manispaa halina master plan ya Mji, kwa hiyo, aongee na Waziri mwenzie anayehusika na master plan wahakikishe master plan ya Mji wa Lindi inapatikana kabla ya michoro hiyo inayoenda kuandaliwa na kuingizwa haijaweza kufanyiwa kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo anaenda kuyafanya hayo anayotaka kuyafanya, atusaidie kutupelekea pesa zetu kwa kumwambia Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwamba zoezi la kuandaa mpango kamambe huu ambao ni master plan unakwama kutokana na kuzuiwa kwa zaidi ya shilingi milioni 700 ambazo ni retention money ambazo ziko kwake zinazotokana na uuzwaji wa viwanja. Tupelekee fedha hizi katika Manispaa ya Lindi, ili tuweze kuandaa mpango kamambe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, anapeleka mradi huu ambao unatarajiwa kupeleka zaidi ya wafanyakazi na watu wengine watakaokadiriwa kuwa 20,000 na Mji wa Lindi una watu takribani 100,000 kwa hiyo, unapopeleka watu 20,000 ni idadi kubwa ya watu. Lakini wananchi wa Lindi wana matumaini makubwa na mradi huu unaenda kutatua, historia yao inaenda kufutwa ya umaskini uliokithiri kupitia ajira zitakazotokana na mradi huu, lakini watu wa Lindi wana tatizo moja kubwa la kihistoria, umaskini wao ni pamoja na kukosa elimu, hawana elimu, yanayoendelea katika mradi huu hata yaliyoanza sasa hivi ajira zile ndogo ndogo za maandalizi wanashindwa kupata kutokana na kukosa elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini, anapopeleka kiwanda hiki ambacho ujenzi wake utakamilika sio chini ya miaka kumi kutoka sasa hivi, basi aungane na Waziri wa Elimu kuweza kuandaa mpango utakaowafanya wananchi wa Lindi waweze kuwa na sifa hitajika na kuingia katika ajira zitakazotokana na kiwanda hiki pale kitakapokamilika. Nasema hivi mpango uwe maalum kwa sababu Serikali kwa mara nyingine au mara zingine imeshawahi kuchukua hatua stahiki za kusaidia baadhi ya maeneo kutatua kero zinazowasumbua especially za elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona maeneo yale ya Wamasai ilipelekwa programu maalum ya kuwafanya wasome, lakini vilevile kwenye maeneo ambayo ukeketaji kulikuwa na shida, Serikali ilichukua jukumu maalum la kuhakikisha kwamba tatizo hili linaondolewa. Nimuombe yeye na Waziri husika na Serikali kwa ujumla, wananchi wa Lindi walio wengi hawana elimu na uwezo wa kuweza kufanya kazi katika kiwanda hiki kitakapokamilika, tuwasaidie kwa kuanza na programu hii anapoanza sasa kuelekea kule kukitengeneza kiwanda hiki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tulisimama hapa Mbunge mwenzangu wa Nachingwea, aliomba Mheshimiwa Waziri wa Viwanda apeleke wawekezaji watakaoweza kuwekeza processing ya samaki kwa sababu tuna ukanda wa kilometa 112 Lindi Mjini ambazo ni za bahari. Na kwa bahati nzuri Mheshimiwa Waziri alisema tusiwahishe shughuli anatuletea kwanza viwanda vya mihogo; lakini lengo letu la kuzungumza viwanda vya samaki tunamaanisha kwamba kuna wavuvi ambao watahitaji soko lile na kwa sababu tunapeleka watu ambao watakuwepo katika kiwanda hiki, tunapaswa tujipange na tuwawezeshe wavuvi hawa waweze kuwa na soko la uhakika, ili waweze sasa na wao kuingia katika uchumi unaoenda wa kiwanda hiki cha gesi. Nimuombe basi, amwambie Waziri pamoja na kiwanda cha mihogo ambacho anatupelekea, basi atusaidie kutupelekea watu watakaowekeza katika sekta ya samaki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika eneo lingine. Eneo hili nataka nishauri kwa ujumla katika mambo yanayohusu uchumi wa Taifa ambao unaendana na Wizara hii ya Nishati na Madini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ununuaji wa mafuta wa jumla ambao kwa kifupi unaitwa BPS. Na katika uagizaji ule wa mafuta makampuni yanayoleta mafuta ambayo yana zabuni ile mengi yamekuwa registered nje ya Tanzania.
Matokeo yake kwamba makampuni yale yanakwepa baadhi ya kodi ambazo zingepaswa kulipwa kama tu wange-register BRELA, Tanzania. Nimuombe Mheshimiwa Waziri alifanyie kazi jambo hili, ili kampuni hizi zinazoingiza mafuta ziweze kulipa kodi stahiki ambazo zitaendeleza Taifa letu la Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo kuna jambo la vinasaba vya mafuta vinavyowekwa katika mafuta tunayoyatumia. Jambo hili linapigiwa kelele na wadau tofauti, wazo langu ni lifuatalo; Mheshimiwa Waziri lengo la kuweka vinasaba katika mafuta tunayoyatumia ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na mafuta salama kwa ajili ya vyoimbo vyetu. Kuna wadau wanaozungumza kwamba jambo hili si zuri. Tunaweza tukaungana nao mkono, lakini tutaungana nao mkono tu pale tutakapohakikishiwa usalama wa vyombo vyetu, hivyo nimshauri Mheshimiwa Waziri jambo hili liendelee mpaka suluhu yake itakapopatikana na kuonekana jambo hili linaweza kutatuliwa kwa namna nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyazungumza haya nimuombe Mheshimiwa Waziri asiponijibu vizuri lini atawalipa fidia wananchi wa Mbanja, wananchi wa Likong‟o, wananchi wa Kikwetu kupisha ujenzi wa kiwanda chake, nakusudia kuondoa Shilingi katika bajeti yake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa wasaa huu wa kuchangia katika Wizara hii. Ahsante sana.