Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi jioni hii ya leo na mimi nitoe mchango kwenye Wizara hii. Awali ya yote nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha mimi kusimama jioni hii ya leo nikiwawakilisha Wanaliwale, nikifikisha vilio vyao Wanaliwale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaenda huko naomba nitoe utangulizi kidogo maana nasikia watu wanalalamika reli, reli, reli, reli. Mbona haijengwi, mbona haijengwi. Nataka niwape faida moja, tatizo la Serikali yetu ni kutanguliza mipango kabla ya nia au dhamira. Sisi kwenye uislamu tunaamini kwamba, mtu unatakiwa utangulize nia, kwanza nia iwepo utende jambo; haiwezekani katika karne ya 21 Tanzania unasafirisha mafuta kutoka Dar es Salaam kwenda Kigoma kwa gari! Unasafirisha mafuta kutoka Dar es Salaam kwenda Mtwara kwa gari! Bandari Mtwara ipo haiwezekani! Hivi Wajerumani wakati wanajenga ile reli tuliwaona wendawazimu? Wamechukua tu nchi wakajenga reli, sisi leo karne ya 21 tunategemea malori, miaka 54 ya Uhuru hapa hatuendi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wakandarasi mnaowapigia kelele, mnawalalamikia wanajenga barabara, maana gari likipiga kona na barabara nayo inapiga kona! Hawa tutaendelea kuwalaumu, hata aje malaika ajenge hiyo barabara kwa malori yale yanayopita kwenye hizo barabara haziwezi kudumu, cha msingi tubadilishe mindset zetu. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunalalamika kwamba, wenzetu sijui Kenya, sijui Rwanda, sijui nani, wameamua kufanya kazi! Wale wameamua kufanya kazi wametoka maofisini wanafanya kazi. Ndugu zangu Watanzania leo hii Mtanzania ukikabidhiwa mradi cha kwanza ni kutafuta kiwanja, cha kwanza ni kuagiza gari, tunakwenda wapi? Hatuwezi kwenda! Tena basi kama wewe ni Meneja wa Mradi, mradi unakwisha huna nyumba, huna gari, jamii inakucheka, unaonekana wewe fala! Tubadilishe mindset zetu, tuondoe ubinafsi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nataka niwaambie reli hii kama Waziri huyu aliyekuja leo anadhamira ya kujenga mimi nitaiona. Huwezi kupingana na hawa wafanyabiashara wa malori, mtu ana malori 2000, 3000, 5000, hivi unayapeleka wapi? Nani atakubali reli ijengwe? Tuache kubabaishana, turudi kwenye uhalisia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye viwanja vya ndege. Mheshimiwa Waziri mimi sielewi Mzee Kawawa aliacha usia gani kwa Wilaya ya Liwale, ile miradi yake yote iliyokuwepo yote imefutwa. Sijaelewa kabisa, kabisa tatizo ni nini! Pengine Waziri atakapokuja atanieleza pengine kuna maagizo special Mzee aliyaacha ile Wilaya muisahau kwa kiwango hicho. Sisi Liwale kulikuwa na kiwanja cha ndege leo hii kuna miti unaweza kuchuma hata matunda ule uwanja wa ndege haupo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye upande wa mawasiliano ya simu. Mawasiliano ya simu kwa Wilaya ya Liwale jamani tunaomba mtutoe kisiwani. Mimi namuomba Mheshimiwa Waziri kwa heshima na taadhima muitoe Liwale kisiwani, Liwale kuna tatizo la barabara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru Mheshimiwa Rais aliyepo madarakani, mnyonge mnyongeni haki yake mpeni, amekuwa muadilifu. Aliulizwa hapa habari za barabara Nangurukulu – Liwale akasema haiko kwenye mpango wa kujengwa kwa lami na kwa kulikumbuka hilo alipokuwa anaenda kuomba kura Liwale hakuja, alijua kwa sababu wameshakataa kwamba hiyo barabara hatowajengea kwa kiwango cha lami na kweli hakujenga na alipoenda kuomba kura hakuenda Liwale kuomba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi namshukuru pengine angekuja nisingekuwa hapa sasa hivi. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hakuna barabara mimi naomba Mheshimiwa Waziri ututoe Liwale kisiwani. Tuna barabara ya Nachingwea – Liwale, kilometa 120, sijaiona kwenye hotuba yako yote. Kuna barabara ya Nangurukuru – Liwale kilometa 230 sijaiona kwenye mpango wako wote, tunakosa nini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kwa jinsi Liwale ilivyo na rasilimali za kutosha, tunazo mbuga za wanyama, tunayo mazao ya misitu, tunao wakulima wanalima ufuta, wanalima korosho. Tungekuwa na barabara Liwale tusingekuwa walalamikaji kama tunavyolalamika leo upande wa afya, tunaolalamika upande wa elimu, tungeweza kujenga hospitali zetu. Hizi zahanati tungeweza kuziwezesha kwa mapato ya Halmashauri, leo Liwale imefungwa, Halmashauri inapata wapi mapato?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi namuomba Waziri atusaidie, atuokoe, atuondoe kisiwani. Nimeona kwenye mpango kuna barabara inatoka Mtwara – Newala – Masasi – Nachingwea inarudi Nanganga; nikupe umbo la hiyo barabara ina “U”, chini ya hiyo “U” ndio kuna Liwale, hebu muone Liwale ilivyotengwa. Yaani umechora “U”, umetoka huku umekwenda ile “U” chini ndio kuna Liwale, wameiacha huko chini! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi watu wale wakiona kwamba CCM haiwataki, wana haki au hawana haki? Mmetengeneza “U”, inatoka Mtwara – Newala – Masasi – Nachingwea inarudi Ruangwa – Lindi, Liwale iko chini! Tunawatendea haki watu wale na tunawahitaji?
