Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Pia naomba nichukue nafasi hii kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kujiunga katika Bunge hili na nimshukuru zaidi Mwenyezi Mungu kwa sababu amerahisisha safari yangu ya kutoka kwenye Utumishi wa Umma na kuingia kwenye Ubunge kwa sababu nilipita bila kupingwa, kwa hiyo Ubunge wangu ulianza tangu tarehe 21 Agosti, 2015 wale wenzetu wa upande mwingine hawakurudisha form. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nichukue nafasi hii sasa, kumpongeza Waziri wa Mipango Dkt. Philip Mpango, na Watumishi wenzake, ambao wametuletea mapendekezo ya Mpango na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ambao wote tunauona unafaa, unatoa matumaini mapya na ni kweli Tanzania yenye viwanda inawezekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu, utajikita kwenye maeneo ya vipaumbele. Eneo la kwanza ni lile la kutangaza Mtwara kuwa eneo la uwekezaji, naomba niishauri Serikali, unapozungumzia Uchumi wa Gesi, huwezi kutofautisha Mtwara na Lindi. Kwa hiyo, naomba vilevile Lindi uangaliwe uwezekano na yenyewe kuwekwa kama eneo maalum la uwekezaji, kwa sababu unapozungumzia uchumi wa gesi na mafuta unazungumzia Mtwara na Lindi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikizungumzia Mtwara ambapo kumetangazwa eneo la uwekezaji kuna changamoto nyingi sana ambazo naomba tupeleke rasilimali za kutosha ili eneo hili litumike ipasavyo. Kwanza kuna ujenzi wa bandari, fedha za kutosha zipelekwe kwa ajili ya upanuzi wa bandari yetu ya Mtwara.
Pili, kama walivyosema wachangiaji waliyopita kuna suala la uwanja wetu wa Ndege wa Mtwara ukabarati umefanyika miaka ya nyuma sana, uwanja huo sasa hivi wa Mtwara hauna taa na hivyo Ndege haziwezi kutua au kuruka usiku, sasa eneo gani la uwekezaji ambao unaweka masharti kwamba Mwekezaji afike mchana tu usiku hawezi kuingia, kwa hiyo turekebishe kasoro hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, kuna ujenzi wa reli ya Mtwara Bamba bay na mchepuko wake ule wa kwenda Liganga na Mchuchuma. Reli hii imesemwa tangu siku nyingi sasa muda umefika tutekeleze, kwa hiyo naomba Serikali yetu sikivu ya awamu ya tano ihakikishe kwamba inatenga fedha za kutosha ili Mradi huu sasa uanze. Ni aibu kwa sababu Mwekezaji wa Kiwanda cha Dangote analeta sasa malighafi ya mkaa toka nchi za nje wakati tuna mkaa wa kutosha toka Mchuchuma ni vizuri reli hii ijengwe ikamilike ili Dangote aanze kutumia rasilimali za humu humu nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna suala la hospitali ya Rufaa ya Kanda ya kusini. Wawekezaji watapenda kujihakikisha masuala ya uhakika wa afya zao. Kwa hiyo, naomba ujenzi wa hospitali ya Rufaa ya Kanda yetu ya Kusini nashukuru ujenzi umeishaanza na kama alivyojibu Naibu Waziri wakati ule wakati anajibu swali la nyongeza alisema kwamba jengo la wagonjwa wa nje linakaribia kukamilika, tunaomba fedha za kutosha zitengwe ili hospitali hiyo Rufaa ikamilike mapema ili isiwe kikwazo kwa Wawekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ili Mji wetu wa Mtwara uweze kuwa kivutio cha Wawekezaji tunaomba barabara ambazo zinaunganisha Wilaya za Mkoa wa Mtwara nazo zijengwe kwa hadhi ya lami, kuna barabara maalum barabara ya uchumi, barabara ya korosho, Mtwara, Nanyamba, Tandahimba, Newala Masasi. Barabara hii inasafirisha asilimia themanini (80%) ya korosho ya Tanzania. Kwa hiyo Barabara hii ni muhimu na lazima zitengwe fedha za kutosha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili utajikita kwenye zao la korosho. Hapa nitazungumzia changamoto zilizopo kwenye Mifuko yetu miwili kwanza kuna Mfuko wa Kuendeleza Zao la Korosho, Mfuko huu unapewa