Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Magdalena Hamis Sakaya

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Kaliua

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ninakushukuru kunipa nafasi niweze kuchangia hotuba ya Wizara ambayo iko mbele yetu. Kwa sababu ya muda nichangie moja kwa moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka zaidi ya 15 sasa tumekuwa tunashuhudia tunajadili hapa Bungeni suala la makaa ya mawe, tangia sijawa Mbunge alikuwepo Profesa alikuwa anaitwa Profesa Mwalyosi ndani ya Bunge hili, kila akisimama ndani ya Bunge nilikuwa nasikia anazungumzia Mchuchuma, Liganga, makaa ya mawe miaka iliyopita, alikuwa ni Profesa wa mimea na mazingira. Leo nimeingia ndani ya Bunge miaka 10 tunazungumza makaa ya mawe, ni kwa nini tunashindwa kutumia makaa ya mawe kwa ajili ya nishati ya matumizi ya nyumbani? Tunaomba Mheshimiwa Waziri akija atueleze kuna tatizo gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii inaenda kuwa jangwa, hatuna means, kwa sababu umeme haushikiki, hata Mheshimiwa Waziri hawezi kupikia umeme. Mafuta ya taa hayashikiki, gesi haishikiki, tunachemshia vitu vidogovidogo tu, asilimia 80 tunatumia mkaa, nchi inakuwa jangwa. Kama kwa mwezi mmoja Dar es salaam peke yake wanatumia magunia 200,000 kwa takwimu za Waziri can u imagine nchi nzima tunatumia gunia ngapi kwa mwezi mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipoangalia tunaenda kuwa jangwa, lakini tunashangaa tumepewa makaa ya mawe ndani ya nchi yetu, kuna tatizo gani Mheshimiwa Waziri, tunaomba kesho utujibu hapa, kwa nini hatuoni umuhimu wa kutumia rasilimali hii tuliyopewa ndani ya nchi yetu tutoe nishati kwa ajili ya kuitumia, naomba sana Mheshimwa Waziri atuambie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ilikwenda Likuyu - Namtumbo mwaka juzi, nilikaa pale Namtumbo karibu siku tatu, jambo la kushangaza niliona malori zaidi ya 100 kila siku yanabeba makaa ya mawe, kwanza napenda kujua yanapelekwa wapi cha kwanza, Mheshimiwa Waziri uniambie, yale makaa ya mawe, yanayotoka Namtumbo, malori 100 kila siku yanapelekwa wapi, kwa sababu kwa takwimu ambazo nilijaribu kuuliza wananchi pale wanasema wanakwenda Uganda nan mengine yanakwenda Kenya. Nikawa nashangaa kama malori 100 yanabeba makaa ya mawe kutoka Namtumbo, rasilimali ya nchi yetu, leo tunaendelea kuteketeza misitu yetu, are we serious?
Naomba uje utuambie yanakwenda wapi, na wale wananchi pale wananufaikaje na sisi kama Tanzania tunanufaikaje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la Wizara ya Madini na Nishati kutoa leseni za kutafuta madini kwenye maeneo ya hifadhi…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilindie muda wangu, ahsante.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwepo na utaratibu ambao kunakosekana coordination kati ya Wizara ya Madini na Nishati na Wizara ya Maliasili. Wizara ya Nishati na Madini inatoa leseni za utafutaji wa madini ndani ya maeneo ya hifadhi, kwa hiyo imeleta migogoro mingi sana. Kuna baadhi ya maeneo ya hifadhi ambayo mpaka sasa hivi kuna migogoro mikubwa sana mojawapo ni Hifadhi ya Manyara. Wamepewa leseni ndani ya hifadhi, hakuna coordination matokeo yake leo kuna migogoro ambayo haiishi. Kwa hiyo, tungependa wakati Wizara inatoa leseni za kutafuta madini kuwepo na coordination kati ya Wizara hizi mbili ili kuondoa migogoro ambayo inatokea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nimeangalia kitabu cha Mheshimiwa Waziri, tuna madini ya Uranium ambayo tunachimba maeneo mengi sana ya Tanzania, napenda kujua haya madini ya Uranium maeneo gani yameanza kuchimbwa, maeneo gani yanafanya kazi, maeneo gani na tunanufaikaje na madini hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, nilitembelea Mgodi ule wa Uranium kule Likuyu Namtumbo, tuliona jinsi ambapo kuna Uranium nyingi iko nje, tulitembea pale wanaita yellow cake, iko peupe ni ya kukusanya. Kwanza ningependa kujua ule mgodi umeshaanza kufanya kazi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, tunanufaikaje kama Watanzania na lingine wananchi wa eneo lile wananufaikaje na ule mgodi kama umeshaanza kufanya kazi. Maana naona kimya, nilikuwa nategemea angalau tuone huku kwenye kitabu cha hotuba ya Waziri, sioni chochote ambacho kimeandikwa huku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la REA, kiukweli kwenye sula la REA kwa kiasi fulani limesaidia sana umeme kusambaa, lakini bado changamoto zake ni kubwa sana. Suala la REA kila Mtanzania anashiriki kwa fedha ya REA, hata bibi wa kule kijijini kabisa akinunua lita moja ya mafuta ya taa tayari kasaidia mchango wa REA kuendelea kuwepo kwa kukatwa shilingi 150. Jambo la kushangaza kwa nini fedha zile hazielekezwi zote maeneo yaliyopangiwa?
