Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata muda wa kuchangia kidogo katika bajeti ya Wizara hii muhimu kwa uchumi wa nchi yetu na wananchi wake. Kwa sababu ya muda mchache nitazungumzia maeneo mawili kwa haraka haraka.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie barabara yetu ya Itigi – Chaya – Nyahuwa - Tabora. Barabara hii kipande cha Itigi - Chaya kimekamilika kwa asilimia zaidi ya 90; kutoka Nyahuwa - Tabora imekamilika kwa zaidi ya 90% lakini katikati kipande cha Chaya - Nyahuwa bado hakijaanza kushughulikiwa. Niiombe Serikali na Mheshimiwa Waziri kwa kuwa kuna umuhimu mkubwa wa kipande hiki kukamilika na kutumika, kwa kweli tuiangalie kwa macho mengi barabara hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, unapotoka Manyoni kuja Tabora kwa kupitia Singida - Nzega unatumia kilometa 460 kufika Tabora. Unapotoka Manyoni kuja Itigi kupitia Chaya mpaka Tabora ni kilometa 254, kwa kuzunguka unaongeza kilometa 206. Wanaokwenda Kigoma wakipitia Chaya maana yake watapunguza zaidi ya kilometa zaidi ya 206 kwa safari yao. Wanaokwenda Mwanza wakipitia njia ya Chaya - Tabora - Nzega watapunguza kilometa zisizopungua 110 kufika Mwanza badala ya kupitia Singida na Igunga. Barabara hii ni muhimu sana, tunaomba Serikali sasa ifike wakati watuambie mkandarasi anaanza lini ujenzi kipande kile cha Chaya - Nyahuwa.
Mheshimiwa Naibu spika, kwa kweli Mheshimiwa Waziri anajua 100% ya kipande hiki kimepita kwenye jimbo langu, atakapokuja kuhitimisha hapa basi atueleze imefikia wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna maombi ya kupandisha hadhi barabara, maombi yako mengi Mheshimiwa Waziri alituambia lakini basi tuone taratibu maombi yale yanaanza kupunguzwa. Mimi nina kipande cha barabara ya Bwekela - Miswaki - Loya - Iyumbu ambacho kinaunganisha majimbo ya Igunga, Manonga, Igalula na Singida Vijijini. Barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi wa wananchi wetu kwa sababu kuna kilimo kikubwa cha mpunga kule, kuna haja barabara hii itengenezwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nisipozungumzia reli wananchi wangu hawatanielewa. Ukianzia Kalangasi mpaka Igalula reli inapita katika jimbo letu na ni muhimu sana. Juhudi zinazofanyika kuimarisha reli yetu zinaonekana tunaipongeza Serikali. Napenda nimpongeze Mkurugenzi wa TRL kwa kufanya sasa TRL ianze kujiendesha kiuchumi kwa mipango mbalimbali ambayo inafanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na Wabunge waliosema kuna haja ya kuunganisha TRL na RAHCO kwa sababu ya kuisaidia TRL kujiendesha. TRL ili ijiendeshe inahitaji kutengeneza pesa za ndani lakini vilevile iweze kukopa. TRL haina assets za kukopea ili iweze kufanya mipango yake ya kimaendeleo. Assets ziko RAHCO, TRL hawana assets, wanashindwa kufanya mipango mizuri ya kimaendeleo mwisho wa siku wanaitegemea Serikali kwa kiasi kikubwa sana. (Makofi)
Mheshimwia Naibu Spika, ukiangalia RAHCO hawajaiangalia vizuri miundombinu ya reli ambapo ili TRL ifanye vizuri lazima miundombinu ya reli iwe imara. RAHCO hawana wafanyakazi wengi, hawana wataalamu wa kutosha kuweza kui-service reli yetu ikawa inapitika kwa muda wote. Kuna haja kabisa Serikali kuleta sheria hii Bungeni tuiangalie upya, tuunganishe sasa RAHCO na TRL zifanye kazi ambayo italisaidia Shirika letu la Reli kuweza kufanya kazi vizuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, reli ni kiungo muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu. Barabara zinaharibika kwa sababu mizigo mingi inasafirishwa kwenye barabara zetu. Kuna haja kabisa ya kutengeneza mazingira yaliyo bora zaidi ili reli yetu ilete tija na faida katika uchumi wa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana.