Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa. Niipongeze sana Wizara ya Fedha, Waziri wa Fedha na timu yake yote kwa namna ambavyo wametuletea taarifa muhimu kutuwezesha kujadili hotuba hii, lakini pia Kamati yako, Kamati ya Bajeti ambayo pia imetupa taarifa muhimu sana na ofisi zingine wezeshi kama NBS pamoja na CAG. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya vizuri tunaisoma taarifa na hatua mbalimbali ya utekelezaji wa miradi yetu tumetekeleza vizuri. Tunaona sasa hivi tunaanza na LNG ambao tuko kwenye hatua nzuri, lakini utekelezaji wa Mradi wa Bomba la Mafuta ambao tayari mchango wetu tumeshalipa bilioni 354, nusu ya fedha zinazotakiwa, lakini pia Mradi wa SGR tuko vizuri na Mradi wa Mwalimu Nyerere tunaendelea vizuri, sasa tuko asilimia 87. Kwa hiyo, ni mambo ambayo ni mazuri na tumepiga hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa labda nianzie mambo ya masuala ya kiujumla. Kwanza, naunga mkono sana pendekezo la Kamati yako ya kuhakikisha kwamba Finance Bill inaletwa na kujadiliwa angalau katika kipindi cha mwezi mzima, kuacha ilivyo sasa leo umewekwa mezani ambayo ni siku saba tu itakuja kuamuliwa hapa Bungeni. Kwa hiyo, naunga mkono kabisa kwamba tupate mwezi mzima wa kujadili taarifa ya Finance Bill. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili katika mambo ya kiujumla, nashauri lile bango kitita waliloshauriana lenye hoja kumi na saba zilizoibuliwa zingine ndani ya Bunge, lakini zingine kwenye Kamati, wangeleta hapa jedwali lile kuona Serikali imejibu nini na wa wamesema nini, badala ya kusema huko huko tu Kamati ya Bajeti walielewana sasa walielewana nini? Sisi tutajua nini hapa Bungeni?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, katika yale maeneo ya kiujumla ni katika hotuba ya Waziri, katika hotuba ya Waziri wa Fedha, ibara nadhani ya 9, anapozungumzia Ibara ya 9 Mheshimiwa Waziri wa Fedha anazungumzia mwaka 2008 ambako Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan hakuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, ukiweka ibara ya namna hiyo kwa maelezo waliyoyaweka pale inakuwa ni kama matumizi mabaya ya jina la Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la nne, katika haya mambo ya kiujumla ni pale ambapo katika Ibara ya 126 ambako Waziri anasema kupiga marufuku ufungaji wa biashara kwa sababu zozote zile. Ukiweka Ibara ya namna hiyo, unaweza kuleta mkanganyiko mkubwa, moja; kwanza mambo haya ni ya kisheria, yanafanyika kisheria, lakini la pili, kuna mambo ambayo yanalazimika biashara ifungwe. Kwa mfano, unakuta kiwanda au unakuta mgodi unatiririsha sumu kwenye makazi ya watu, unatiririsha sumu kwenye vyanzo vya maji, hizi Mamlaka za Usimamizi zifanye nini? NEMC wafanye nini katika mazingira ya namna hiyo kama siyo kufunga ili kuhakikisha kwamba wana–rescue maisha ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine unaweza kukuta mtu anafanya biashara hana leseni, hana kibali chochote, anauza bidhaa bandia, anauza bidhaa fake, unamfanya nini? Kwa hiyo, tukiweka vifungu kama hivyo vinaleta mkanganyiko kwa wasimamizi wa sheria ambao tumetunga sheria sisi wenyewe na kuwaagiza katika maeneo hayo wafanye nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ibara za namna hiyo aidha ziondolewe au Waziri azitolee ufafanuzi na mamlaka hizi zinazohusika na hizi kazi tujue kwamba zinafanya pia kazi nzuri sana ya ulinzi wa biashara. Kwa hiyo tusizikatishe tamaa kwa kuweka mistari mikubwa hivi kwenye hotuba ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda siwezi kuendelea kuzi–mention, lakini nadhani zinafanya kazi nzuri na zinahitaji kupongezwa, lakini pale ambapo mtumishi anaonekana ame–violate sheria za nchi ashughulikiwe na natamani watu wa namna hiyo atuambie kuwa amewachukulia hatua wangapi, lakini siyo kuzituhumu hizi taasisi za usimamizi na udhibiti ambazo zinafanya kazi nzuri sana hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la tatu ni ukusanyaji wa mapato. Nataka nizungumzie suala la ukusanyaji wa mapato na namna ambavyo hatujakusanya zaidi ya trilioni 15, kwa