Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote na mimi ninapenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutuwezesha kuwepo hapa leo kukamilisha kazi ambayo niliianza toka siku jana tarehe 17 Mei, ambapo niliwasilisha hoja hii. Katika siku hizi mbili Waheshimiwa Wabunge 209 wametoa michango yao kwa njia ya maswali, mapendekezo na maoni kuhusu namna bora ya kusimamia, kuendesha, kuboresha na kuendeleza miundombinu ya Sekta ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kutoa shukrani zangu za dhati kwako wewe binafsi, Wenyeviti wote na Makatibu wa Bunge kwa umakini wa hali ya juu mliotuonesha kwa kusimamia kwa ufanisi mkubwa majadiliano yote kwenye Mkutano huu wa Tatu wa Bunge letu hili Tukufu. Aidha, napenda pia kumpongeza Kiongozi wa Shughuli za Serikali Bungeni, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa utendaji kazi wake wenye ufanisi na tija ya hali ya juu ambao umetufanya sisi wasaidizi wake kuwa na kazi rahisi kutekeleza majukumu yetu. Ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)
Mwisho, lakini si kwa umuhimu, napenda pia kuwapongeza Wenyeviti na Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu na Kamati ya Bunge ya Bajeti kwa kufanya kazi kwa karibu sana na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Kamati hizi zimetuonesha upeo mkubwa wa ufahamu kuhusu wajibu wa sekta, kuwezesha sekta nyingine kufikia malengo yao. Ahadi yangu kwa Wajumbe wote wa Kamati hizi ambao waliwawakilisha Waheshimiwa Wabunge wote wengine ni kuwa yote tuliyokubaliana kwenye vikao mbalimbali kati ya Wizara na Kamati tutayatekeleza. Wizara itaendelea kufanya kazi kwa karibu na kamati hizi, ili kufikia malengo yake. (Makofi)
Mheshmiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Wizara ninayoisimamia ina sekta kuu tatu (sekta ya ujenzi, uchukuzi na mawasiliano), nitajibu kisekta hoja kuu za Waheshimiwa Wabunge. Mheshimiwa Naibu Waziri tayari amejibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge, kazi yangu itakuwa ni kujibu hoja kuu zilizojitokeza ambazo ndio msingi wa utekelezaji wa majukumu ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaanza na sekta ya ujenzi ikifuatiwa na sekta ya uchukuzi na hatimaye sekta ya mawasiliano. Kitakwimu Waheshimiwa Wabunge 209 walichangia wakati wa majadiliano ya hoja ya Wizara ya Ujenzi Uchukuzi na Mawasilino ambapo Waheshimiwa Wabunge 89 walichangia kwa kuzungumza na Waheshimiwa Wabunge 120 walichangia kwa maandishi. Ninawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukuhakikishia kuwa tutajibu hoja zote za Wabunge kwa maandishi na kuwapatia Waheshimiwa Wabunge wote majibu ya hoja hizo kabla ya kuanza kwa Mkutano wa Kumi na Nne wa Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hivyo kwa yale yote ambayo hatutoweza kuyajibu hapa leo kwa sababu ya muda, majibu yatapatika kupita maandishi ambayo Wizara yangu itaandaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nianze na sekta ya ujenzi na ukarabati wa barabara. Barabara ni moja ya miundombinu muhimu kwa ajili ya kuchochea maendeleo. Serikali itaenda kutenga fedha ili kujenga na kukarabati barabara ikiwa ni pamoja na kutekeleza sera ya kuunganisha mikoa kwa mikoa pamoja na nchi jirani kwa barabara za lami kama walivyoshauri Waheshimiwa Wabunge wengi waliochangia hoja hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2016/2017 Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Fungu 98 - Ujenzi kwa ajili ya miradi ya maendeleo imepangiwa shilingi trilioni 2.176. Kulikuwa na hoja kwamba je, kati ya fedha hizo, fedha ngapi au shilingi ngapi zitakwenda kwenye kulipa madeni?