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ninakuomba kwa heshima na taadhima uiondoe Liwale kutoka kisiwani. Tatizo kubwa ninaloliona hapa, tatizo kubwa, Chama cha Mapinduzi tangu Uhuru mnaongoza hii nchi, lakini hii nchi kila siku inazaliwa upya! Kila tunapobadilisha uongozi nchi inazaliwa upya. Kwa maana ya kwamba, kila Rais anayekuja ana vipaumbele vyake, hatuwezi kufika! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, alikuja Mheshimiwa Mkapa na Mtwara Corridor, Mheshimiwa Mkapa kaondoka na Mtwara Corridor imekufa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sijui kama ipo tena?
Mheshimiwa Mwenyekiti, atakuja huyu na lake, mimi nafikiri, sijui tuseme waongoze milele, sijui kama Rais mmoja abaki tu, sijui tufanyaje? Maana kila tunapobadilisha pamoja kwamba chama ni kile kile, watu ni walewale, lakini mikakati yao ni tofauti kabisa. Utafikiria aliyekuja ni tofauti yaani utafikiri ni chama kingine na nchi ni nyingine...
Mheshimiwa Mwenyekiti, tena kwa kujisifia kabisa kwamba Tanzania inazaliwa upya! Inazaliwa upya kwa kuyaacha yale ambayo yalipangwa awali.
TAARIFA....
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hiyo sijaipokea kwa sababu zifuatazo; amesema Mtwara Corridor bado ipo, anaweza kuniambia Mtwara Corridor ilikuwa ni mradi wa miaka mingapi? Na uliishia wapi? Na ulitengewa fungu kiasi gani? Na ni kwa miaka mingapi? Na utekelezaji wake leo umefika wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtwara Corridor ilikuwa inatuunganisha sisi mpaka Msumbiji, leo hii huyu mchangiaji aliyetoka hapa anaongelea suala la kutuunganisha na Msumbiji. Eti mtu anakuja anasema Mtwara kule. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua hili ni tatizo la watu kutokujua jiografia ya Tanzania. Watu jiografia ya nchi hii hawaijui na ndio maana leo hii ukiongelea barabara ya Kusini mtu anakwambia daraja la Rufiji! Mimi nataka niwaambie daraja la Rufiji halina tofauti na daraja la Ruvu kwa sababu mtu leo anadai barabara ya Kigoma unamwambia daraja la Ruvu, inaeleweka?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio hicho mnachokifanya! Maana tukiwaambia jamani tunahitaji barabara ya Kusini, aah, ninyi Kusini sijui mmetengenezewa daraja la Mkapa. Daraja la Mkapa ndio nini sasa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kuanzia leo hii Kigamboni nako wamepata daraja lile huku Kimbiji, Gezaulole, nani, hawaitaki tena barabara kwa sababu, wanadaraja la Nyerere. Tunakwenda wapi? Mbona tunakuwa wavivu wa kufikiri? Mbona tunakuwa wavivu wa kufikiri! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nafikiri tunahitaji kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji kufanya kazi nchi hii, tunahitaji watu…
MWENYEKITI: Mheshimiwa, muda wako umeisha, naomba ukae tafadhali.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.