Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye hoja mezani ya bajeti ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote naomba niipongeze sana Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri na watendaji wa Wizara. Lakini kipekee nimpongeze sana Katibu Mkuu wa Wizara hii Mhandisi Balozi Aisha Amour, mama huyu ni msikivu na anafikika na nimpe pole kwa mitihani aliyoipata, Mwenyezi Mungu ampe nguvu aendelee na utendaji wake wa kazi. Wizara hii inafanya kazi nzuri, kazi nzuri, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kumpongeza kidhati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya kwa miradi ya miundombinu. Miradi yote mikubwa haijawahi kusimama hata siku moja anatenga fedha za ndani na kwenye safari zake anatafuta fedha za nje, nampongeza sana na tumeambiwa hapa maana wakati mwingine ukipongeza wako watu wanapenda kuhoji. (Makofi)

Tumeambiwa tarehe 25 Mei kule Accra, Ghana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan anakwenda kupata tuzo ya Benki ya Maendeleo ya Afrika (African Development Bank) ya ujenzi wa miundombinu ya barabara na reli, tunampongeza sana wanaotaka kujibu wajiandae kujibu kwa kiingereza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye hotuba ya Waziri ameeleza kazi kubwa Serikali inayoifanya kwenye upanuzi wa bandari zetu nchini na kule bandari kazi kubwa inafanyika. Tunaipongeza Serikali, tunampongeza Mkurugenzi wa Bandari Ndugu Eric Hamisi, niwaombe tuendelee kuiunga Serikali mkono.

Mheshimiwa Spika, tarehe 30 Machi wakati Mheshimiwa Rais anapokea ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa mwaka wa fedha unaoishia Juni, 2021 alitoa agizo muhimu sana ambalo Kamati zako ya Public Accounts Committee na Public Investment Committee imekuwa ikiishauri Serikali kuomba kuisaidia Air Tanzania Corporation Limited. Mheshimiwa Rais aliagiza zile ndege zote zinazomilikiwa na Tanzania Government Flight Agency (TGFA) umiliki wake urejeshwe kwenye Shirika la Ndege la ATC. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, agizo hili linakwenda kuwa na mchango chanya kwenye mizania ya Shirika hili, mizania ambayo kwa vipindi vichache vya miaka ya fedha imekuwa ikipata negative equity ambapo ukienda kwenye notes zake kule kwenye plan tern equipment’s walikuwa na plans and equipment’s zenye thamani yenye shilingi bilioni 119 tu. Ndege hizi 11 zina thamani ya shilingi trilioni 1,473.2 na ndege hizi zikihamishiwa ATC mizania yake sasa inakwenda kuwa chanya. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais tunaamini sasa Serikali itakwenda kusaidia yale madeni hasa ya kurithi ya Aerovista na mengine, madeni yale ya kukodi ndege toka TGFA ambayo ni kampuni dada ama kampuni kaka zote zinamilikiwa na Watanzania na tunategemea, kuanzia mwaka wa fedha unaofuata ambao Audit yake itakuja mwaka 2024 vitabu hivi vitakaa vizuri sana; Engineer Matindi, Mwenyekiti wa Bodi Profesa Morick tunawatakia kila la kheri tutaendelea kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kazi kubwa imekuwa ikifanyika kwenye Shirika la Reli Tanzania, tumekwenda juzi kuzindua Lot III ya awamu ya kwanza kutoka Makutupora kwenda Tabora, tunaomba tuendelee kuwaunga mkono na Masanja Kadogosa ama almaarufu Engineer Masanja Kadogosa aendelee kufanya kazi hii na sisi kazi yetu kubwa ni kuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili sitoacha kulisema nililisema na ninasema tena nitaendelea kulisema, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, Watanzania hata viongozi wa Serikali, haya mashirika yanayofanya biashara yakipata faida yanatoa gawio kwa Serikali na gawio hili linakwenda kufanya maendeleo kwa wananchi wetu. Kama yana mapungufu unazo Kamati zako, ni uwanda mzuri zaidi wa kuyakosoa, tukiyakosoa kwenye uwanda wa wazi clip hizi tunazozisema hapa zinatumiwa na competitor wa mashirika haya kwenda kuwachafua kibiashara halafu tunaanza kujiuliza kwa nini Mashirika hayafanyi vizuri.

Mheshimiwa Spika, pale Dar es Salaam tuipongeze Serikali inatekeleza mradi wa mabasi yaendayo haraka (BRT) awamu ya pili ambayo ina kilometa 19.3 kutoka Mbagala kwa Mheshimiwa Chaurembo inakuja mpaka Kariakoo kwa Mheshimiwa Zungu kutoka pale Kurasini kwa Mheshimiwa Kilave inakwenda mpaka Magomeni kwa Mheshimiwa Tarimba. Mradi ule una mkandarasi wa Lot I na Lot II mwezi Disemba wakati Mheshimiwa Rais amealikwa kuzindua Lot II kuna maneno aliyasema naomba kuyanukuu na ulishatuelekeza jinsi ya kunukuu kauli za viongozi na nimezingatia. (Makofi)