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 400, zitatumika kukamilisha malipo ya madeni ya nyuma ya Makandarasi na Wahandisi Washauri wa miradi ya barabara itakayobakia, yaani shilingi trilioni 1.776 zitatumika kwa kujenga barabara. Kama unavyojua, Wizara yangu imepewa takribani shilingi trilioni 4.895, hii ni historia kwa nchi yetu, haijawahi kutokea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wenzangu kwamba, tutasimamia wajibu wetu kwa uadilifu mkubwa na hatutawaangusha. Waheshimiwa uwezo tunao, nia tunayo ya kuhakikisha kwamba tunawajengea Watanzania miundombinu ya kisasa ili waweze kuingia kwenye uchumi wa kati ifikapo mwaka 2020/2025. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila miundombinu bora hakuna nchi yoyote iliongia uchumi wa kati. Kwa kulitambua hili, tutalifanyia kazi na tutajipanga inavyopaswa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiendelea katika maoni ya Msemaji wa Kambi ya Upinzani Bungeni, kumetolewa hoja inayohusu upotevu wa shilingi bilioni 5.616 ya riba inayotokana na TANROAD kutokulipa madai ya Makandarasi kwa wakati, katika kipindi cha mwaka 2012 hadi 2015 ambayo imetoka na Ripoti ya CAG iliyotolewa mwezi Machi, mwaka huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuweka kumbukumbu sawa napenda kunukuu mapaendekezo ya CAG kwenye ripoti ya mwaka 2014/2015 kuhusu taarifa ya fedha za Serikali kwa mwaka unaoishia tarehe 30 Juni, 2015 iliyotolewa Machi mwaka huu, ukurasa wa 143 kama ifuatavyo; “Napendekeza Wakala wa Barabara yaani TANROADS ifuatilie fedha ili kuhakikisha miradi inakamilika kwa wakati, pia napendekeza mikataba itolewe kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Hii itasababisha Serikali kuepuka gharama zisizo za lazima yaani riba zinazotokana na ucheleweshaji wa malipo ya wakandarasi.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu ya hoja hiyo ni kwamba madai ya riba kwenye madeni ya wakandarasi kumetokana na ukosefu wa fedha za kulipa madeni ya makandarasi na wahandisi washauri wa miradi ya barabara kwa wakati. Serikali kwa sasa inaendelea kutoa fedha kwa ajili ya kulipa madeni ya makandarasi na wahandisi washauri wa miradi ya barabara na madaraja, kwa hivyo kupunguza madeni hayo na kupunguza riba inayotokana na malimbikizo hayo. Nyote mmekuwa mashahidi mara baada ya Mheshimiwa Magufuli kuingia madarakani, kuanzia mwezi wa Novemba mpaka sasa hivi, Wizara yetu imepelekewa takribani shilingi trilioni moja, hili ni jambo kubwa na tunamshukuru sana Mheshimiwa Magufuli. Tunaamini huko tunakokwenda hakutokuwa na malimbikizo tena kwa vile tunaamini tukipata ukaguzi wetu utakuwa uko safi na hautokuwa una matatizo tena.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja nyingine inayosema kwamba barabara zilizotengewa fedha kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami katika Mkoa wa Mara ilikuwa ni kilometa 0.8, ukweli wenyewe ambao uko katika bajeti yetu kwa mkoa wa Mara tumetenga zaidi ya kilometa 58 katika mwaka wa fedha 2016/2017 ambazo zimetengewa jumla ya shilingi bilioni 64.88 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mikubwa kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa kwanza ni Makutano- Nata- Mugumu shilingi bilioni 12, mradi wa pili ni Simiyu - Mara Border - Mosoma, shilingi bilioni 16.4, mradi wa tatu, Makutano - Sirari shilingi bilioni mbili, mradi wa nne ni Nansio - Bulamba shilingi bilioni 20.697. Mradi mwingine Nyamuswa – Bunda - Bulamba shilingi bilioni 8.435, mradi mwingine ni Musoma- Makojo- Besekela shilingi bilioni 2 na mradi wa mwisho ni daraja la Kirumi na daraja la Mara zote daraja mbili zimetengewa shilingi bilioni 3.8. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa kurejea, Waheshimiwa Wabunge, nendeni kwenye kitabu changu cha bajeti na tembeleeni ukurasa wa 218, 219 na 225 wa kitabu hicho mtaona maelezo hayo ambayo nimeyaweka hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, jumla ya shilingi bilioni 31 zimetengwa kwa ajili ya miradi mingine ya ujenzi na ukarabati wa barabara kwa kiwango cha lami na changarawe pamoja na matengenezo ya barabara katika Mkoa wa Mara. Fedha zote zilizotengwa kwa Mkoa wa Mara ni shilingi bilioni 96.38, ninaomba, Waheshimiwa Wabunge rejeeni kwenye kitabu changu cha bajeti, ukurasa 218, 219, 244, 262, 273, 275, 279, 284, 289, 293, 305, 319, 329, 337 na ukurasa wa 345. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja nyingine ambayo inasema, mkandarasi wa barabara ya Makutano - Nata - Mugumu, sehemu ya makutano Sanzate amelipwa fedha kama ifuatavyo; kulikuwa na hoja kwamba amelipwa fedha zaidi, lakini tulilofanya kwanza tumelipa malipo ya awali (advance payment) ambayo ni shilingi bilioni 6.7 halafu tumelipa ya kazi zilizofanywa ambayo ni shilingi bilioni 8.2, jumla shilingi bilioni 14.9 zimelipwa. Kati ya fedha ya advance payment ya shilingi bilioni 6.7 zilizorejeshwa ni shilingi bilioni 1.4. Kazi zilizofanyika ni pamoja na ujenzi wa daraja ambalo limekamilika kwa asilimia 80, mkandarasi ameunda tuta la barabara la kilometa 40 baada ya kukamilika ujenzi wa tuta la kilometa 40, mkandarasi amefanya maandalizi ya ujenzi wa matabaka ya msingi, yaani sub base na base course na hatimaye tabaka la lami.
Waheshimiwa Wabunge naomba muelewe kwamba katika ujenzi wa barabara, sehemu ndogo ya fedha inatumika kwa kuweka lami, lakini asilimia kubwa ya fedha inatumika kwa ile kazi ya msingi. Kwanza ile civil work, halafu course work, halafu base work, sasa tumemlipa huyu mkandarasi kutokana kazi aliyoifanya sivyo hivyo ilivyoelezwa. Mradi huu unahusisha makandarasi 11, una lengo la kuwajengea uwezo makandarasi wazalendo. Makandarasi hawa walimaliza mradi mkubwa wa ujenzi wa daraja la Mbutu, mkoani Tabora kwa ufanisi mkubwa. kwa hivyo, tuna wajibu sana wa kuwezesha Watanzania, Serikali hii ina jukumu kubwa la kuwa-empower Watanzania, Wizara tuna wajibu mkubwa wa kufanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja inayohusu kivuko cha Mv Dar es Salaam, nikirejea tena kwenye hoja ya CAG, kwenye ripoti yake CAG alisema kuna mapungufu yafuatayo; mapungufu ya ununuzi wa kivuko shilingi bilioni 7.9, naomba nisome hoja hiyo kama ilivyoelekezwa na Mheshimiwa CAG:
Wizara ya Ujenzi kupitia Wakala ya Umeme, Mitambo na ufundi yaani TEMESA iliingia mkataba na Ms Jones Gram Hansen DK Copenhagen ya Denmark kwa ununuzi wa kivuko cha Dar es Salaam - Bagamoyo chenye thamani ya dola za Kimarekani milioni 4.98 bila Kodi ya Ongezekoo la Thamani. Mapungufu yafuatayo yalibainika katika manunuzi hayo:-
Kwanza, kasi ya kivuko haikukidhi matakwa ya ununuzi. Ripoti maalum ya mkaguzi ilibainisha kwamba kiwango cha juu na cha chini cha kasi ya kivuko wakati wa majaribio kilikuwa ni kati ya notes 19.45 na 17.25 kinyume na makubaliano yalioainishwa kwenye mkataba ya kasi ya note 20, maana yake haikufikiwa ile speed ambayo ilikubalika kwenye mkataba.
