Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kupata nafasi jioni ya leo na ninafikiri hii imekuwa ni tabia yangu ya kupata nafasi jioni. Kwanza kabisa natoa shukrani za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo anaitekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi lakini kubwa kabisa kwa kweli katika siku mbili tatu hizi zilizopita tuna mijadala mikubwa sana inayoendelea huko nje ikihusiana na suala zima la uwekezaji wa bandari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kusema ukweli kupitia jambo hili nampongeza sana Mheshimiwa Rais kuwa amepata utulivu, ametulia, ameruhusu watu wanafanya mjadala kwa kadiri wanavyopenda na yapo mambo mengine yanazungumzwa yana kera katika nafsi ya kawaida lakini kama kiongozi amenyamaza anawasikiliza kwa hiyo nampongeza sana na tunamwombea afya aendelee kuwasikiliza lakini viongozi wanaomsaidia waendelee kuyapokea yale yanayotolewa kama sehemu ya ushauri na kuyafanyia kazi ili mambo yale yanayokusudiwa na nchi hii yaweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo nimpongeze Mheshimiwa Waziri. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri na wataalamu wake wote pamoja na Naibu Waziri kwa Hotuba nzuri ya Bajeti ambayo ametuwasilishia na Mpango mzima ambao umekuja mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika jambo hili ningeomba nikumbushe jambo moja. Mheshimiwa Waziri utakumbuka mwisho wa Bajeti moja inayowasilishwa na kupitishwa na Bunge ndiyo mwanzo wa maandalizi ya Bajeti nyingine na kila Bajeti ina mapokeo yake kwa wananchi, ina mapokeo yake kwa viongozi ambao tuko humu Bungeni na kila Bajeti ina dhima yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhima ya Bajeti ya mwaka jana ilikuwa ni Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu. Nakumbuka wakati Mheshimiwa Waziri anawasilisha Bajeti ile kila Mbunge aliyesimama alisema kwa kadiri alivyoweza kwamba ni Bajeti ya pekee na niseme tulikuwa tunasema ni Bajeti ya pekee kwa namna ambavyo aliiwasilisha na kuonesha Serikali inajiandaa kwenye kufunga mikanda na kupunguza matumizi makubwa ya Serikali ili kuelekeza fedha kwenye miradi ya maendeleo na kuwafikishia wananchi maendeleo kwenye maeneo mbalimbali vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa lipo jambo ambalo nafikiri Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa nafikiri atupe kidogo takwimu tumeokoa nini kutokana na msingi wa bajeti ya mwaka jana. Kwenye mazungumzo ya mwaka jana tulisema tutafunga mikanda lakini alisema atabadilisha namna bora ya ununuzi wa magari kwa viongozi mbalimbali katika nchi hii na lengo la kufanya hivyo ilikuwa ni kuhakikisha kwamba tunaokoa baadhi ya fedha na zinakwenda kusaidia miradi mingine ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kabla sijatoa mchango wangu huku ningemuomba Waziri kwa sababu Watanzania ambao sisi ndiyo wawakilshi wao wanataka kuona ni namna gani tumeokoa kwa sababu ndani ya Bajeti ya mwaka jana kulikuwa na bajeti ya manunuzi ya magari na mambo mengine. Sasa ni kwa kiwango gani tumeweza kunusuru fedha ambazo zinaweza zikafanya kazi kwenye maeneo mengine na ninasema hivyo kwa sababu nimejaribu kusikiliza hotuba sikuweza kuona ni kiasi gani kimeelekezwa kama sehemu ya kuokoa fedha za mwaka jana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapa nirudi kwenye, nijielekeze kwenye mchango wa mwaka huu. Bado mwaka huu pia tumekwenda na dhima ile ile ambayo tulikuwa nayo