Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba hii muhimu sana ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Lupembe kwanza nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anafanya kwa ajili ya nchi yetu na kupeleka maendeleo sehemu mbalimbali za nchi yetu ya Tanzania. Kwa sababu ni wazi kwamba sekta nyingi Mheshimiwa Rais anaendelea kuzifungua na hata Jimbo la Lupembe ambalo mimi ndiye Mbunge wake Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa sana kwenye maeneo ya TARURA na maeneo ya afya na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu eneo hili la barabara, naomba niseme wazi pamoja na Mheshimiwa Waziri kuwasilisha bajeti yake vizuri sana hapa Bungeni leo, nimesoma hotuba nzima ya bajeti ya Mheshimiwa Waziri kwa wananchi wa Jimbo la Lupembe kuhusu barabara ya Kibena - Stop Lupembe - Lupembe - Madeke. Naomba niseme wazi kwamba sitaunga mkono bajeti hii kwa siku ya leo na kama nitaunga mkono wananchi wangu wa Lupembe hawawezi kunielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema haya kwa sababu gani? Sababu ya kwanza nimesoma kwenye hotuba hii ya bajeti ukurasa wa 27 wa hotuba hii unasema kwamba barabara ya kutoka Kibena - Stop Lupembe - Madeke - Ifakara kilometa 270 Serikali inasubiri fedha kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika kwa ajili ya kufanya usanifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi katika ukurasa wa 73 – 74 barabara hii ya Kibena – Lupembe - Madeke ilishaahidiwa ipo namba 22 pale inasubiri kuanza ujenzi wa kiwango cha lami. Maana yake ni kwamba wenzetu Wizarani hata Ilani ya Chama cha Mapinduzi hawajasoma wanapoandaa bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sababu ya pili ambayo napenda kusema hapa nimesoma kwenye vitabu vya bajeti mwaka jana Bajeti ya mwaka 2021/2022 Serikali ilitenga shilingi bilioni mbili na niliongea ndani ya Bunge hili kwa ajili ya barabara hii kwamba hii bajeti ilikuwa ni kidogo sana. Mwaka huu wameongeza mpaka shilingi bilioni tano, lakini siyo ya kuanza ujenzi wanazungumza kuendelea ku-mobilize na kutafuta mkandarasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ya Lupembe imeahidiwa tangu Serikali ya Awamu ya Tatu ya Mheshimiwa Mkapa, imeahidiwa Awamu ya Nne Mheshimiwa Jakaya Kikwete, Awamu ya Tano na bahati nzuri hata Rais wetu akiwa Makamu wa Rais amekuja Lupembe eneo la ujenzi mara mbili amewaahidi wananchi wetu kwamba barabara hii usanifu umeshakamilika inaanza ujenzi. Sasa leo kwenye bajeti hii mwaka wa sita sasa tunazungumza kuendelea kuwa na ahadi ya kutafuta fedha kwa ajili ya mkandarasi na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufunga bajeti yake hii, ili mimi niweze kubadili msimamo wangu wa kuunga mkono hii bajeti au laa, atoe ufafanuzi kwa wananchi wa Lupembe ni lini barabara hii ya Kibena – Lupembe – Madeke inaanza ujenzi? Kwa sababu usanifu ulikamilika tangu mwaka 2014. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili, namuomba sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu hii barabara ina ahadi kubwa za Serikali na viongozi wakubwa wa Serikali, namuomba Mheshimiwa Waziri baada ya bajeti yake hii tuondoke mimi na yeye mgugu kwa mguu mpaka Lupembe akawaambie wananchi barabara hii inaanza ujenzi lini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, hii barabara kama ambavyo nimesema imefanyiwa usanifu tangu mwaka 2014 na wananchi wa maeneo ya Nyombo, maeneo ya Kidegembye, Matembwe, Lupembe Barazani, Igombora, Mfilige mpaka Madeke nyumba zao zimewekwa alama za “X” mpaka leo wanasubiri uamuzi wa Serikari. Hawaendelezi wanasubiri Serikali ichukue uamuzi wa kuanza ujenzi wa hii barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa inapochukua muda mrefu wananchi hao hawajui