Pili, ilikuwa Hati ya makabidhiano haikutolewa, kivuko kilikabidhiwa bila hati ya makubaliano (good acceptance certificate) mwezi Novemba, 2014, baada ya ucheleweshwaji wa siku 16. Naomba niwachukue Waheshimiwa Wabunge kwenye utaratibu wote ambao tuliweza kununua kivuko hicho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakala wa Ufundi na Umeme ulitangaza zabuni ya ununuzi wa kivuko hiki kwa kupitia njia ya International Competitive Bidding ambayo ilifanyika tarehe 29 Oktoba, 2012 kupitia gazeti la Daily News. Kampuni tano ziliomba na kampuni ya Jones Gram Hansen ambayo ilikuwa na bei ya chini ndiyo ilikubaliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, thamani za zabuni baada ya thamani kufanyika ilionekana kwamba kampuni ya Jones Gram Hansen ya Denmark ndiyo ilikuwa imetuma zabuni hiyo lowest evaluated bidder kwa gharama ya dola za Kimarekani milioni 4.98 sawa na shilingi za Tanzania bilioni 7.968.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Zabuni kuridhia; Bodi ya Zabuni ya TEMESA kupitia kikao kilichofanyika tarehe 20 mwezi wa Pili mwaka 2013, ililidhia zabuni hiyo kupewa kampuni ya Ms Jones Gram Hansen ya Denmark kwa gharama iliyotajwa hapo juu yaani dola za Kimarekani milioni 4.98 sawa na shilingi za Tanzania bilioni 7.968 kama ilivyopendekezwa na Kamati ya Thamini ya Zabuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kusaini mkataba; mkataba wa zabuni ya ujenzi wa kivuko cha Mv Dar es Salaam ulisainiwa kati ya TEMESA na kampuni ya Ms Jones Gram Hansen ya Denmark tarehe 25 Aprili, 2013.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa kivuko; ujenzi wa kivuko ulianza kutekelezwa baada ya mkataba kusainiwa na wakati wa ujenzi wa kivuko hiki ukaguzi ulifanyika hatua kwa hatua na ulihusisha watalaam wa SUMATRA. Picha zilizoambatanishwa ambazo ziko hapa zinaonyesha watalaam mbalimbali ambao walikwenda kuangalia kivuko hicho hatua kwa hatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni ya Ms Jones Gram Hansen ilikamilisha ujenzi wa kivuko cha Mv Dar es Salaam mwezi Septemba, 2014 na ilisafirisha kivuko hicho kuja nchini Tanzania mwezi Novemba, 2014.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kivuko kuwasili kulingana na matakwa ya mkataba, mzabuni alitakiwa kufanya ukaguzi wa pamoja na Kamati ya mapokezi na majaribio ya kivuko hicho kabla ya kukikabidhi kivuko hicho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa ukaguzi wa Kivuko, vifaa vyake na majaribio kitu kikubwa kilichoonekana ni kivuko kutofikia kasi uliyotakiwa ya note 20 badala yake ilifikia note 15.7. Mzabuni Jones Hansen alifahamishwa juu ya upungufu huu na alikubali kufanya marekebisho hayo kabla kivuko kupokelewa na kulipwa asilimia 10 ya malipo ya mwisho kwa gharama zake, kwa sababu alitakiwa alipwe ten percent lakini kutokana na matatizo haya alitakiwa afanye kazi hii aimalize ndiyo alipwe fedha zake na hii kazi aifanye kwa gharama zake. Hadi sasa mzabuni hajalipwa kiasi hicho cha fedha hadi atakapo kamilisha marekebisho hayo. Kwa sasa mzabuni ameleta mpango wa marekebisho anayotarajiwa kuyafanya ili kufikia mwendo kasi uliokusudiwa yaani note 20. Wakala wa Ufundi na Umeme utapitia mpango huo ili kujiridhisha marekebisho hayo kufanywa kwa mzabuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo ndiyo maelezo kuhusu utaratibu mzima wa kununua Mv Dar es Salaam na kulikuwa hakuna ukiukwaji wowote uliyofanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee na hoja nyingine. Kuna hoja ambayo imewasilishwa juu ya suala la uuzwaji wa nyumba za Serikali. Ni kweli kuwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilipitisha Azimio kuhusu Uuzwaji wa Nyumba za Serikali tarehe 24 Aprili, 2008 katika Mkutano wa Kumi na Moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia Azimio hilo, Serikali kupitia iliyokuwa Wizara ya Ujenzi iliwasilisha taarifa ya mwisho ya utekelezaji wa Azimio hilo tarehe 01 Julai, 2009. Taarifa ambayo ilipokelewa na kupitiwa kwa kina na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu. Baada ya Kamati hiyo kuridhika na hatua za utekelezaji zilizochukuliwa, Serikali iliwasilisha taarifa yake mbele ya Bunge ambalo liliipokea na kukubali, kwa mantiki hiyo hoja hii ilikuwa imeshafungwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kulinda miundombinu ya barabara ambayo inagharamu fedha nyingi. Tuna mizani 60 kwa ajili ya kupima uzito wa magari ili kudhibiti uzidishaji wa uzito ambao unaharibu barabara zetu. Pamoja na kuwepo kwa mizani hizo bado baadhi ya barabara zinaharibika kutokana na uzito wa magari yanayopita katika barabara hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na utafiti uliyofanywa na Wizara hivi karibuni kwenye magari yenye matairi ya super single imebainika kuwa asilimia 70 ya magari yote yanayotumia matairi ya super single ambayo hayana viwango vinavyokubalika kisheria. Aidha, imebainika kuwa magari yenyewe hayana viwango vya air suspension vinavyokubalika. Kutokana na matokeo hayo ya utafiti, Wizara inafanya utaratibu wa kuzuia matumizi ya matairi ya aina ya super single yasiyo na viwango vinavyokubalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya ujenzi; hoja ya mwisho ilikuwa athari zilizojitokeza kutokana na kujitoa kwa MCC katika ufadhili wa miradi. Kwa upande wa miradi ya barabara na viwanja vya ndege hakuna athari zilizojitokeza kutokana na kujitoa kwa MCC katika ufadhili wa miradi. Miradi ifuatayo ya barabara na kiwanja cha ndege imejengwa kwa kiwango cha lami na kukamilika kwa ufanisi mkubwa wakati wa awamu ya kwanza ya MCC. Tanga - Horohoro kilometa 65, Tunduma - Sumbawanga kilometa 223.1, Peramiho - Mbinga kilometa 78, Songea - Namtumbo kilometa 72 na uwanja wa ndege wa Mafia umejengwa na hakuna tatizo lolote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze kwenye sekta ya uchukuzi. Hoja ambayo imevuta mvuto mkubwa sana kwenye Bunge lako leo ni hoja ya ujenzi wa reli ya kati. (Makofi)
Kwanza kabisa kwenye kitabu changu cha hotuba ya bajeti kuna baadhi ya Wabunge kidogo hawakunielewa. Kwenye kitabu changu cha hotuba ya bajeti ukurasa wa 72, tunazungumzia utekelezaji wa miradi, hatuzungumzii utekelezaji wa miradi kwa mwaka 2016/2017. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua hata kama tutatumia pesa gani kujenga barabara, lakini barabara zetu hazitaweza kudumu kama hatutawekeza kwenye reli. Bila reli hatutaweza kujenga uchumi wa kati kama tunavyosema. Kwa kulitambua hilo, Serikali ya Awamu ya Tano imesimama kidete kuhakikisha kwamba tunajenga reli ya kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge kwamba reli ya kati ina urefu takribani wa kilometa 2,527 ambao unaanzia Dar es Salaam – Tabora – Isaka - Mwanza kilometa 1,219. Tabora - Kigoma kilometa 411, Uvinza - Msongati kilometa 200, Kaliua – Mpanda - Karema kilometa 360 na Isaka - Rusumo kilometa 337. Kama tunataka kujenga mradi huu wote kwa pamoja tunahitaji tuwe na takribani dola za Kimarekani bilioni nane ambazo ni takribani trilioni 16. Hizi ni pesa nyingi, hakuna nchi yoyote inayoweza kuipa Tanzania mkopo wa dola bilioni nane.