mwaka jana. Mwaka jana tulikuwa na dhima hiyo ya kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu. Tunapozungumza maendeleo ya watu tunataraji kila mmoja kwenye maeneo ambayo anayaongoza aone baadhi ya mambo yanakwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuna miradi mingi imetekelezwa, tunampongeza Mheshimiwa Rais na Wanatanzania wanapongeza kwa namna ambavyo miradi ile imetekelezwa. Tumeingia mwaka huu tunatarajia kuwa na uwekezaji mkubwa sana wa bandari. Uwekezaji ambao mimi Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini na Wananchi wa Kibaha Vijijini tunapongeza sana Serikali kwa maamuzi mazito ya kuhakikisha kwamba tunaweka mwekezaji pale na kupata fedha za kutosha za kuendesha miradi mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema hivi kwa sababu sisi watu wa Jimbo la Kibaha Vijijini tunao pale Mradi wa Bandari Kavu na ukiangalia ili Bandari ya Dar es Salaam iweze kufanya vizuri ni lazima kuwe na maandalizi mazuri kwenye lile eneo la Bandari Kavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bandari Kavu ya Kwala inapata bahati inaungana na barabara kubwa ya Morogoro Road kwa kupita pale Vigwaza lakini inapitiwa na reli mbili zote muhimu. Sasa nilikuwa na ushauri pale kwamba kwa kuwa ile bandari inategemea kupokea mizigo ya kutokea Dar es Salaam ni vizuri tukahakikisha kwamba tunafanya maandalizi hata wale wananchi walio jirani na bandari ile wanasikia amani kupokea uwekezaji huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu gani? Nilikuwa natoa michango katika baadhi ya Wizara zilizopita lakini nilizungumzia sana suala zima la migogoro. Bandari ya Kwala ambayo ndiyo inatarajia kuwa sehemu ya upungufu wa mizigo ya Dar es Salaam wananchi wake bado kuna maeneo vijiji vya jirani vina migogoro na Serikali. Ni vizuri Serikali ikajielekeza kwenye maeneo hayo ikaondoa hiyo migogoro ili wananchi wakawa na amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale watu wa Kwala kwenye eneo la Waya wana tatizo la kuambiwa wanatakiwa wahamishwe kwa sababu lile ni shamba la mifugo. Wale watu wa Mwembengozi katika Kata ya Dutumi wanaambiwa eneo ambalo limewekezwa kuwa na Kongani ya Viwanda siyo eneo lililokuwa la vijiji kwa hiyo na wao waondoke wapishe uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi ningeishauri Serikali tunapokwenda kufanya uwekezaji kwa ajili ya wananchi, tunataka kupata maendeleo kwa ajili ya Watanzania hawa ni vizuri tukamaliza migogoro hii ili wananchi walio maeneo hayo na wao wakawa na amani ili waweze kufaidi michango ya wananchi wengine ambayo inakuja kuendelezwa katika maeneo yale. Hakuna busara itakayokuwa inapendezwa na watu walioko kwenye eneo hilo ikionekana kuna uwekezaji mkubwa unafanywa lakini wao wanaonekana siyo sehemu ya uwekezaji huo. Katika hali ya kawaida binadamu hawa waliokuwa jirani na eneo hilo watakuwa na kinyongo na kinyongo kikimzidi mwanadamu basi anapatwa hasira na hatimaye anaweza akaingia kwenye mgogoro mwingine na anayemsababishia hasira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wazo langu na ushauri wangu ningeiomba Serikali hasa Wizara ya Ardhi iende ikasaidie kutuliza ile hali kule ili miradi ile itakapokuwa imekuja kuendelezwa katika maeneo yale wananchi wale nao wajisikie amani kwa sababu ni jambo jema kwa sababu linakuja kuleta maendeleo katika maeneo ambayo wanaendeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo katika Jimbo la Kibaha Vijijini