Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie katika bajeti hii kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wetu kwa kazi kubwa anayoifanya na bajeti hii ni mfano mmoja wa muendelezo wa kazi zake za kuboresha maisha ya Watanzania. Nampongeza sana na kumshukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Mwigulu na wenzake wote kwenye Wizara kwa kutuletea bajeti hii ambayo ni ya viwango. Mwaka jana kwenye bajeti kama hii, Bajeti Kuu ya Serikali nilipata fursa ya kuchangia na nikazungumzia jambo nililoliita makambi ya kilimo ya vijana. Nikasema kwamba ningetamani kabisa kama vijana wangewezeshwa waanze kilimo cha makambi, kilimo kikubwa, wapewe nyenzo, wapewe matrekta, wapewe power tiller, wapewe pembejeo kama mbolea na mbegu, madawa na nini. Makambi yajengwe kwa majengo ya muda halafu kilimo kiwe kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nashukuru sana kwamba mpango huu umeanza Mheshimiwa Bashe nampongeza sana unaitwa BBT. Wameupa jina jingine BBT (Building a Better Tomorrow), napongeza sana kwa sababu mpango huu utaenda kuondoa shida ya ajira kwa vijana na kuongeza uchumi kwa sababu wanazalisha mazao mengi watauza ndani na nje ya nchi watapata pesa na kupata utajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hofu yangu ni moja kwamba mpango ulivyokwenda umekuwa mno wa kutumia fedha, kingereza wansema capital intensive. Hii sina hakika kama itatusaidia, bahati mbaya tuna watu wengi ambao ni wezi. Wanakaa wameangalia pesa ilipo wadokoe. Sasa ndiyo maana mimi nikapendekeza kwamba, tungefanya utaratibu ule wa labor intensive, vijana wanapelekwa makambini, wanajengewa makambi yale wanapewa hata chakula, mahindi, unga maharage ya kuanzia wanapewa usimamizi, matrekta yale wanazalisha. Pesa kidogo sana lakini zaidi vifaa vile pembejeo na vifaa vingine ili watu wasipate mwanya wa kuiba hizi fedha, kazi ifanyike na matunda yapatikane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa mtindo uliopo vijana wanakaa kwenye vyuo pale kwangu Bukoba pale Maruku Chuo cha Kilimo, kuna vijana sijui wangapi wametoka sehemu mbalimbali za nchi. Semina ya miezi sijui mingapi, mimi naona ile haina tija. Tija ingekuwa ni kutafuta maeneo mazuri mashamba ambayo tunayo mengi nchi nzima imejaa maeneo yenye rutuba na mvua na mito ipo, kilimo hiki kikasonga mbele kwa sababu kwa kweli kikifanikiwa hiki tutapata tija kubwa sana. Kwa hiyo, tuwe macho sana na matumizi ya fedha kwenye mradi huu au mpango huu badala yake tutumie ile ambayo nilipendekeza, kwamba iwe ni kutumia vijana na nguvu zao na vifaa wapewe badala ya kuwapa fedha ambazo zitatuletea matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuwe macho sana na matumizi ya fedha kwenye mradi huu au mpango huu, badala yake tutumie ile ambayo nilipendekeza kwamba, iwe ni kutumia vijana na nguvu zao na vifaa wapewe badala ya kuwapa fedha ambazo zitatuletea matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza, hata kwenye Wizara ya Elimu tumeletewa mpango mpya hapa ambao baadaye kidogo, wanasema mwakani ikiwezekana itaanza utaratibu wa masomo ya sekondari ambapo kutakuwa na njia mbili. Kwanza ni masomo ya kawaida, mwanafunzi atasoma mpaka Form Four, lakini upande mwingine akipenda mwanafunzi anasoma masomo ya amali; ufundi, kilimo, ufugaji, na masomo mbalimbali. Hii nayo ni njia mojawapo ya kupunguza tatizo la ajira kwa vijana wetu ambao wanamaliza shule, japo itachukua muda mrefu. Kwa hiyo, ule mpango wa kwanza wa BBT ukiboreshwa utakuwa