Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya njema aliyonijalia. Nawashukuru wanawake wa Dodoma kwa kunipenda tena na kunichagua kuwa Mbunge lakini pia Chama changu cha Mapinduzi.
Nawapongeza sana Watanzania kwa uamuzi wa dhati walioufanya kwa kuichagua tena CCM kuitawala nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli Mheshimiwa Goodluck amenifurahisha, nampongeza sana. Tunachofanya leo ni kuisaidia Serikali. Wameleta mwelekeo wa Mpango na tunatakiwa tujadili na kuwapa mawazo mapya ni wapi wanaweza wakapata mapato zaidi ili matumizi yaendane na mapato. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, hiyo ndiyo kazi kubwa tuliyonayo hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma taarifa ya Serikali na nimeona jinsi sekta ambayo Watanzania ni wengi ilivyochangia kwa kiasi kidogo sana, 4% ya pato la Taifa, ni sekta ya kilimo, uvuvi na misitu. Najiuliza kwa nini sekta ya kilimo na ufugaji ichangie kidogo? Tanzania kila kona kuna ugomvi wa wakulima na wafugaji ina maana tuna mifugo mingi ambayo haileti faida ndani ya nchi, haichangii kwa kiasi kikubwa kwenye pato la Taifa. Ndiyo maana mifugo, kilimo, misitu, uvuvi imechangia 4% tu. Lazima tutafute ni wapi tulipokosea mpaka sekta hii isichangie pato la Taifa kwa kiasi kikubwa. Kuna mazao yanayotokana na mifugo mfano maziwa, ngozi, nyama na kuna mifugo mingi sana ndani ya Tanzania. Nadhani Serikali itafute sasa namna ya kushughulikia matatizo yaliyopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suluhisho siyo kupima ardhi ni kuwasaidia wafugaji kupunguza mifugo. Nilikwenda Mkoa wa Arusha kipindi fulani tukaambiwa, tena alisema mfugaji mwenyewe yeye ana ng‟ombe 10,000. Kama mtu mmoja ana ng‟ombe 10,000 na hana jinsi ya kupunguza mifugo yake lazima ugomvi wa wakulima na wafugaji utaendelea lakini hatuwezi kuona faida ya kuwa na mifugo mingi. Vilevile hatuwezi kuona faida ya wavuvi wakati maziwa tunayo yamezunguka nchi yetu; tuna Ziwa Tanganyika, Ziwa Viktoria lakini tuna bahari. Nadhani Serikali iangalie namna ya kutumia sekta hii kuzalisha kwa wingi. Tupate viwanda vya nyama, viwanda vya maziwa, viwanda vya kusindika samaki, viwanda vya matunda, tutaona ugomvi wa wafugaji na wakulima hautakuwepo tena. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tumemuudhi Mwenyezi Mungu, siku hizi mvua hainyeshi inavyotakiwa. Kwa hiyo, tukiendelea na kilimo cha kutegemea mvua hatutafika mbali. Ndiyo maana mvua isiponyesha vizuri baada ya muda mfupi wananchi wetu wana njaa. Kwa hiyo, lazima tutafute namna ya wakulima wetu kuwa na ukulima endelevu. Bila hivyo, kila mwaka tutakuwa tunalia hatuna chakula, sekta ya kilimo haijachangia kwa kiasi kikubwa lakini hatuna mipango mizuri kwa wakulima na kwa wafugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna fukwe nzuri sana kuanzia Mtwara hadi Tanga, tunaweza kuzalisha kupitia fukwe zetu. Siyo lazima Serikali ifanye, tunaweza tukaingia ubia na watu binafsi. National Housing ni mfano mzuri, wana ubia na makampuni na watu binafsi na tunaona National Housing inavyofanya kazi kubwa katika nchi hii. Kwa nini tusiungane na sekta binafsi katika kuhakikisha kwamba nchi yetu tunapata mapato ya kutosha kwa ajili ya huduma za jamii?
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tuna madeni mengi. Wakandarasi waliotengeneza barabara wanatudai, wanaopeleka vyakula katika shule, inawezekana Mheshimiwa Magufuli amelipa hilo deni, lakini kipindi cha nyuma tulikuwa tunadaiwa na Walimu walikuwa wanadai kwa sababu hatuna mapato ya kutosha. Pia matumizi yetu, hata ukiangalia taarifa ya Waziri, ni makubwa kuliko mapato tuliyonayo, kwa nini matumizi yetu yasiendane na mapato? Hata kama nakisi inakuwepo, isiwepo nakisi kubwa kama iliyopo kwenye ripoti ya Serikali. Tusipoangalia namna tunavyotumia na namna tunavyopata mapato kwa kweli tutabaki kila siku miradi yetu ya maendeleo haikamiliki tukitegemea fedha kutoka nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaolima Nyanda za Juu Kusini wanalima vizuri lakini masoko pia bado shida. Mwaka jana walipiga kelele sana mahindi yanaoza Mbeya, Iringa, Rukwa na Ruvuma. Lazima tutafute masoko ya uhakika kwa wakulima wetu. Tanga kuna matunda mengi lakini hawana soko, hakuna kiwanda. Bado kuna haja ya kuwa na uhakika wa masoko ya wakulima wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimeangalia pia Kitabu cha Wizara, suala la utalii sikuliona vizuri. Kwa sababu utalii unachangia kwa asilimia kubwa katika pato la nchi yetu lakini sikuona mikakati iliyowekwa na Serikali kwa ajili ya kutangaza utalii wa ndani na wa nje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nizungumze pia kuhusu retention kwa mashirika haya yanayoshughulika na mambo ya utalii; ukiondoa retention kwamba fedha zote ziende Hazina, TANAPA itakufa, Ngorongoro itakufa. Kwa hiyo, niombe kabisa suala la retention liangaliwe kwa mashirika ambayo aidha hayafanyi vizuri, lakini mashirika kama TANAPA, Ngorongoro, ambayo retention inawasaidia pia kutengeneza miundombinu kwa ajili ya watalii naomba retention yao wasinyang‟anywe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ngoja nirudi kwangu Dodoma ambako wanawake wanapata tabu ya kubeba ndoo na kuamka alfajiri kwa ajili ya kutafuta maji. Suala la maji Wilaya ya Bahi tumeongea tumechoka. Tuliomba shilingi milioni 500 mwaka jana mpaka bajeti imemaliza muda wake mpaka tukaanza bajeti nyingine hatujawahi kuona hayo maji. Bahi maji ni ya chumvi mno hayafai kwa matumizi ya binadamu. Niiombe Serikali, wanapoangalia namna ya wananchi au miji ile midogo iliyoanza hivi karibuni kupata maji suala la Bahi lisiwekwe pembeni. Shida ya maji Kondoa ni ya muda mrefu, tumeshalizungumza mpaka tumechoka. Suala la maji Wilaya ya Chemba wameshindwa hata kujenga Wilaya, hakuna maji pale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia Waziri wa Maji atakumbuka tumepiga kelele sana kuhusu suala la kilimo cha umwagiliaji na tuliambiwa bwawa kubwa sana linachimbwa pale Farkwa na bwawa lile lingesaidia wakulima wa mpunga wa Bahi, wakulima wa Chamwino, wakulima wa Chemba na baadhi ya wakulima wa Kondoa lakini mpaka navyozungumza hilo bwawa utaratibu wa kujengwa sijauona. (Makofi)
MWENYEKITI: Mheshimiwa, muda wako umekwisha.
MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, najua ni kengele ya pili, lakini taarifa hii haina mpango wa Serikali kuhamia Dodoma.