Mheshimiwa Waziri hebu kesho utuambie, zile fedha ambazo hazikutumika kwa hii miaka mitatu hazikupelekwa kwenye REA zimeelekezwa wapi na ni kwa sababu gani? Kwa sababu kupanga ni kuamua, kama tumeamua kutengeneza mradi wa kusaidia umeme vijijini, tumeamua kama Watanzania, tunawakata kwenye mafuta, kwanye diesel, petrol, na kwenye mafuta ya taa. Tuwe na nidhamu basi ya matumizi ya hizi hela.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli kama Wabunge wengine walivyosema, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri alikuja kwenye Jimbo langu la Kaliua, namshukuru Mheshimiwa Waziri, kiukweli alikuta hali ni mbaya. Wakati anakuja katika Jimbo la Kaliua tulikuwa na asilimia moja tu ya usambazaji wa umeme wa REA katika Wilaya nzima mpaka alishtuka.
Nashukuru baada ya kuwepo kwake alisukuma watendaji wake angalau shughuli zimeanza kwenda lakini Mheshimiwa Waziri uliagiza tarehe 30 mwezi wa nne, umeme wa awamu ya kwanza na ya pili uwake, mpaka leo ni kijiji kimoja tu kinawaka umeme, hivyo, bado tunayo changamoto nyingi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, REA inahitaji ufuatiliaji wa hali ya juu, siyo suala kwamba watendaji wa TANESCO wanawaachia wale makandarasi hapana. Nimeona mfano mmoja Kaliua, Mameneja walikuwa wamekaa ofisini hawafanyi kazi, walivyonyanyuka kutoka ofisini kuwafuata makandarasi leo kazi inafanyika.
Kwa hiyo, watu wa TANESCO watoke maofisini waende kwa makandarasi wahakikishe kwamba wanawasimamia, makandarasi wale wanapoachiwa peke yao wanafanya wanavyotaka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukiangalia nguzo zinazopelekwa kwenye maeneo ya vijiji ni chache sana, wanasambaza barabarani mwa kijiji au makao makuu ya kijiji, vitongoji vyote hakuna umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Serikali na Watanzania ni kila Mtanzania anayetaka kutumia umeme atumie umeme, siyo maeneo ya barabarani, ni lazima pia umeme uende mpaka maeneo ya vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni migodi mikubwa ya dhahabu kutolipa Kodi ya Mapato. Leo nimesikia kauli ya ajabu, eti wanasema watu wa migodi wamekuwa wanapata hasara endelevu. Sijawahi kusikia hasara endelevu. Hakuna mfanyabiashara yeyote duniani, hata kama ni mama ntilie akubali kupata hasara endelevu. Kama wanapata hasara endelevu, kwa nini waendelee kuwepo? Kama wanapata hasara endelevu, kwa nini waendelee ku-run? Wanakuwaje na watumishi? Wanakuwaje na kila kitu? Hapa ni wizi mtupu. Tunataka migodi yote ilipe kodi. Tumekuwa tunayabeba sana makampuni. Leo kama Tanzania hatunufaiki sana na migodi yetu ya madini kwa sababu wanabebwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba ya Mwenyekiti wa Kamati, wametuambia kwamba kuna makampuni yanayodaiwa shilingi bilioni kadhaa. Makampuni ambayo hayakulipa Kodi ya Zuio yanadaiwa shilingi bilioni 89 lakini kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri anasema Acacia wamelipa almost karibu shilingi bilioni 13. Sasa hebu tujue, Mheshimiwa Waziri utuambie, kwanza haya makampuni mengine ambayo hayakulipa, umesema kuna makampuni matatu hapa ambayo hayakulipa, wamelipa tu Acacia kidogo, yale mengine tunayafanyaje, ikiwepo Mantra na hao wengine Tanzania One?