sasa wafanye lipi, nyumba zao zina alama ya “X”, hawawezi kuziendeleza. Sasa mimi naiomba Serikali ni vizuri tukajua kwamba tunapokuwa tumewaahidi wananchi wetu kutekeleza baadhi ya masuala yanakuwa na athari kwa wananchi wetu pia. Kwa hiyo, naomba pia kauli ya Mheshimiwa Waziri aseme wananchi hawa ambao nyumba zao zina alama ya “X” tangu mwaka 2014 wanapewa matumaini gani leo zaidi ya miaka 10 sasa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeongea mara nyingi ndani ya Bunge lako tukufu. Barabara hii ya Kibena – Madeke ni barabara inayounganisha kati ya Mkoa wa Njombe na Mkoa wa Morogoro na kwenye sera yetu ya ujenzi wa barabara na Waziri anajua vizuri sana, kama nchi tulikubaliana kwamba barabara za mkoa mmoja na mkoa mwingine ni kipaumbele namba moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini barabara hii inaunganisha Mkoa wa Njombe na Mkoa wa Morogoro. Mkoa wa Morogoro unazalisha mpunga mzuri sana katika nchi hii; Mkoa wa Njombe na eneo la Lupembe mathalani kuna viwanda vikubwa vya chai maeneo haya vinaiingizia Serikali fedha za kigeni, lakini barabara hii wakati wa masika mvua ikinyesha siku mbili magari hayatembei, abiria hawatembei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tupo karne ya 21 wananchi wangu wa Jimbo la Lupembe wakitoka kwenye vijiji mbalimbali kwenye hili Jimbo kufika Njombe Mjini kama wanasafari ya kwenda nje ya Mkoa wa Njombe lazima wabadilishe nguo kwa sababu zinakuwa zimechafuka sana. Katika karne ya 21 hatuwezi kuwa na sehemu ya nchi ambayo ina hali kama hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba sana Serikali na Mheshimiwa Waziri, tumeshauri mara nyingi hapa badala ya kuendelea kupanua maeneo mengine kwa sababu nimesoma kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ipo mipango ya Serikali baadhi ya maeneo tunapanua upana wa barabara, yapo baadhi ya maeneo tunaunganisha barabara za Wilaya na Wilaya lakini barabara za Mikoa na Mikoa hatujamaliza kwa mujibu wa sera ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali sana barabara hii ya Kibena – Madeke mpaka Morogoro ipewe kipaumbele ili na wananchi wangu wa Lupembe wajisikie kwamba na wao ni sehemu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo napenda kuchangia ni kuhusu ujenzi wa uwanja wa ndege Mkoani Njombe. Kwenye Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi pia chama changu kimeahidi vizuri kwamba Mkoa wa Njombe kutokana na hali ya uchumi wake kuwa mkubwa na kuwa na mazao mengi ya biashara ikiwemo parachichi na mazao mengine ya kilimo, lakini pia kutokana na kuwa na hazina kubwa ya Mgodi wa Mchuchuma Naliganga kule Ludewa, Mkoa wa Njombe ni kati ya Mikoa muhimu sana katika nchi hii. Ikiwekewa vipaumbele vya Kiserikali inaweza kuwa ni sehemu ya kuinua uchumi wa Taifa letu. Na kwa maana hiyo Serikali iliona umuhimu mkubwa wa kuahidi kwenye Ilani kwamba uwanja wa Njombe utafanyiwa usanifu ili ujenzi wa uwanja wa ndege uweze kufanyika pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma kwenye hotuba sijaona mahali popote ambako jambo hili limeahidiwa na huu ni mwaka wa pili tunazidi kwenda mbele. Namuomba Mheshimiwa Waziri pamoja na kazi nzuri ambazo mnafanya kwenye Wizara hii, tumeshauri kwenye mpango wa Serikali, tunapopanga vipaumbele vya Serikali ni lazima tufungamanishe sekta mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta hii ya uchukuzi na usafirishaji ni lazima ifungamanishwe na sekta ya kilimo. Sasa kama kwenye mikoa ambayo kuna kilimo kikubwa miundombinu haipewi kipaumbele, hatuwezi kukuza uchumi wa nchi yetu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi ndugu naomba niseme kwamba siungi mkono hoja, nitaunga baada ya kupata ufafanuzi ambao nimetoa pale mwanzoni, ahsante. (Makofi)