nizungumze kidogo kwenye maeneo ya Jimbo la Kibaha Vijijini ni Jimbo ambalo limekaa kimkakati kwa ajili ya miradi mingi ya kimaendeleo ikiwemo ujenzi wa viwanda na ni dhahiri shahiri kwamba unapojenga viwanda katika maeneo mbalimbali unafungua wigo kwa ajili ya uwekezaji na tunapata wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi hii na tunatarajia kwenye eneo hilo kuwe na kiwango kikubwa cha ukusanyaji wa mapato ya Serikali lakini sasa ukiangalia hali halisi iliyo leo, zipo barabara zinazounganishwa na sehemu ambazo tunatarajia kukusanyia fedha hazijawekewa mikakati mizuri. Ningeishauri Serikali ikafanye utaratibu wa kuweka mikakati ya kimiundombinu ili wawekezaji wanapofika kwenye maeneo yale waweze kuwekeza na miundombinu ikiwa imekaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wa maeneo hayo pale Ngimi – Mlandizi kwenye eneo moja la Gisunyara kuna eneo la Kongani ya Viwanda kama ekari 1,000 tayari amekabidhiwa mwekezaji Kamaka na anaendelea vizuri sana na utekelezaji wa mradi ule lakini ukiangalia barabara inayotoka Mlandizi kwenda kwenye eneo hilo la Kamaka yenye urefu kama wa kilometa nane hivi au sita ni mashimo, utaratibu wa kuishughulikia umekuwa mgumu, uendelezaji wa eneo lile unakuwa shida. Ni vizuri Serikali ikaondoa tatizo la barabara ile japo kwa kilometa hizo nane ili mradi tu pale katika lile eneo la viwanda wawekezaji wale waweze kufika kwa urahisi na wawe na moyo wa kuwekeza kwa nguvu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu kila muwekezaji anachagua eneo la kuwekeza akitarajia miundombinu itakuwa rafiki kwake na kumrahisishia uzalishaji wa maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile pale katika lile eneo ninalozungumza la Kongani ya Viwanda Kwala linaloenda sambamba na eneo la Bandari Kavu Kwala. Kutoka Kwala kuja kwenye station ya Ruvu ambapo hapo ndiyo kuna station inaitwa station ya kupakia mizigo ya mwendokasi kuna urefu kama wa kilometa tatu, nne hivi lakini barabara ya kukatisha kutoka hapo Kongani ya Viwanda kuja kwenye hiyo station hakuna utaratibu wa kuishughulikia. Ni vizuri Serikali ikaenda kufanya miundombinu kwenye eneo lile ili tuweze kuona ni namna gani tunaunganisha kati ya Kongani ya Viwanda na station ambayo inatakiwa kupakia mizigo pale kutengenezwe utaratibu wa kuweka daraja katika Mto Ruvu na kutengeneza ile barabara kwa lami ili mizigo iweze kusafirishwa kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tumesikia kwenye Hotuba ya mwaka huu kwenye mipango ya mwaka huu. Tunakwenda kuongeza shilingi 100 katika kila lita ya mafuta kwa mtumiaji wa Tanzania ambaye ataingia kwenye sheli yoyote Tanzania. Hili ni jambo jema kwa sababu tunaenda kuongeza pato kwa ajili ya miradi. Kuna jambo nilikuwa nataka tuliweke wazi na Mheshimiwa Waziri ikiwezekana atusaidie Wabunge na anapotusaidia Wabunge naye anakuwa amesaidia Watanzania wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana tulipokuwa na tozo, tozo ilielekezwa ilisema itakwenda kwenye ujenzi wa vituo vya afya, itakwenda kuwenye masuala mazima ya barabara. Kwa hiyo, kila Mbunge alikuwa tayari anasikiliza atapata kiwango gani kwa ajili ya miradi hiyo. Leo hapa Mheshimiwa Waziri amewasilisha tunasema tunapongeza tunaomba tu atakapokuja atuambie ni miradi ya namna gani inayokwenda kutengenezewa mazingira hii ya shilingi 100 ili tukienda Majimboni tutakapokuwa tunawahamasisha wananchi juu ya tozo hii iliyoongezwa watu wawe na