ndiyo njia ya kukomboa tatizo hili kubwa la kukosa ajira kwa vijana wetu na kuongeza uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipendekeza hata Wizara ya Biashara na Viwanda iwe na idara maalum pale Wizarani ya kutafuta masoko kwa mazao ya vijana hawa. Nilisema mazao ya muda kwanza ndiyo waanzenayo. Wakilima mazao kama mahindi, maharage, mtama, alizeti, ambayo yanavunwa haraka sana; miezi mitatu, miezi minne, lakini kuwe na kitengo maalum kwenye Wizara ya Biashara ambacho kitashughulika na kutafuta masoko ya ndani na nje ya nchi kwa ajili ya hawa vijana kwa mazao yao. Ziko nchi nyingi ambazo hawalimi kama kule Uarabuni, Afrika ya Kati hapa, Darfur, Sudani na wapi. Kwa hiyo, mazao haya kile kitengo kisaidie kutafuta masoko ya vina hawa na kuwapelekea mazao na kupata biashara nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kwenye Jimbo langu pale Bukoba Vijijini. Nimesema mara kadhaa kuna maeneo ambayo bado yana tatizo la maji. Kwa hiyo, naomba kwenye bajeti hizi haya maeneo yaangaliwe kwa jicho la huruma. Yako maeneo mengi ambayo yana shida kubwa sana ya maji, maeneo kama Umbweya pale kwangu, Kagarama, Vijiji vya Rugaze, Amani, Nsheshe na maeneo mengine kama Kanyangeleko na wapi, maji hayajafika. Kwa hiyo, bajeti ziongezwe kusudi maeneo haya nayo wapate majisafi, salama na ya kutosha kusudi shida ya wananchi katika maeneo haya ipungue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Bukoba kumekuwa na tatizo la muda mrefu la umeme kuzimika mara kwa mara. Kwanza napongeza umeme unasonga kwenye vijiji na vitongoji, kila siku kuna hatua inapigwa, lakini pamoja na hatua hiyo, umeme huu hauaminiki, unazimika sana. Ukizimika, sasa tija yake haionekani, na vifaa vinaharibika; kama ni taa, zinaungua, kama una fridge au nini, vinaungua mara kwa mara na wananchi wanapata shida kubwa sana. Ni hasara kubwa. Kwa hiyo, kazi kubwa inatakiwa ifanyike pale, bajeti iongezwe, kutafutwe njia ya kuondoa tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kazi inafanyika, lakini kasi iongezeke. Njia sahihi ni kuweka ile gridi badala ya kutumia umeme wa Uganda, tutumie umeme wa Tanzania. Gridi isogezwe ifike mpaka Kagera na Bukoba yote ipate umeme huu wa gridi kusudi tatizo hili la umeme kuzimikazimika liwe ni historia, liishe na wananchi wafaidi umeme huu na hili tatizo la vyombo vyao kuungua liishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie na jambo moja la mwisho ambalo hivi karibuni Serikali imeruhusu tena mabasi ya abiria kusafiri usiku kucha. Mwaka 1987 nilikuwa nakaa Dodoma hapa nafanya kazi Wizara ya Serikali za Mitaa, lakini familia yangu ilikuwa inaishi Dar es Salaam. Kwa hiyo, nilikuwa nasafiri sana Dar es Salaam – Dodoma. Nilichokiona barabarani ni kitu kibaya sana. Usafiri wa usiku siyo mzuri. Hatujaweza kudhibiti madereva wetu kuwa na nidhamu ya kulala mchana wasafiri usiku. Mchana wanafanya kazi nyingine ya kubangaiza, usiku anaendesha gari. Ajali zilikuwa ni nyingi sana. Watu wanakufa, mabasi yanawachinja barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Malecela akiwa Waziri Mkuu, ndiye aliyefuta mabasi kusafiri usiku mwaka 1994. Sasa leo tumerudisha, sifahamu tumejiandaaje na jambo hili. Tutapata tatizo la kupata ajali nyingi sana barabarani usiku, watu watakufa sana. Tujiangalie kama hatujafikia uwezo wa kuyadhibiti magari haya, tusifanye hivyo. Tuendelee kusafiri mchana na tuache kusafiri usiku. Kama tunaweza, basi tuendeleenalo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)