Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia bajeti iliyoko mbele yetu. Nitamke bayana kabisa kwamba naunga mkono bajeti hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa karama hii ya uhai na kwamba leo napata fursa ya kuzungumza ndani ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nizungumzie eneo la REA, nitumie fursa hii kupongeza kazi kubwa iliyofanywa na wenzetu wa REA, imefanyika kazi kubwa sana, kazi ambayo ripoti inaonesha kwamba tumefikia kupeleka umeme vijijini sasa kwa asilimia 40, ni jambo zuri. Wakati tumefanya kazi hii vizuri ni ukweli vilevile kwamba zipo changamoto kubwa sana katika utekelezaji wa miradi hii ya REA. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Nishati, kwa hiyo nilipata fursa ya kuzungukia miradi ya REA, vilevile nina hazina ya uzoefu kwa miradi ya REA kule kwenye Jimbo langu. Kubwa tuliloliona ni kwamba kuna changamoto kubwa sana ya kusimamia utekelezaji wa miradi hii. Maeneo mengine yamerukwa kwenye vitongoji, maeneo mengine vijiji vimerukwa bila sababu za msingi na maeneo haya ni maeneo ambayo awali yalikuwemo kwenye mpango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilayani kwangu vipo vitongoji vimerukwa na bahati mbaya sana vitongoji vilivyorukwa wananchi wamekatiwa mazao yao ili umeme uweze kufika, mimea imekatwa hakuna fidia, lakini mwisho wa siku wanakosa umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano na hili Naibu Waziri analijua kwa sababu nililisema tukiwa kweye Kamati, kijiji ninachotoka mimi zimepelekwa nguzo 15, hivi nguzo 15 zinapelekaje umeme kwenye kijiji? Sasa matokeo yake taasisi muhimu kama zahanati, sekondari, shule za msingi zimekosa huduma hii, ukiacha wananchi ambao wamekatiwa mazao yao. Nadhani hii siyo sahihi tujitahidi katika kusimamia ili tuondokane na kero hii ya wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeliweka tena eneo hili la Kata ya Kigongoi kwa matumaini kwamba linaingia kwenye REA Awamu ya Tatu. Hivyo, naomba miradi hii ya REA tuisimamie iende vizuri, mapungufu yote ambayo yameonekana sasa yasije yakaathiri utekelezaji wa REA Awamu ya Tatu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haingii akilini, kwamba umeme unapelekwa kwenye kijiji lakini wananchi wanaambiwa umeme ulioletwa hauwawezeshi ninyi kuendesha mashine za kusaga unga na mambo kama hayo, tufanye marekebisho, tufanye usimamizi wa karibu ili changamoto hizi ziweze kuondoka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine linalokwenda sambamba na hilo ni kukatika umeme katika maeneo ya Mkoa wa Tanga, nilisema hapa eneo la Maramba, mwenzangu Majimarefu akazungumzia kule Korogwe, dada yangu Chatanda akazungumzia Korogwe Mjini na Waziri akatuambia kwamba upo mradi mkubwa wa kuboresha upatikanaji wa umeme, naomba jambo hili lisimamiwe kwa karibu ili tuondokane na tatizo hili.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kwenye eneo la uchimbaji wa madini ya graphite. Taarifa zilizopo sasa zinasema Tanzania itakuwa miongoni mwa Mataifa makubwa yanayozalisha graphite, tutakuwa ndani ya nchi kumi zinazozalisha graphite ulimwenguni. Wakati tukielekea huko nataka tujiulize, tumejipanga namna gani kusimamia eneo hili ili yasije yakatukumba kama yaliyotokea malumbano wakati tunaenda kwenye uchimbaji wa dhahabu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwnyekiti, taarifa zilizopo ni kwamba tayari wapo wajanja wachache ambao hawastahili kuajiriwa kwenye sekta hii, makampuni ya nje yamewaajiri watu ambao vibali vyao vinatia mashaka kuajiriwa kwenye sekta hii, taarifa zilizopo zinasema wapo watu wameajiriwa kwa fani ambazo Watanzania wanaweza kuzisimamia. Hivi inakuwaje leo tunaajiri mtu wa sekta ya ununuzi kutoka Australia, kwamba Watanzania hawapo wenye uwezo wa kusimamia mambo haya? Mheshimiwa Waziri naomba tufanye due diligence katika mambo haya ili tusije tukaingia kwenye matatizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo taarifa kwamba ipo kampuni imepewa leseni, kampuni hiyo tunaambiwa inatoa asilimia tano ya hisa kwa Tanzania, madini yetu tunapewa asilimia tano, mimi sitaki kulikubali hilo, lakini kama ni kweli Mheshimiwa Waziri hebu lifuatilie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni madini ya vito. Tumelizungumza kwenye Kamati tukajielekeza moja kwa moja kwenye Tanzanite, ripoti za kitafiti duniani zinaonesha kwamba madini ya vito asilimia 50 yanazalishwa kwenye ukanda wa Afrika Mashariki. Lakini kwa bahati mbaya sana nchi hizi zimeshindwa kunufaika ipasavyo kwenye madini haya, hapa ndipo linapokuja suala la Tanzanite, tumezungumza kwenye Kamati nini cha kufanya, naiomba Serikali imuelekeze Mkaguzi na Mthibiti Mkuu Hesabu za Serikali aende akafanye ukaguzi maalum kule Tanzanite ili ripoti hiyo ituwezeshe Bunge kuishauri Serikali ipasavyo, hatujanufaika na Tanzanite. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu yangu Lema pale anasema, sasa jamaa wameondoka kutoka kununua Arusha, Tanzanite inafungashiwa Mombasa, nataka wakati tukiyasikia haya turudi kwenye tafiti, taarifa ya Umoja wa Mataifa inasema nini, taarifa ya Umoja wa Mataifa inasema madini haya gemstone ndiyo imekuwa kichaka cha magaidi, kujificha kwenye jambo hili. Sishangai kusikia kwamba badala ya watu wale kuwa Nairobi sasa Tanzanite inafungashiwa Mombasa, nikisema hivi nafikiri mnaelewa ninasema nini, tuyasimamie madini yetu vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni EWURA, tulifanya uamuzi wa kuanzisha EWURA na tulipoanzisha work load ya sekta ya nishati haikuwa kubwa sana, kwa hiyo ilikuwa ni sahihi pengine EWURA kusimamiwa na Wizara ya Maji. Sasa workload ya upande wa nishati imepanuka sana, nadhani siyo sahihi kuendelea kuiacha EWURA ikasimamiwa na Wizara ya Maji, nafikiri busara itumike, Mheshimiwa Rais ashauriwe ili ile instrument inayoelekeza EWURA kusimamiwa na Wizara ya Maji sasa ibadilishwe na hata ikibidi EWURA igawanywe, tuwe na kitengo kinachosimamia sekta ya nishati ibaki Wizara ya Nishati, na ile inayoshughulikia sekta ya maji ibaki Wizara ya Maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni matumizi ya gesi, tumekuwa tukijielekeza kwenye matumizi…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.