Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia bajeti hii ya Nishati na Madini. Kabla sijaanza kutoa salamu za Wanamtwara na maagizo ya Wanamtwara kwa Wizara hii, naomba kwanza nitoe masikitiko yangu kwa kiasi kikubwa sana. Mheshimiwa Waziri hapa wakati anawasilisha hotuba yake kazungumzia mambo mengi yanayohusu gesi, mambo mengi yanayohusu petroli na mambo mengi yanayohusu mafuta ambayo ndiyo chachu ya uchumi wetu wa sasa hivi hapa nchini Tanzania.
Mheshimiwa Spika, masikitiko yangu, nilikuwa napitia gazeti leo hii, gazeiti la The Citizen, CAG ameeleza masikitiko yake makubwa kabisa na naomba ninukuu, halafu nimuulize Mheshimiwa Waziri swali langu. Amesema hivi:
“It was unfortunate that NAOT does not have a single expert in auditing accounts related to oil and gas despite trillions of cubic feet of fossil fuel reserves having been discovered in Tanzania”.
Mheshimiwa Spika, gazeti la leo, kwamba anasikitika na anaeleza, analiambia Taifa hili kwamba pamoja na umuhimu wa gesi na mafuta tuliokuwa nayo na wingi wake wote, lakini hana mamlaka ya kwenda kukagua, sasa sijui tatizo ni nini? Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kutoa majibu atueleze kwa nini account zile zinazotokana na visima vya mafuta na gesi havikaguliwi na CAG.
Mheshimiwa Spika, naomba nianze kuzungumzia suala zima hili la umeme vijijini. Ile Mikoa ya Kusini tuna bomba la gesi na kwa bahati nzuri Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini alizungumza katika mihadhara yake mingi sana kwamba Wanamtwara na Lindi watakuwa wananufaika na gesi kupitia mle lilimopita bomba la gesi kupitia Sekta ya Umeme.
Mheshimiwa Spika, mpaka hivi sasa ninavyozungumza ule unaitwa mkuza wa bomba la gesi ambalo Serikali imekuwa inaahidi kupitia miradi yake ya REA Awamu ya Kwanza, REA Awamu ya pili, mpaka hivi sasa tunakwenda kwenye REA Awamu ya tatu bado vijiji vile vyote havijapata umeme huu pamoja na ahadi nyingi na majigambo makubwa ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Madini. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri ya kwamba, ni lini sasa atahakikisha kwamba maeneo yote yanayopita bomba la gesi, mkuza wa gesi, anatekeleza ahadi yake ya kupeleka umeme? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuna suala hili la wananchi wa mikoa ya kusini kunufaika na gesi. Hata hivyo, nitoe masikitiko yangu makubwa sana, kwamba tumekuwa tunazungumza sana, tumekuwa tukiahidi sana, tukieleza sana, kuliko kutekeleza.
Mheshimiwa Spika, nilikuwa napitia mpango wa TPDC wakati tuko kwenye Kamati, lakini juzi taarifa yao tumekuwa tunapitia. Kuna mkakati ambao Serikali wameweka wa kuhakikisha kwamba gesi inayotoka mikoa ya kusini, Mtwara na Lindi inafika Dar es Salaam, baadaye itapelekwa mikoa mingine ya kaskazini kwa mfano Tanga, Mwanza na maeneo mengine. Katika mkakati ule pia wameeleza kwamba hii gesi itakuwa inapelekwa kwa ajili ya matumizi ya majumbani kuanzia Dar es Salaam, lakini cha ajabu ukipitia taarifa ile ya TPDC mikoa ya kusini, Mtwara na Lindi haipo.
Mheshimiwa Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri atakapokuja na majibu yake atueleze wananchi wa Mtwara na Lindi mkakati ukoje. Kwa sababu niliuliza swali hili wakati tunasikiliza taarifa ya Kamati ya Nishati na Madini tulivyowaita kwenye Kamati yetu hii ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma na wakasema kwamba watakwenda kulishughulikia. Naomba majibu ya Mheshimiwa Waziri kwamba asije akawa anazungumza tu wakati kwenye maandishi kule hakuna na Wanamtwara na Wanalindi pia wanasubiri majibu stahiki kutoka kwa Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Spika, nizungumzie pia suala zima ambalo Mheshimiwa Silinde ameligusia hapa, la kuwapa wawekezaji ambao wapo mikoa hii ya kusini nishati hii ya gesi waweze kutumia kama nishati. Leo hii tuna kiwanda ambacho kilitarajiwa kujengwa Mtwara maeneo ya Msangamkuu, ni kwa miaka minne hivi sasa yule mwekezaji anaomba apewe gesi ili aweze kujenga kiwanda cha saruji, mpaka leo tunavyozungumza ni danadana tu kwenye Wizara hii ya Nishati na Madini.
