Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa mwisho. Awali niipongeze sana Serikali kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya hasa ya kupeleka miradi ya maendeleo, hasa kwenye miradi mikubwa ambayo imeanza kutekelezwa na inaonekana mbele ya nchi yetu. Miradi hiyo hiyo mikubwa ni kama ujenzi wa reli, barabara, miradi ya umeme, miradi ya maji, miradi ya elimu ambayo kimsingi imekuja kuwa na mafanikio makubwa sana mbele ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninalo eneo moja ambalo ningependa kulichangia kwa kina kuishauri Serikali. Bahati mbaya tu leo hata wasaidizi wa Waziri ambao wanaweza wakachukua mawazo ya Wabunge hawapo kabisa, yupo Waziri na Naibu Waziri, lakini yapo mambo ya msingi ambayo tunaweza tukalisaidia Taifa letu ili liweze kuepukana na kodi tunazozichukua kwa wananchi za kila mwaka kwenye eneo la mafuta na eneo la bia na kwenye maeneo mengine madogo madogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana niliishauri Serikali, lipo eneo ambalo hatujawekeza kabisa na kuna fedha nyingi na wenzetu wananufaika sana. Nchi yetu imebahatika kuwa na misitu mingi na sasa hivi tunapata fedha nyingi kwa sababu dunia nzima wanahamasa kubwa ya uvunaji wa hewa ya ukaa, kwa sababu mataifa ya nje yameharibu hali ya hewa huko duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa fursa tuliyonayo sisi Watanzania hatujaitumia vizuri kabisa. Ninao mfano, Nchi jirani ya Kenya, wenzetu wanavuna hewa ya ukaa kwa mwaka wanapata dola bilioni moja ambazo wanazivuna kupitia kwenye hifadhi zao. Sisi nchi yetu Tanzania ina maeneo makubwa mno karibu kila sehemu tuna Hifadhi za Taifa, tuna misitu inayomilikiwa na TFS, tuna misitu inayomilikiwa na vijiji, nchi yetu tu tunao uwezo wa kuvuna karibu tani zinazoweza kutoa shilingi trilioni 6.9 kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tungepata hizi fedha zingeweza kutusaidia kuepukana kuwakamua wananchi kupitia kwenye mafuta, lakini bahati mbaya Wizara hawajatoka ofisini na hatujazitumia Balozi zetu zilizoko huko nje. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, eneo hili lina fedha nyingi na inawezekana mkawa mnaona kama hadithi. Nchi ya Brazil inavuna hewa ya ukaa na asilimia kubwa wanatumia hizo fedha kwa ajili ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetolea mfano Nchi jirani ya Kenya, wao wanavuna hewa ya ukaa karibu dola bilioni moja. Sisi tuna nafasi ya kufika dola bilioni tatu ambazo zinaweza kutupelekea shilingi trilioni 6.9. Tunao mfano ambao kwa nchi yetu tayari walishaanza kuvuna hewa ya ukaa. Katika Jimbo langu wanavuna hewa ya ukaa kupitia misitu ambayo ipo, kati ya shilingi bilioni nne na wanaweza kufika mpaka bilioni 30 na kuachana na utegemezi wa kutegemea Serikali Kuu. Eneo hili ni eneo muhimu, waendeni wakajifunze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Pakistan baada ya kupata tatizo la mafuriko, yale maeneo ambayo walihama wananchi wao saa hizi wanayatumia kwa ajili ya uvunaji wa hewa ya ukaa. Mheshimiwa Waziri aende akalifanyie kazi eneo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo aina tatu za uvunaji wa hewa ya ukaa na inawezekana hata kwenye Wizara yake Mheshimiwa Waziri hajui hivi vyanzo. Kuna soil carbon ambayo inazalisha organic kwenye eneo la agriculture, wanaweza kupata fedha huko. Kuna eneo lingine ambalo ni kwenye blue carbon inayopatikana kwenye Maziwa Makuu na ufukwe wa Bahari, katika maeneo hayo yote