fedha nyingi sana, takribani bilioni 30 kwa mwaka, lakini matumizi ya fedha hizi hayana matokeo yaliyokusudiwa kwa wananchi. Kwa hiyo, naomba tathmini ifanywe, uchunguzi ufanywe na kama kuna kasoro ambazo ziko wazi, basi hatua za mara moja na za makusudi zichukuliwe ili fedha nyingi ambazo zinapekekwa huku, zionekane katika upatikanaji wa pembejeo, pembejeo zipatikane za kutosha, kwa wakati na za bei nafuu na sivyo ilivyo sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana ndugu yangu Mheshimiwa Mwigulu kwamba eneo la uchunguzi ukifika Mtwara ni pamoja na Mfuko huu, umeniambia kwamba una ziara karibuni ya kuja Mtwara. Tembelea Mfuko huu, upate maelezo ya kutosha kwa Watalaam, kwa Management, lakini hata na wanufaika, Wakulima na wale wauzaji wa pembejeo za korosho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili ni kuhusu Bodi ya Korosho, ukisoma ile Sheria ambayo imeanzisha Bodi ya Korosho wana majukumu mengi sana, lakini ile Bodi ya Korosho ufanyakazi wake bado hauna matokeo makubwa tunayotarajia kwa Mkoa wetu wa Mtwara. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mwigulu Waziri wa Kilimo hebu fuatilia kwa ukaribu, utendaji wa Bodi hii na ikiwezekana marekebisho makubwa yafanywe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haraka nizungumzie suala la umeme vijijini. Mtwara ndiko kwenye Kiwanda cha Uchakataji wa Gesi Madimba na kile Kiwanda cha Msimbati. Hata hivyo, umeme vijijini bado haujawanufaisha vizuri wakazi wa Mkoa huo, kwa hiyo, naomba idadi ya Vijiji iongezwe na sioni kwa nini Serikali isitangaze kwamba tuwe na universal coverage kwa Mkoa wa Mtwara kwamba vijiji vyote vya Mkoa wa Mtwara vipitiwe na mradi huu wa umeme vijijini, kwa sababu wao ndiyo wazalishaji wa ile gesi ambayo ipo Madimba na kule Msimbati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika Jimbo langu la Nanyamba nina Vijiji 87, lakini viijiji ambavyo sasa hivi kuna umeme wa uhakika ni vijiji vitatu tu, sasa hapo Wananchi hawatuelewi. Gesi ipo kama kilometa 30 kutoka Nanyamba lakini Vijiji vitatu tu vyenye umeme hatueleweki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa mwisho niende kwenye uboreshaji wa sekta ya Elimu. Kwanza nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa jitihada ambazo inafanya ya kutoa elimu bure. Kwa kweli manufaa yake yanaonekana kwa wananchi wale ambao wanabeza ni kawaida yao kubeza, lakini mwananchi wa kawaida anajua kabisa nini ya maana ya Elimu bure, lakini ningeomba sana Serikali yangu ya Awamu ya Tano sasa hivi tujikite kwenye process teaching and learning process tusijikite kwenye output mambo ya division, GPA hayamsaidii mtoto anapotoka shuleni, tujikite maarifa na ujuzi anaoupata mtoto akiwa darasani.
Tuhakikishe vitabu vinapatikana vya kutosha, Walimu wanalipwa vizuri ili wawe na moral ya kufanya kazi, vilevile Walimu hawa wanajengewa nyumba za kutosha, lakini pia zana za kufundishia zinapatikana za kutosha na maabara zinakamilika na kutumika ipasavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili kuna Kitengo cha Udhibiti wa Ubora wa Elimu, Wakaguzi wa shule. Hiki kitengo hakifanyi kazi yake ipasavyo, vilevile hawapewi rasilimali za kutosha, kule nyuma kulikuwa na mawazo kwamba kitengo hiki nacho kipelekwe TAMISEMI. Kukawa na mawazo kwamba hawawezi kumkagua Mkurugenzi, lakini sikubaliani na hoja hiyo, kwa sababu kwenye Halmashauri kuna Mkaguzi wa ndani bado anamkagua Mkurugenzi na anapeleka ripoti kwake. Kwa hiyo, naomba ili kitengo hiki kiwe fanisi basi wathibiti wa ubora wa shule nao wapelekwe TAMISEMI.
MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umemalizika.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja.