Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kuchangia katika hoja iliyopo mbele yetu. Nianze kwa kuunga hoja bajeti ya Wizara ya Ujenzi na nikiipongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri zilizofanywa. Ni ukweli usiopingika katika majimbo yetu barabara nyingi sana zimefunguliwa na nyingine zinaendelea kufunguliwa kupitia Mfuko wa TARURA katika fedha za tozo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiupekee nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuidhinisha kazi hii ifanyike kwa sababu tungeweza kutegemea tu bajeti ile asilimia 30 kutoka Mfuko Mkuu wa Barabara kazi hii kubwa isingeweza kufunguka. Kufunguka kwa barabara hizi kunasadia kupungua kwa gharama ya usafiri katika maeneo yetu ambayo walikuwa wanatumia fedha nyingi kufika katika sehemu za huduma za jamii kwa sababu ya kutokuwa na barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kufunguka kwa barabara hizi kunaenda kuongeza mtandao mkubwa katika barabara za TARURA, kunaenda kuhitaji fedha nyingi kwa ajili ya ukarabati na kuziendeleza hizi barabara na huku tukiangalia fedha za ukarabati wa barabara za TARURA ni asilimia 30 ya Mfuko wa Barabara; huku ni asilimia 20 tu ya mtandao katika mtandao wote ukitekelezwa. Mathalani katika Jimbo la Meatu, Wilaya ya Meatu katika mtandao wote ni asilimia 20 tu ndio inatekelezwa kwa kila mwaka kutokana na ile asilimia 30. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni wakati muafaka, tunajua yapo maombi mengi kutoka katika Halmashauri mbalimbali ambazo wanaomba barabara zao zipandishwe hadhi kutoka TARURA kwenda TANROADS. Mimi naomba sasa Wizara ya Ujenzi ipitie maombi haya iweze kuzipandisha hadhi ili tuupunguzie mzigo mkubwa ilionao TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wanafanya hayo wasiisahau Wilaya ya Meatu, barabara ya kutoka Mwanhuzi – Mwamanongu mpaka Mwabuzo ni kilometa 40 ambayo tumeiombea kuipandisha hadhi kutokana na umuhimu wa barabara hii ambayo inaunganisha Meatu na Wilaya ya Igunga. Ni barabara muhimu kiuchumi ambayo wakati wa masika imekuwa ikijifunga na wananchi kushindwa kupita hiyo barabara na wananchi kushindwa kufika Igunga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu umuhimu wa hiyo barabara kutokana na uchumi wa Meatu ambao unategemea pamba. Magari ya pamba yamekuwa yakikwama kutokana na ubovu wa barabara hiyo. Barabara hii inahitaji fedha nyingi kwa ajili ya kufanyiwa matengenezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niiombe Wizara ya Ujenzi watuunganishie sasa barabara kutoka Mwabuzo kwenda Igunga kwa sababu barabara ya TANROADS inayotoka Kabondo mpaka Mwabuzo imeshia hapo halafu ikakosa mwelekeo. Watumishi kutoka Wizara ya Ujenzi walifika wakaikagua ile barabara na waliona wingi wa magari yanayopita kutoka Igunga mpaka Mwabuzo. Niombe sasa watufungulie ile barabara ili wananchi waweze kupita mwaka wote mzima wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana tulipitisha Mpango wa Maendeleo wa Taifa na katika mpango huo kwa mara ya kwanza barabara ya Kolandoto – Lalago – Nghoboko – Mwanuzi mpaka Sibiti iliingizwa katika mpango wa maendeleo na sisi Wanasimiyu tulifurahi. Isitoshe katika mwaka wa kwanza wa utekelezaji wa mpango barabara hiyo iliingizwa katika kutekelezwa baada ya miaka takribani 20 kuwepo tu katika ilani ya uchaguzi bila kuingizwa katika mpango wa maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ilipoingizwa kiasi cha shilingi milioni 5,000 kilitengwa kwa ajili ya barabara hiyo na walianza kwa kutengeneza daraja la Mto Itende, lakini ni mwaka mzima kuanzia Julai mpaka leo ninapoongelea ni mchakato wa manunuzi unafanyika. Mimi najiuliza kama ni kipande hicho tu kidogo mwaka mzima tunafanya mchakato wa manunuzi, je, tutakapopokea yale mafedha tunayoyategemea kutoka wahisani tutafanyaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niiombe Wizara iangalie hii changamoto kwa nini miradi mingi changamoto iliyopo ni mchakato wa manunuzi? Mara tender imerudiwa, mara mchakato mwaka mzima na kuendelea. Hii inakwamisha utekelezaji wa maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ile barabara kuna Daralja la Sibiti ambalo liligharimu takribani shilingi bilioni 34.4 kujengwa. Barabara hiyo imechukua muda mrefu na imetekelezwa, lakini imekosa tija kwa sababu zifuatazo; kwanza kuna kilometa 25 ambazo ilinyanyuliwa mbuga, magari mengi kwa sasa hivi hata kiangazi hayapiti kwa sababu changarawe ile inapasua madaraja, kwa hiyo, inawalazimu kuzungukia Shinyanga. Mwaka jana ilitengwa fedha, lakini mwaka huu sijaona hata nini kinaenda kufanywa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe hizo kilometa 25 za maingilio ya Daraja la Sibiti zitengenezwe kwa kiwango cha lami kwa sababu magari makubwa yanayoleta mizigo inabidi yazunguke kwa sababu inachana matairi, lakini sababu ya pili, daraja lile lilitengenezwa kwa gharama kubwa, lakini sasa hivi linaanza kumalizwa na mvua, kwa hiyo, itaigharimu tena Serikali kuanza kulinyanyua tena ili liweze kutengenezwa kwa kiwango cha lami. Daraja hili linakosa manufaa kwa ajili ya ile mito iliyopo upande wa Meatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ni kubwa. Mito hiyo imekuwa ikipoteza maisha ya wananchi, mito hiyo imekuwa ikizifunga kata zilizopo ng’ambo ya pili kuja Wilayani, lakini wananchi wamekuwa wakipoteza mali zao kutokana na mito ile inapojaa maji, wanafunzi wamekuwa wakishindwa kwenda shuleni kwa sababu ya mito ile kujaa maji. Niiombe sasa Serikali kama imekusudia kutekeleza ifanye basi ili lile daraja liweze kupata thamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Nashukuru sana. (Makofi)