Mheshimiwa Spika, niombe sana Mheshimiwa Waziri ahakikishe kwamba wawekezaji hawa ambao wana nia ya kuwekeza Mikoa ya Kusini wanapewa nishati hii ya gesi ili waweze kuondoa umaskini ambao wananchi wa mikoa hii ya kusini umekuwa unatutawala kwa muda mrefu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini kama hiyo haitoshi, Mheshimiwa Silinde kazungumza, mwekezaji Aliko Dangote, kwa muda mrefu sana amekuwa akiomba gesi ili aweze kuitumia kama nishati. Mheshimiwa Silinde kazungumza kwamba ananunua makaa ya mawe kutoka Msumbiji, sio Msumbiji Mheshimiwa Silinde, ananunua makaa ya mawe kutoka South Africa. Meli inakuja Mtwara ku-gati kutoka South Africa ambayo mwekezaji huyu Aliko Dangote anatumia kama nishati wakati Mtwara tuna gesi iko kedekede, cubic meter za kutosha, kwa nini asipewe hizi gesi sambamba na kwamba yuko tayari kuuziwa, lakini Wizara mpaka leo inaleta danadana? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mwaka 2012, wananchi wa Mtwara na Lindi waliandamana kwa kiasi kikubwa sana wakidai manufaa ya gesi, kwamba kwa namna gani hii gesi itaanza kuwanufaisha wananchi wa mikoa ile. Na madai yetu yale yalipotoshwa sana, watu walifikia wakati, wengine viongozi kabisa wa Kitaifa wakiwabeza wananchi wa kusini kwamba wao wanahitaji kutumia gesi peke yao. Madai yetu yalikuwa ni kwamba gesi inayotoka mikoa hii, kwa sababu inaanzia pale, kwanza tunufaike kwa kupata mrabaha. Nimepitia na nimesikiliza hotuba ya Mheshimiwa Waziri, wakati anawasilisha sijaona hata sehemu moja na sijamsikia anasema kwamba mrabaha kiasi gani utabakizwa Mtwara na mikoa ile ya kusini ya Mtwara na Lindi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini cha ajabu kabisa kule kwenyewe inakotoka hii gesi, Msimbati, hata barabara ya kufika Msimbati ni kizungumkuti. Kwa nini Wizara na Serikali isitenge bajeti ya kujenga angalau barabara ile kiwango cha lami kutoka Mtwara Mjini mpaka kule Msimbati? Wananchi wa kusini wakidai haki hizi mnawapiga mabomu, mnatuletea Wanajeshi na kwamba sisi hatuipendi Serikali. Tunachosema ni kwamba, Serikali ihakikishe kwamba manufaa yanayotokana na gesi hii na sisi wananchi wa kusini tuweze kunufaika nayo.
Mheshimiwa Spika, upotoshwaji unaofanywa wa kwamba tunataka tuitumie gesi peke yetu si kweli. Nazungumza haya kwa sababu tuna ushahidi wa kutosha sana, tuna ushahidi wa kutosha. Sisi wote ni mashahidi, kwa kiasi kikubwa Korosho inazalishwa Mikoa ya Mtwara, Lindi na Pwani, lakini korosho ile kwa taarifa za mwaka jana na miaka mingi mfululizo limekuwa ni zao ambalo linaingizia Taifa pesa nyingi sana. Mwaka jana, 2014/2015 limekuwa ni zao la pili, lakini zile pesa zinazokusanywa na mapato ya korosho zote zinapelekwa Hazina zinanufaisha Watanzania wote.
Mheshimiwa Spika, tunachosema Wanakusini, tunachosema Wanamtwara na Lindi ni kwamba tunufaike na fursa za ajira na isiwe Serikali na Wizara inaondoa fursa hizi. Kwa sababu unapomnyima mwekezaji huyu kutumia gesi, kwa mfano, Aliko Dangote akiagiza makaa yake ya mawe kutoka South Africa anakodi meli, gharama zinakuwa ni kubwa, mwisho wa siku simenti inakuwa bei mbaya. Tunaomba sana wananchi wa Mtwara na Lindi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini jambo la ajabu sana, Serikali hii imekuwa ni sharp sana katika kuondoa rasilimali za kimaendeleo Mikoa ya Kusini kuliko kupeleka kwingine. Nimekuwa nazungumza hili kwa muda mrefu sana. Bomba la gesi limejengwa kwa miezi 18 tu. Kwa miezi 18 pesa zilizotumika zaidi ya Dola za Kimarekani bilioni mia mbili kama na hamsini na tano, lakini tunavyosema kwamba, tunahitaji maendeleo yaletwe kusini yanachukua muda mrefu sana. Suala la kufanya negotiation ya mkataba tu kwamba huyu mwekezaji wa Kiwanda cha Mbolea Mtwara, Dangote na yeye mwekezaji wa simenti inachukua muda mrefu, kwa nini? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, siungi mkono hoja mpaka haya maswali yangu yaweze kupatiwa majibu.