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kulitambua hilo mimi nilipata fursa ya kufuatana na Mheshimiwa Rais Mstaafu kwenda China kuzungumzia jinsi ya kupata mkopo kwa ajili ya reli ya kati. Serikali ya China ilitoa ushauri kwamba huu mradi ni mkubwa ni lazima tuugawe kwa awamu. Kwa busara tukaona tuchukue tawi kubwa ambalo ndilo litakuwa backbone ya mradi huu ambayo itakuwa kuanzia Dar es Salaam - Tabora - Isaka - Mwanza yenye kilometa 1,219, kwa vile awamu ya kwanza ya mradi huu tunataka tuanze Dar es Salaam - Tabora - Isaka - Mwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kawaida ulimwenguni kilometa moja ya reli inajengwa kwa takribani dola za Kimarekani kuanzia milioni 3.5 mpaka dola za Kimarekani milioni 4.5, kwa mahesabu ya haraka ukichukua kilometa 1,219 tunatakiwa tupate angalau dola za Kimarekani, kwa bei ya chini bilioni 4.256 na pengine ya juu inaweza kwenda bilioni 4.876, itategemea geology ya eneo ambalo unajenga, itategemea miamba ya eneo ambalo unajenga, itategemea, kama eneo hilo lina matetemeko bei itabadilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya China ilitukubalia tunaweza tukachukua mkopo kwa ajili ya mradi huo na kawaida ukichukua mkopo China, kuna mikopo ya aina tatu. Mkopo kwanza kabisa kuna 100 percent loan ambayo ni concession loan unapata asilimia 100 mkopo. Kikawaida katika Tanzania ni miradi michache imepata mkopo asilimia 100, mradi ninaojua mimi ni mradi wa National ICT Backbone, ule umepata mkopo wa asilimia 100 kutoka China. Mikopo mingine ambayo unaweza kupata, unapata mkopo wa asilimia 85 na wewe mwenyewe unatakiwa uwe na asilimia 15. Mkopo wa mwisho ni mkopo wa commercial.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile sisi tunataka kuchukua mkopo, lazima tujipange tuwe na mtaji wa kuanzia, ndiyo Serikali ikaweka trilioni moja kwenye bajeti ya mwaka huu. Trilioni moja maana yake nini, maana yake kama umechukua mkopo wa dola za Kimarekani bilioni 4.2, 10 percent ya hiyo ni dola milioni 420 za Kimarekani. Sasa tukichukua trilioni moja tunapata kama dola milioni 400, ina maana tuna uwezo wa kuchukua mkopo hata kama tukiambiwa tulipe asilimia 85.
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tumefanya nini kwenye jambo hili.
Kwanza tumeanzisha technical team, pili tumeanzisha National Steering Committee kwa ajili ya mchakato huu. Step inayofuata ni kutangaza tender ili kupata kampuni za Kichina ziweze kujenga reli hiyo. Kwa nini tumeamua kufanya hivyo, Waheshimiwa Wabunge nitawapa tu kidogo. Wenzetu wa Kenya wamejenga reli kutoka Mombasa - Nairobi kwa standard gauge ambayo ni kilometa 485, kwa kilometa moja wametumia dola za Kimarekani milioni 7.84. Nigeria wamejenga reli yao inaitwa Nigeria Railway Modernisation Project wametumia dola za Kimarekani milioni 6.31. Chad wamejenga reli yao wametumia dola za Kimarekani milioni 5.58. Tunafikiria lazima tuitangaze tender, watu waombe, tunaamini tukifanya hivyo tutapata bei nzuri kuliko kwenda kwa bei ya Kenya na nchi nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo mengi lakini muda umeisha. Mwisho kabisa sasa na mimi naomba kutoa hoja.