wanaweza wakapata fedha hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tunayo green carbon ambayo inaweza ikazalisha fedha nyingi kupitia misitu tuliyonayo. Maeneo haya Serikali haijawahi kuyafanyia kazi, tunakaa tu kwa ajili ya kuhakikisha wanyama wanaongezeka na wakiongezeka ndiyo wanaoenda kuleta shida kwa wananchi, kula mazao ya wananchi. Eneo hili Waziri aende kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua wana mipango mizuri ambayo Serikali wanategemea kupeleka fedha. Mimi kwenye eneo langu Jimbo la Mpanda Vijijini, tunayo Barabara ya kutoka Kabungu kwenda Kalema, Serikali wamewekeza ujenzi mkubwa sana wa bandari karibu shilingi bilioni 48. Zile fedha ni kama wameenda kuzi-dump, muhimu ni kujenga ile barabara ili waweze kuunganisha na nchi jirani ya DRC, Congo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo wenzangu wa Mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma wamezungumzia umuhimu wa kuwepo kwa meli itakayofanya shughuli za maendeleo kwenye Ziwa Tanganyika. Ziwa Tanganyika ndiyo pekee ambalo halina usafiri wa aina yoyote na kwenye maeneo ambayo yana mzigo mkubwa sana ni Ziwa Tanganyika, tunayo Bandari ya Kasanga ambayo ikitumika vizuri itaunganisha na eneo la Lubumbashi upande wa Congo, Bandari ya Kalema yatakayounganishwa na Mji wa Kalemie, lakini tunayo Bandari ile ya Kigoma itakayounganisha na nchi ya Burundi na Kongo ya Mashariki kwa maana ya Miji ya Uvila na Goma wanaweza wakatumia hiyo na tukatengeneza uchumi mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali tujenge barabara ya haraka na ya dharura ili iweze kuunganisha na ile bandari ambayo tumeijenga kwenye maeneo yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo tunaomba kwa Mheshimiwa Waziri, tunaomba fedha za dharura za Mkoa wa Katavi, Mkoa wa Katavi kwa sasa hauna umeme. Tunaishukuru Serikali ilileta jenereta, lakini kadri ya idadi ya watu na shughuli za maendeleo zinavyokuwa tayari Mkoa wa Katavi una shida kubwa sana ya upatikanaji wa umeme. Nimwombe Mheshimiwa Waziri kwenye hii bajeti wapeleke jenereta mpya ambayo inaweza kwenda kusaidia na kutatua kero ya wananchi. Wakati tunasubiri ule mradi mkubwa wa Gridi ya Taifa bado kuna haja ya kupeleka umeme wa dharura kwenye eneo hilo ambalo litasaidia ukuaji wa kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuiomba Serikali kujenga mradi mkubwa wa maji. Nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha ampe Waziri wa Maji ajenge Mradi mkubwa wa Maji kutoka Ziwa Tanganyika kuleta Makao Makuu ya Mkoa pale Mpanda Mjini. Watakuwa wamewasadia wananchi na hilo linawezekana, kama maji wanayatoa Ziwa Victoria na wana mpango wa kuyafikisha mpaka Dodoma ambako ni eneo la kilometa nyingi zaidi ya kutoka pale, kutoka Mji wa Kalema hadi Mpanda ambao ni kama kilometa 100. Nina imani Serikali ikiwa na dhamira ya dhati wanaweza wakawasaidia wananchi wa Mkoa wa Katavi na wao wakanufaika na keki ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana, lakini narudia kuisisitiza Serikali, wapate mawazo kutoka kwa watu wa chini, wana uwezo kabisa wa kuweza kupata mbadala wa fedha. Mawazo ya Wabunge tunapoishauri Serikali kwamba iache kukamua watu hapa, kuna eneo lingine walifanyie kazi, huko ndiko ambako tunaishauri Serikali. Naamini na nina uhakika, chanzo hiki cha mapato wakikitumia vizuri Serikali watapata fedha nyingi na wana uwezo mkubwa sana wa kukusanya mapato na nchi ikanufaika, ahsante. (Makofi)