Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anazofanya na mimi nitajikita zaidi kwenye ujenzi wa barabara na pengine kwa ujumla, mambo mengine machache. Napenda kuwapongeza kwa sababu si kazi rahisi kujenga barabara za lami katika miaka michache kwa kilometa 17,000 na ninashukuru sana Mkoa wa Manyara una kilometa 223 za lami.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuiomba Wizara, pamoja na kilometa hizi 223 sisi tuna barabara ambayo tumeiomba na Mheshimiwa Rais aliahidi barabara kutoka Mogitu kwenda Haydom – Mbulu mpaka Karatu na Haydom ndio Hospitali ya Rufaa, kuna miezi mingi ya mvua ambapo wananchi hawawezi kwenda kwenye hiyo hospitali, kwa hiyo, tunaomba sana barabara hiyo iwe ya lami. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi zangu naomba Wizara iangalie gharama za kujenga barabara za lami. Nilivyoangalia takwimu kwenye kitabu hiki ni karibu shilingi milioni 800 mpaka shilingi bilioni moja kujenga kilometa moja. Ninaomba sana tuliangalie hilo kwa sababu, badae hii itakuwa reflected kwenye gharama za uchumi ndani ya nchi na ninajua kwamba, mwanzo ni mgumu, lakini tunavyoendelea tunaweza tukafanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo naliomba ni barabara za Mkoa wa Manyara, ni chache sana ambazo zina hadhi ya mkoa, tunaomba sana barabara zile zipandishwe hadhi. Na tumeshaandika barua kwenye Wizara, lakini naomba nikumbushe barabara ya Dongobesh - Obesh - Basodesh - Gawal mpaka Singida tunaihitaji kwa sababu itatusaidia sana kwenye uzalishaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ambalo ninaliomba ni kwamba tumeweza kujenga barabara nyingi kuu kwa ajili ya kupewa asilimia 70 ya Mfuko wa Barabara. Ninafikiri muda umefika sasa kupeleka nguvu kubwa zaidi kwenye barabara za Wilaya na vijijini na ni wakati muafaka na ninawaomba Wabunge tukubaliane kwamba sasa mgawanyo uwe asilimia 50 kwa 50 ili barabara hizi ziende sambamba na barabara kuu ziwe served na barabara zile za Wilaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema kwamba nitajielekeza zaidi kwenye mambo ya ujumla; nasema kwamba jamani katika usafirishaji na uchukuzi, gharama ndogo iko kwenye usafiri wa maji, ukifuatiwa na usafiri wa reli. Na uchumi utakuwa na gharama ndogo kama reli itakuwa inatumika zaidi kuliko barabara. Ninaungana mkono na watu wa reli ya kati, reli ya Tanga na ile ya Kaskazini kuelekea Kaskazini Magharibi kwa kufanya uchumi wetu uwe wa ufanisi kulinganisha na nchi zingine ili tuweze kufanya biashara nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana hili tuliangalie ili baadae sasa barabara ziwe zina-feed reli na ninajua kuna watu, na mimi kama ningekuwa na malori ningeogopa kwa binafsi yangu kuzamisha reli kwa ajili ya barabara. Ninaomba sana hili tuliangalie, lina maslahi binafsi, ni ngumu na tuliangalie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ningependa kusema namna ya kuendesha Bunge hapa. Ninaomba sana jamani habari ya kutukanana, habari ya kukashifiana, haikubaliki na Kanuni za Bunge, lakini hili ni jumba tukufu, hili ni jumba ambalo tunapaswa kuwaheshimu viongozi wetu wa nchi…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono bajeti ya Waziri, pamoja na…