Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante.
Mheshimiwa Mwenyekiti nilikuwa nimejipanga kwa ajili ya dakika kumi lakini nitajitahidi nitumie muda mfupi kadri itakavyowezekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti tarehe 22 Februari, 2016 wananchi wa maeneo ya Omukajunguti ambao walielekezwa wasiendelee na shughuli za maendeleo katika eneo hilo na tathmini ikafanyika kwa ajili ya kulipwa fidia kwa ajili ya uwanja wa Kimataifa wa Omukajunguti; na tarehe 22 Februari, 2016 wakapokea barua kutoka Wizara ya Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano iliyowekwa sahihi na Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Ndugu G. Migire kwamba fedha hizo zitatengwa katika bajeti hii. Sasa wananchi wakaniomba wakisema ukienda huko unga mkono bajeti ya Wizara ili tuweze kupata fedha yetu ya fidia. Lakini nimepitia kitabu hiki na vitabu vingine, sioni fedha hizo za kulipa fidia. Kwa hiyo nachelea kuunga mkono bajeti hewa inapokuja kwenye suala la kulipa fidia watu wa Omukajunguti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo nataomba Mheshimiwa Waziri anisaidie kunipa maelezo nielewe vizuri ili nitakapokuwa naunga mkono bajeti yake nikikutana na mpiga kura wangu akaniuliza niwe na majibu sahihi ya kumueleza kwanini niliunga mkono bajeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia ningependa kumkumbusha Mheshimiwa Waziri, tunayo ahadi thabiti ya Mheshimiwa Rais alipokuja kwenye kampeni alituahidi akiingia Ikulu fedha zote atakazozikuta atazichukua azilete Omukajunguti kwa ajili ya kulipa fidia. Mheshimiwa Rais akishazungumza, Mheshimiwa Waziri natarajia asaidie katika kutekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais. Vigezo vingine vyote vinathibitisha ule uwanja ni muhimu kwa ajili ya maendeleo ya Mkoa wa Kagera, kwa ajili ya Kanda ya Ziwa na maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jambo la pili kwa harakaharaka tunayo ahadi ya kilometa tatu za lami kwa ajili ya Mji wa Bunazi, nimeangalia kwenye kitabu hiki sizioni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kilometa 40 za barabara kujengwa kwa kiwango cha lami kuanzia Katoma hadi Kashenye.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli ukiangalia hesabu kwa haraka haraka, barabara hii imekuwa ikijengwa kwa kiwango cha lami kwa mita 500 kila mwaka. Kwa mwendo huu itachukua miaka 80 ya kukamilisha ujenzi wa barabara hiyo. Sasa miaka 80 kujenga kilometa 40, huo sio mwendo wa hapa kazi tu, ni mwendo wa konokono ambao nakuomba Mheshimiwa Waziri unisaidie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kwa sababu dakika zenyewe ni chache tuna ahadi inayotoka kwa Makamu wa Rais juu ya barabara ya lami kutoka Kaja hadi Mugana, Hospitali Teule ya Wilaya. Naomba Mheshimiwa Waziri akiwa anjibu atusaidie kufafanua hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo ningependa kulizungumza kwa sababu ya muda, naona figisufigisu katika ujenzi wa meli mpya katika Ziwa Victoria. Ahadi ilikuwa kujenga meli nne, mbili Ziwa Tanganyika, moja Ziwa Victoria na nyingine kule Ziwa Nyasa. Lakini ukisoma kitabu hiki, ahadi hiyo sasa taratibu inabadilika sasa tunaona fedha zilizotengwa ni shilingi bilioni 20 za kuanza kujenga meli katika Ziwa Victoria, sioni lini tutaanza kujenga kule Ziwa Tanganyika wala Ziwa Nyasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia ukisoma kitabu hiki kwa haraka haraka kama una akili ya kufikiria kidogo unapata mashaka, kwa sababu inaonekana zimetengwa shilingi bilioni 20 za kujenga meli mpya katika Ziwa Victoria, lakini hatuelezwi, meli hiyo mpya itagharimu Shilingi ngapi. Lakini katika kitabu hiki hiki tunaambiwa itakarabatiwa MV Victoria kwa shilingi bilioni 20. Sasa kama shilingi bilioni 20 zinatumika tu kukarabati inakuwaje tena unatenga shilingi bilioni 20 kwa ajili ya kujenga meli mpya? Mimi nadhani kama ni kweli shilingi bilioni 20 ndizo zinazotakiwa kwa ajili ya ukarabati basi zingetengwa fedha nyingi zaidi kwa ajili ya kujenga meli mpya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mheshimiwa Waziri anafahamu Serikali ilitoa shilingi bilioni 600 kwa ajili ya ukarabati MV Victoria lakini fedha hizo hazikufanya kazi iliyokusudiwa. Namshukuru Mheshimiwa Waziri alichukua hatua. Lakini napenda niseme kama siku chache zilizopita, shilingi bilioni 1.3 zilikuwa zinatosheleza kukarabatia MV Victoria, imekuwaje leo sasa inabadilika si shilingi bilioni 1.3 tena ni shilingi bilioni 20 zinazohitaji kufanya ukarabati. Ndiyo maana nakuwa na wasiwasi, ningependa Mheshimiwa Waziri, anieleze kwamba katika maamuzi haya hakuna figisufigisu bali kweli tunataka kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi na kuji-adress kwa yale tunayokusudia.
Mheshimiwa Mwenyekiit, kwa sababu ya muda naomba niishie hapo. Nachelea kuunga mkono hoja mpaka hapo nitakapokuwa nimepewa maelezo yatakayoniwezesha mimi kurudi kwa wananchi na kuwaeleza kwa nini nimeunga mkono hoja, ahsante.