Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipa fursa kuongea kwenye sekta hii muhimu kwa uchumi wa nchi na kwa maslahi ya watu binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote kwa kazi nzuri wanayoifanya kuangaza Tanzania na kuleta maendeleo kwa Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana kwa sababu muda ni mfupi ningependa kushukuru watu wengi lakini niende moja kwa moja kwenye mambo ambayo ni pressing kwa Wilaya yangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti,Mkoa wa Manyara ni Mkoa wa kilimo na Wilaya ya Hanang ni Wilaya ya kilimo na ufugaji. Umeme wa REA namba moja ulitpelekwa kwa vijiji vinne tu Wilaya ya Hanang na mpaka leo vijiji vile vinne bado havijapata umeme, naomba Mheshimiwa Waziri atueleze vijiji hivyo vitapata umeme lini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu tulipata vijiji vichache wakati Wilaya za jirani zinapata zaidi ya 20, zaidi ya kumi nikamwomba vijiji 19 na yeye akaniahidi, naomba uwahakikishie watu wa Hanang kwamba Hanang nayo inathaminiwa kwa hivyo vijiji 19 kuweza kupata umeme na orodha nimekupa. Kwa ajili ya muda mfupi nisingependa kupoteza muda. Ninaomba uone umuhimu wa Wilaya moja kwa REA zote tatu sasa tunaenda kwenye REA tatu imepata vijiji vinne na nafikiri utaona umuhimu wa kuona kwamba Mbunge akilia hapa ana sababu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Tanzania ni nchi iliyojaaliwa kuwa na vyanzo vingi vya nishati, siwezi kuvitaja kwa kuwa mnavijua, lakini ninafikiri gharama ya kupata nishati kwenye chanzo kimoja vinatofautiana na vingine. Na miaka ya awali ya Tanzania tulikuwa tunapata umeme kutokana na maji. Tabianchi ilipoanza kubadilika tukakumbwa na ukame tukapatwa sasa na dharura za kukimbilia kuweka umeme wa dharura. Mimi nafikiri sasa wakati umefika wa kuwa na mkakati mzuri. Ninajua kuna power master plan, lakini ninaomba sana tuangalie mix ya hiyo power master plan kusudi gharama iwe baadaye si kubwa kwa watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwamba tusifikirie vidogo vidogo, mmefanya kazi kubwa, kuna Kinyerezi I, Kinyerezi II, Kinyerezi III mnafanya kazi nzuri na kuna vyanzo vingine ambavyo mnashughulikia. Mimi bado naamini tufikirie vikubwa na mimi nafikiria hakuna umeme ambao utaokoa Tanzania kama siyo ule wa Stigler’s Gorge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Stigler’s Gorge unaweza ukatoa umeme wa kilowatts 2100, tukijielekeza huko wakati wa master plan nimeona Stigler’s Gorge iko kwenye master plan lakini iko mbali. Naomba muilete karibu kusudi tuwe Taifa la kufikiria vitu vikubwa. Nitakushukuru sana, najua una uwezo na ukiamua hilo unaweza ukalifanya vizuri na mimi sina wasiwasi, ninajua wakati wa dharura dharura ile ndipo tulipoingia kwenye IPTL, kwenye DOWANS na mambo ambayo yalileta madhara makubwa kwa Taifa letu.
Kwa hiyo, sasa ni wakati mzuri wa kufikiria kwamba katika ile master plan tuwe na mkakati ambao utajielekeza kwenye kuona kwamba tumeamua kuwa nchi ya viwanda na uchumi wa kati. Bila kuwa na umeme wa hakika huko hatutafika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilifikiria kwamba Mkoa wa Manyara ndipo ambapo Mererani ipo. Kutokana na Tanzanite ya Mererani Wilaya ya Simanjiro ikatoa eneo la EPZA bure na wengine wote wanadai fidia.
Ninaomba sana tuangalie Mererani na tuone jinsi ambavyo tutaweza kuongeza thamani ya Tanzanite kwa kuweka viwanda ili tuweze kuwa na faida ya Tanzanite kuliko inavyoonekana sasa Tanzania ni nchi ya tatu. Tukifanya hivyo tutakuwa tumeleta manufaa makubwa ya vito ambavyo vimeletwa na Mwenyezi Mungu nchini kwetu na Mkoa wa Manyara ambao hauna resources nyingi isipokuwa ardhi yenye rutuba. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana nirudie tena kwamba naomba Wilaya ya Hanang iletewe umeme kwenye vijiji nilivyosema ili tuongeze thamani ya mazao ya kilimo, thamani ya mazao ya mifugo na watu ambao zamani ndiyo walikuwa nyuma kuliko wengine wamekubali kukimbia muwawezeshe kukimbia kuwakuta watu wa Kilimanjaro na Arusha. Mkoa wa Manyara umejigawa kwa sababu tulikuwa nyuma sana na kwa ajili ya Arusha tukawa tunaonekana tumeendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa tuingie kwenye huo mkakati wa kuendelea wa kutuletea umeme na wewe ndiye utakuwa savior, ninakushukuru, ninakupongeza na Mwenyezi Mungu atakupa nguvu zaidi na kuendelea kuwa kwenye hii Wizara, maneno yapo, Upinzani wanasema wao wanaisimamia Serikali naomba tukumbushane hapa kwamba ni jukumu la Wabunge wote pamoja na wale wa CCM kuishauri na kuisimamia Serikali, siyo kazi ya Wapinzani tu. Na sisi ndiyo tuna wajibu mkubwa wa kuishauri na kuisimamia Serikali yetu kuliko ninyi, Ilani ya Uchaguzi ni yetu na kwa hivyo lazima tuisimamie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kama dakika zangu hazikuisha wengine nao wanufaike. Ahsanteni wote.