Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. George Ranwell Mwenisongole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa hii nafasi na mimi kuchangia kwenye hii Wizara muhimu sana katika maendeleo na ustawi wa nchi yetu. Nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma kwanza kwa anavyotujalia uhai na anavyoendelea kuibariki nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipekee nimshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi anavyohangaika kutafuta fedha kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka nimuulize Mheshimiwa Waziri kwamba anafahamu katika Tanzania kuna Mkoa unaitwa Mkoa wa Songwe? Labda nafikiri hajui katika huu mkoa kwa sababu nimesoma hotuba nzima ya Wizara hii ambayo Naibu wako naye anatoka kwenye huo huo mkoa. Tulichopewa sisi kule ni ahadi tu, lakini hakuna hata mradi mmoja wa barabara wa lami ambao utafanyika ndani ya huu mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nataka nimuulize Mheshimiwa Waziri hivi mnavyokuwa mnapanga hizi barabara kujenga lami mnatumia kigezo gani kati ya Mikoa na Mikoa? Na kwanini Mkoa wa Songwe kila mwaka unarukwa? Kila wakati kila mwaka, mwaka jana wakati naingia hapa Bungeni niliuliza swali hili na mara nyingi nimeuliza sana barabara zetu, lakini ukiangalia Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Songwe inaachwa nyuma sana kwenye hizi bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nataka Mheshimiwa Waziri utakapokuja ku-windup hii hotuba yako utuambie vigezo gani vinatumika katika kuchagua barabara za kuwekewa lami. Maana yake sisi hatuelewi, sasa tusije tukaanza kuwa na fikra zingine ambazo ni za ajabu na siyo sahihi. Lakini mimi nataka nikufahamishe kule katika mkoa wetu wa Songwe ambao tunakukaribisha kwa hamu sana ambao ndio mkoa pekee bado haujautembelea, kuna barabara ya kutoka Mloo kwenda Makao Makuu ya Wilaya ya Momba, Chitete na kwenda mpaka Kamsamvu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya Mkoa wa Songwe hii ni barabara ya pili kwa ukubwa ukiacha hii barabara inayotoka Mbeya mpaka Tunduma. Barabara hii kilometa 145 upembuzi yakinifu umekwishakamilika, usanifu wa kina umekwishakamilika, ipo ndani ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama chetu cha Mapinduzi. Lakini ni ahadi ya Marais wote wa Awamu ya Tano na Awamu hii ya Sita kuhusu hiyo barabara. Lakini sasa hata kutengewa kiasi cha fedha hakuna, taratibu zote za tender zishakamilika. Kinachotakiwa ni kutengewa tu fedha, sasa shida nini Mheshimiwa Waziri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpunga wote unaolimwa kule Kamsamba hii ndiyo njia yake, na ile barabara ikifunguliwa ikijengwa kwa lami kutoka Mbozi mpaka Tabora itakuwa ni kilometa chini ya 700 tu, maana yake inakwenda mpaka Kiliamatundu kutoka pale unaenda Muze, Majiyamoto ushaingia Tabora, lakini sasa nashindwa kuelewa shida ni nini ambayo tunashindwa kutengewa hii barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukiacha hiyo barabara Mheshimiwa Waziri kuna barabara inayotoka Uyole inaanzia Igawa inakuja Uyole mpaka Tunduma, mwaka jana niliongea hapa na nilimwambia Naibu Spika kabla hajawa kuwa Spika; nikwamwambia hii wameweka kwenye bajeti ya mwaka huu lakini fedha haitatoka na kweli mwaka jana fedha haikutoka, mwaka huu mmeiingiza tena kwenye bajeti ya mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini mwaka huu vilevile fedha itatoka. Sasa Mheshimiwa Waziri shida nini? Sasa hivi ukitaka kutoka Tunduma kwenda mpaka Mbeya unatumia zaidi ya saa tatu; kwa sababu ukifika mahali unaambiwa simama, subiri nusu saa kwanza malori yapite. Unaenda tena unatembea kilometa kadhaa unaambiwa simama subiri kwanza nusu saa malori yapite. Sasa uchumi wa kwetu wa mikoa yetu hii miwili ya Mbeya na Songwe unadumaa kwa sababu ya hizi foleni ambazo hazina maana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri, wananchi wa Mbeya na Songwe wamesubiri vya kutosha hizi barabara ziwekewe lami zifanyiwe matengenezo na sielewi shida ni nini? Lakini tukiangalia vilevile ndani ya Mkoa wa Songwe katika bajeti ya TANROADS katika Mikoa yote Tanzania, Mkoa wetu wa Songwe ndiyo unaoongoza kupata bajeti ndogo ya TANROADS na sijui shida ni nini Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ndio maana nimeuliza vigezo gani vinatumika kugawa hii keki ya Taifa kwa hii mikoa? Na hata ukiangalia bajeti inayotoka kwenye hizi fedha kwa Hazina mwaka huu tumetengewa shilingi milioni 100 tu. Sasa shilingi milioni 100 utakarabati nini kwenye barabara yenye urefu wa kilometa 145? (Makofi)

Mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri tunajua sisi Wabunge wa Chama cha Mapinduzi tunaowajibu kwa chama chetu na tunawajibu kwa Serikali kupitisha bajeti, lakini hiki kinachoendelea siyo sawa na kuna kipindi itafika mpaka uvumilivu sisi utatushinda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia tena itafika mahali uvumilivu sisi utatushinda kwa sababu hata kule sisi tunahitaji lami. Inanitia uchungu sana hii barabara ya kutoka kila siku ninaporudi Jimboni kwangu napita hii barabara ya Mtera hii, imewekewa lami sasa hivi inakwanguliwa tena, basi tupeni hata hiyo lami iliyokwanguliwa kwenye hiyo barabara mtupe sisi tuwekewe kule, kuna shida gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wanawekewa lami baadae zinatolewa lami, zinakwanguliwa sisi hata hiyo lami iliyokwanguliwa hatuna. Mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri tunaomba sana wananchi wa Mkoa wa Songwe na Mkoa wa Mbeya barabara zetu nazo zina thamani sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)