matumaini sasa kumbe barabara inakuja kutengenezwa, kumbe zahanati inakuja kutengenezwa, kumbe kituo cha afya kinakuja kutengenezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiiweka katika lugha ya kwamba tumeongeza shilingi 100 kwenye mafuta kila lita ya mafuta ambayo itakwenda kwenye miradi ya kimkakati uhamasishaji wa kwenye jamii waione lakini kama walivyoiona tozo ya mwaka jana unaweza ukawa mgumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ombi langu kwa Mheshimiwa Waziri najua ni jambo ambalo analiweza na ninajua nia yake njema aje atuambie Wabunge kwa sababu tukitoka hapa tunakwenda kuyavamia Majimbo na kwenda kuwafahamisha wananchi nini Serikali imejipanga kwa ajili ya maendeleo ya nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naamini kabisa itakuwa ni nafasi nzuri ya kuwaambia hii shilingi 100 mliyoisikia kwenye lita moja ya mafuta tunaitarajia baada ya kukusanywa Jimbo la Kibaha Vijijini, Jimbo la Makete, Jimbo la Iramba na kwingine kwingine kokote Tanzania inakwenda kutekeleza kilometa kadhaa za lami, hii inakuwa ni sehemu ya faraja kwao na utaona watakavyoilipa pasipo tatizo kwa sababu ni watu wote wanatarajia kuhakikisha kwamba huwezi kuendesha maendeleo katika eneo lolote kama watu wa maeneo hayo hawajachangia chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ombi langu Mheshimiwa Waziri ukija fungua ule mtego uliouweka wa kusema ni miradi ya kimkakati. Nenda kaweke wazi kwamba ni miradi gani inakwenda kukusanyiwa hii shilingi 100 ili twende tukaiseme vizuri kwa Watanzania walio huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo langu la mwisho kwa leo nataka kuchangia ni jambo zima la ukamilishaji wa utekelezaji wa miradi. Sote hapa tumesimama tumempongeza Mheshimiwa Rais, tumepongeza Serikali kwa namna ya miradi ilivyotekelezwa kwenye maeneo yetu lakini kuna changamoto kwenye maeneo mbalimbali ambayo miradi hii imeshindwa kumalizwa kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo kwamba hili jambo halijulikani. Kamati zote zinazofanya upitiaji wa miradi ikiwemo LAAC ambayo mimi ni Mjumbe wake tunatoka na Taarifa ya CAG inatoka inaonesha ni kwa namna gani miradi inakwama kwenye utekelezaji lakini kwa nini jambo hili linaendelea? Linaendelea kusema ukweli kasi yetu ya kuwachukulia hatua waharibifu wa fedha za miradi ni ndogo sana na inapokuwa ndogo sasa inajenga uzoefu. Mtu aliyezoea kupiga akiona wa jirani yake kapona halafu baya zaidi hawa wapigaji wana silka ya kuchekana. Anamcheka mwenzie kiko wapi umekaa ofisini huna unachofanya. Sasa ni vizuri tukachukua hatua kwa wanaoharibu miradi ili watu waogope na miradi hii ikamilike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kwenye Kamati yetu ya LAAC tuna tatizo chungu mzima tumepitia taarifa yetu na Mwenyekiti wetu Mheshimiwa Halima Mdee pale. Kuna mambo mbalimbali yameelezwa na CAG kwetu lakini ukiangalia hatua ambazo tunazipendekeza Kamati na hatua ambazo zinachukuliwa hatua ni vitu viwili havifanani kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa hali hii sisi tunaofanya kazi ya kutoa mapendekezo ya hatua za kuchukua tunaonekana kama tunatoa mapendekezo kwa sababu tuna jazba na tunayoyatolea mapendekezo. Ni vizuri Serikali ikachukua hatua kwa maana ya kuleta discipline ya kusimamia utekelezaji wa miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye halmashauri…

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naunga mkono hoja. (Makofi)