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini hawakulipa na ni kwa sababu gani? Kwa nini Mheshimiwa Waziri hajatueleza kwenye kitabu chake kwamba wanafanywaje? Kwa sababu ametuambia tu wamelipa Acacia kiasi kidogo. Kwanza Acacia hawajamaliza, tunataka walipe kodi yetu yote, lakini yale ambayo hawajalipa, tunawafanyaje? Mheshimiwa Waziri, tuache kuwabeba, wanatunyonya, hii rasilimali ni yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni la wachimbaji wadogo wadogo. Kwenye Jimbo langu ninayo machimbo ya madini ya dhahabu kwenye eneo la Ulyankulu, machimbo ya Silambu. Tulikubaliana hapa Bungeni Serikali iwezeshe wachimbaji wadogo wadogo, kuwapatia maeneo lakini pia wapatiwe mitaji, pamoja na vitendea kazi. Bado halitekelezwi kama tulivyokuwa tumekubaliana, bado wana hali ngumu ya utendaji wao wa kazi, bado wanahangaika hapa pale, wamekuwa ni watu wa kufanyia kazi kama za utumwa, wanatumika tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunaomba sana, Serikali inajua na Mheshimiwa Waziri anajua, anawajua wote wako wapi na vitalu vyao, hebu wekeni utaratibu wa kuwawezesha, waweze kunufaika na ile kazi yao wanayoifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, ndani ya Wilaya yangu ya Kaliua, Kata ya Igwisi, Kijiji cha Twende Pamoja, kuna machimbo ya madini ya mawe, yanachimbwa na kampuni ya CHICO. Kampuni ya CHICO imechimba pale karibu miaka mitatu wanatengeneza kokoto, hawajawahi kulipa chochote kwenye kata ile wala kwenye kijiji kile, lakini kikubwa kuliko yote, kuna nyumba zaidi ya 25 hazijalipwa, baruti zinapasuliwa usiku na mchana, wananchi wale wengine wanateseka, wengine wanazimia, hawajaweza kuhamishwa, lakini wapo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipofuatilia kwa CHICO anasema, sisi tuna-deal na watu wa madini. Sasa Mheshimiwa Waziri utusaidie, pale kampuni inapopewa mlima, pale ni mlima wamesambaratisha mlima wote umekwisha, wananchi wanateseka. Hakuna hata coin moja ambayo wamewahi kulipa. Tunaomba Mheshimiwa Waziri ukija kujibu utuambie, wale kampuni ya CHICO ambao mmewapa mlima wa pale Twende Pamoja, Igwisi, wamechimba miaka mitatu, wanatengeneza kokoto, kwa nini hawalipi ushuru unaotakiwa kwa kijiji husika na kwa Halmashauri? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni kwa nini mpaka leo hawalipi watu haki zao? Wawaondoe pale. Nilishawahi kukuta mwanamke amezimia pale, mpaka kijiji kwa huruma, wakamhamisha wakampeleka sehemu nyingine. Wananchi wa kawaida, lakini Serikali ipo na sheria iko wazi kwamba pale unapotaka kutumia eneo kwa ajili ya matumizi mengine, lazima watu wapewe haki zao waondoke. Makanisa, mawe yanadondoka mpaka ndani ya kitanda cha mtu. Makanisa...
MWENYEKITI: Ahsante kwa mchango wako.