Mheshimiwa Rais alisema: “Mwezi Juni nadhani nilifanya ziara ndani ya Wilaya ya Temeke, lakini nikapita pia barabara ya BRT na nikakuta ubovu ambao Waziri umeutaja na nikaeleza hatua zichukuliwe na ubovu ule kama viongozi wasingesimama na kusema hapa ni pabovu mkandarasi angeendelea na kutujengea ubovu ule ule. Kwa hiyo, niombe sana viongozi wa Wilaya, Halmashauri mlioko huko muwe macho lakini wakati mwingine nao labda na sisi Serikali tuna tatizo kwa sababu unaweza kukuta mkandarasi mmoja ana kazi nne, tano kwa wakati mmoja. Sinohydro utaikuta kwenye hydropower kule Nyerere, Sinohydro utaikuta kwenye BRT, Sinohydro iko Msalato, Sinohydro iko Maji, Sinohydro iko kule kwenye umeme sasa mkandarasi mmoja maeneo yote hayo lazima atavuruga. Kwa hiyo, mnaotoa tender hizi nanyi muwe makini kuangalia nani yuko tayari kujenga miradi tunayowapa.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waziri alikuwepo, TANROADS walikuwepo na Sinohydro walikuwepo. Wakati Mheshimiwa Rais anasema nadhani wenzetu mioyoni walikuwa wanasema mama sema haraka umalize kwa sababu sio kazi nne, tano tunakwenda kumpa kazi ya sita.

Mheshimiwa Spika, Sinohydro amepewa mradi wa mabasi yaendayo haraka awamu ya tatu toka Gongolamboto mpaka Kariakoo. Mkandarasi huyu ambaye tayari kilometa 2.5 zimetinduka zimeweka ufa kule Mbagala ,mkandarasi huyu asiyelipa wafanyakazi, mkandarasi huyu asiyelipa wazabuni amekwenda kuongezewa kazi nyingine. Kazi hii ya kilometa 23.6 inapatikana ukurasa wa 69 wa Ilani hii ya Uchaguzi, wala haikusema tutajenga mradi wa mabasi yaendayo haraka awamu ya tatu na tutampa Sinohydro; ilisema tutakwenda kutatua kero kwa wananchi wetu wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ndio Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi, amesema hadharani, ameonya, mmekwenda kutoa kazi ile. Mheshimiwa Rais kule Mbagala alisema alikwenda mwezi Juni, akaenda Disemba, hii Nyerere ndio anapita kila siku kwenda kwenye safari zake kwenda kutafuta fedha kwa ajili ya miradi kama hii. Mnakwenda kufanya vitendo vya namna hii.

Mheshimiwa Spika, Bunge lako hili na wewe ukiwa Spika ndio litakuwa Bunge ambalo limesimamia bajeti hii ambayo inakwenda kututengenezea kero ambayo leo iko Mbagala, iko Temeke inakwenda kurejeshwa tena kwa Gongolamboto na maeneo mengine tutakuwa ni Bunge la namna gani? Mkuu wa Wilaya pale Temeke Jokate Mwegelo alikwenda kusimamia haki za wale wananchi wanaonyanyaswa na wale Wachina, TANROADS wakamuandikia barua usiingilie mikataba hii ya ujenzi inayosimamiwa na TANROADS. Kuna mkataba unaosema mtu asilipe watu? Ndio TANROADS hii, halafu ukisema unaonekana una jambo lako binafsi, jambo gani binafsi? Hatuwezi kuacha watu hawa wakaendelea kufanya kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jambo nilisema hapa na kuna watu walinifikiria vibaya haya mambo ya single source. Single source sio mbaya competitive tender sio mbaya ubaya ni uadilifu wa wale wanaosimamia kazi hizi. Mradi wa mwendokasi awamu ya kwanza kutoka Kimara mpaka Posta umejengwa na STRABAG leo mwaka wa sita, wa saba hata shimo moja halijatokea. Hivi wangempa DRT Phase III Single Source STRABAG kuna mtu angelalamika? Kwa nini wanafanya hivi? Leo nenda pale Arusha mradi wa shilingi bilioni 520 una Lot 13; Lot 12 zimekamilika, Lot moja ya Sinohydro mpaka leo haujakamilika wananchi hawapati maji kwa sababu ya Sinohydro. Vyanzo vya maji vimekamilika matenki yamekamilika ila mtu mmoja anafanyakazi kwa utaratibu anaoona yeye unafaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na nimuombe Waziri akija hapa kujibu mimi nitashika shilingi ya mshahara wake, nitashika shilingi ya Fungu la TANROADS ukiwauliza, wanakujibu eti World Bank walitoa letter of no objection, msituletee habari za namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Manunuzi Sura ya 410 ya mwaka 2011 TANROADS ndio procurement entity ndio anaandaa nyaraka za zabuni, ndio anaandaa sifa za mwombaji. Mmetunga mtihani wenyewe, mmempa majibu wenyewe, mmehakikisha ameshinda, Rais ametoa kauli bado mnakwenda kumpa kazi mnataka nchi iende namna gani? Sisi tunakwenda kwenye uchaguzi 2025… (Makofi)

(Hapa Mhe. Jerry W. Silaa alilia)

SPIKA: Haya ahsante sana Mheshimiwa muda wako umekwisha.