Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kunipa nafasi hii nichangie Wizara hii muhimu ya Nishati na Madini. Nianze juu ya umeme katika Mkoa wa Katavi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Katavi una umeme usio na uhakika. Nilikuwa naomba Wizara kupitia Waziri aangalie umuhimu wa kuboresha miundombinu ya umeme katika Mkoa wa Katavi. Mkoa huu umekuwa ni chaka la kupelekewa zana zile ambazo zimetumika katika baadhi ya maeneo zikichoka wanapeleka Mkoa wa Katavi. Ninaomba Mheshimiwa Waziri atambue kwamba Mkoa wa Katavi ni sehemu ya Tanzania na wote wanastahili kupata stahili ya mgawanyo wa keki ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba mradi wa Orion ambao ulikuwa unaunganisha Mkoa wa Katavi baada ya Wilaya ya Biharamulo na Ngara tunahitaji sana ule mradi upelekewe fedha ili uweze kutoa umeme wenye uhakika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni umeme vijijini, eneo hili bado kuna ubaguzi ambao unatolewa katika baadhi ya maeneo. Mkoa wa Katavi ni baadhi ya maeneo ambayo yana vijiji vichache sana ambavyo vimepelekewa umeme, Jimboni kwangu sina hata kijiji kimoja ambacho kimepelekewa umeme vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme wa Phase II. Nilikuwa na kijiji cha Kabungu, Mchakamchaka, Ifukutwa, Igalula na Majalila, bahati mbaya mpaka Phase II inakwisha bado huo umeme haujafika. Kwenye eneo la Phase III limetengewa vijiji 49, ninaomba hivyo vijiji vipelekewe umeme ikiunganishwa na vile vijiji ambavyo havikupata awamu ya kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo ya msingi ambayo yanahitaji kuboreshwa kupelekewa umeme vijijini, hasa maeneo ya Ukanda wa Ziwa. Eneo la Ukanda wa Ziwa lina vijiji vya Kapalamsenga, Itunya, Karema, Ikola, Kasangantongwe na vijiji ambavyo viko jirani vinahitaji kupata umeme kwa sababu kuna maeneo ya uzalishaji mali. Upo utafiti unaofanywa wa mafuta kwenye maeneo hayo lakini kuna shughuli za uvuvi zinazofanywa na wananchi katika kata hiyo na tarafa ya Karema kwa ujumla naomba vijiji hivi vipewe kipaumbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipate majibu ya uhakika kwenye vile vijiji ambavyo vilikuwa vimelengwa kwa awamu ya kwanza na muunganisho wa vijiji vya tarafa ya Mishamo ambapo kuna vijiji 16 havina hata kijiji kimoja ambacho kimepata umeme vijijini, naomba vijiji vya Bulamata, Kusi, Kamjela, Ifumbula na vijiji vya eneo la Isubangala, Ilangu, tunahitaji vipewe umeme ambao ni muhimu uwasaidie wananchi katika maeneo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi umeanzishwa ambao ungesaidia eneo zima la Mkoa wa Katavi na Mkoa wa Kigoma, Mradi wa Umeme wa Malagarasi, ungekuwa suluhisho la umeme wa uhakika. Bahati mbaya sana eneo lile la Malagarasi kuna vitu ambavyo vinaelezwa huwa tunashindwa kuwaelewa, kinapozungumzwa unashindwa kuelewa kwamba Serikali ina maana gani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kuna vyura, hawa vyura wamekuwa na thamani kubwa kuliko hata mahitaji ambayo yanaweza yakawasaidia wananchi. Umeme ule ambao ungefungwa mradi mkubwa ungesaidia Mkoa wa Kigoma na ungesaidia Mkoa wa Katavi kwa ujumla. Naomba Serikali ije na majibu ya msingi; je, mpaka sasa uwepo wa wale vyura kwenye maeneo yale umetoa tija kwa Taifa hili kwa kiasi gani? Tuambiwe kwamba kuna thamani ya fedha imetolewa kubwa ambayo inazidi kuleta ule mradi ambao ungetusaidia wananchi kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia nizungumzie suala la utafiti wa mafuta kwenye Ziwa Tanganyika. Eneo la Karema ni eneo ambalo limekuwa likifanyiwa utafiti, lakini mpaka sasa hivi hatujajua kinachoendelea kwani baada ya tafiti na wale waliokuwa wanatafiti hawapo kwa sasa. Wananchi bado wanaangalia ni nini ambacho kitafanyika na walikuwa tayari kutoa baadhi ya maeneo kwa ajili ya kupata utafiti ule wa mafuta na gesi katika Ziwa Tanganyika. Sasa mpaka saa hizi hatujui ni kitu gani ambacho kimefanyika na kina tija ipi kwa wananchi wa maeneo yale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la madini. Jimboni kwangu kuna miradi ya madini ya dhahabu kwenye Kata ya Katuma na kwenye Kata ya Kapalamsenga kuna machimbo ya shaba; nilikuwa naomba Serikali inawasaidia vipi hawa wachimbaji wadogo wadogo? Kwani wachimbaji wadogo wadogo wamekuwa kama yatima ambao hawasaidiwi na Serikali kwa karibu ili waweze kupata manufaa ya machimbo yale ambayo yanafanywa ili yaweze kuwanufaisha wachimbaji. Naiomba Serikali iandae mazingira ya kuwasaidia hawa wachimbaji wadogo wadogo ili waweze kunufaika na machimbo ambayo yapo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijue kuhusu mradi wa shaba ambao uko Kata ya Kapalamsenga, naiomba Serikali ije na majibu mpaka sasa ule mradi unawanufaisha vipi wananchi? Wawekezaji wamekuja wamewekeza pale lakini hakuna mrahaba wowote unaopatikana kuwapa manufaa wananchi wanaozunguka kwenye maeneo yale na bado hata Halmashauri ya Mpanda hawajapata fedha za kuwanufaisha kutokana na madini yale yanayochimbwa. Niombe sana Serikali ije na majibu ya msingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nasisitiza Wizara iangalie umuhimu wa kuweka uwiano ulio sawa kwenye Mikoa iliyosahaulika hasa Mikoa ya pembezoni. Miradi mingi hasa ya umeme vijijini bado imekuwa ikielekezwa kwenye maeneo ambayo wao wana miradi mingine, wanaongezewa mradi juu ya mradi. Tunaomba vijiji vya Wilaya ya Mpanda kwa ujumla vipewe miradi ya umeme ili iweze kuwasaidia na sehemu hizo zifunguke.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.