sababu ya usimamizi mbovu wa ukusanyaji wa mapato hapa nchini. Moja, imeripotiwa hapa kufikia Aprili, 2023 hatujakusanya fedha ambazo ziko kwenye malimbikizo ambazo zimeshikiliwa za kikodi zaidi ya trilioni 7.35. Trilioni 7.35 hatujazikusanya. Kesi hizo ziko kwenye mahakama hizi za rufaa za kodi TRAB na TRAT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unajiuliza mwaka mzima umeisha tumeshindwaje kuzikusanya fedha hizi? TRAB na TRAT hizi mamlaka zetu zina changamoto gani kiasi cha kushindwa kukusanya hizi fedha na ukiangalia uwezo wa TRA kushinda kesi katika haya mashauri ni asilimia 81, ina maana kwamba kwenye malimbikizo ya trilioni 7.35 tuna uwezo wa kukusnaya trilioni sita. Kwa hiyo, katika kipindi hiki tunaweza kukusanya trilioni sita kupitia hiki chanzo. Lakini tatizo ni nini tunashinda kuyakusanya hapa mapato? Nini kinachotukwaza kufanya hivyo? Tunaingia kwenye mikopo, tunaingia kwenda kuwa-harass wananchi wetu kuwawekea kodi ambazo hazina sababu za msingi, mapato yapo hayakusanywi kwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili hapa kwenye suala la ukusanyaji wa mapato ni utakatishaji wa fedha haramu, ufadhili wa ugaidi na ufadhili wa silaha za maangamizi. Taarifa ya FIU inaonesha miamala ya fedha taslimu na fedha zilizopitia katika miamala, zaidi ya trilioni 280 kuishia Aprili, 2023. Hivi utawezaje kukusanya kodi katika nchi ambayo ina miamala ya fedha haramu trilioni 280, halafu hauoni mikakati ya kushughulika na hizi fedha, hauoni mikakati iliyowekwa ya FIU kushughulika na hizi kesi na katika kipindi hicho kesi zilizosikilizwa au miamala iliyochambuliwa na FIU ni miamala 769 tu, kati ya miamala 16,035 iliyochambuliwa ni 769 peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo huoni mkakati wowote huwezi ukakusanya fedha, kodi katika eneo hili kwa sababu ukikuta miamala mingi namna hiyo maana yake ni kuna ukwepaji wa kodi uliopitiliza, maana yake kuna a list financial flow iliyopitiliza, maana yake kuna utoroshaji wa fedha nyingi nje ya nchi uliopitiliza, kuna transfer pricing illegal zinazofanyika zilizopitiliza. Utakusanyaje kodi katika mazingira haya? FIU ni kitengo tu mpaka leo, hakuna mechanism huioni, DCI anashughulikaje? PCCB anashughulikaje? DPP anashughulikaje kuhakikisha kwamba hii miamala tunapata fedha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili eneo tu ni fedha nyingi sana zilizopotea, lakini bado Tanzania iko kwenye financial action tax force na nini na mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni magendo, magendo katika mipaka na katika maeneo ya bandari. Tunazo bandari bubu 693. Tunashindwaje kuwa-engage vijana wetu wa JKT tukaweka fence kila mahala tukaweza kukusanya fedha nyingi tu katika hili eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wangu una changamoto nyingi na mambo ni mengi niende kwenye mikopo, matumizi ya mikopo ya ECF na LTP. Kamati imetueleza bayana kwamba matumizi haya ya hizi fedha ni mikopo imeingiwa na Serikali. Serikali zaidi ya mikopo hii iliyoko kwenye hili eneo la ECF na LTP ni trilioni 2.75 na Kamati ya Bajeti inatueleza dhahiri kwamba hapa fedha hizi hazikwenda kwenye matumizi yenye tija, zaidi ya trilioni 2.75. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukiambiwa hapa tunakopa fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo, inaenda kwenye miradi ya maendeleo. Leo Kamati yako ya Bajeti ina-prove kwamba fedha nyingi hizi zimekopwa, trilioni mbili zitakopwa na kuelekezwa kwenye maeneo ya matumizi ambayo hayana tija, trilioni 2.75. Fedha hizi tumekuwa tukikopa tunasema tunapeleka kwenye miradi ya maendeleo. Leo deni letu la Taifa limekuwa kwa asilimia 13.9 it is almost asilimia 14.9 kutoka mwaka mmoja kwenda mwaka mwingine. Ni mikopo ambayo hatujawahi kukopa kwa kiwango hicho, lakini tumekuwa tukiambiwa fedha zinaenda kwenye miradi ya kimkakati, lakini tumekuwa tukiambiwa kwamba fedha hizo tumekopa kwa sababu tuna miradi mingi ya maendeleo na mpaka sasa hivi tuna hiyo hoja ya Mkaguzi kwamba zaidi ya trilioni 1.285 zimekopwa nje ya kibali cha Bunge hili lilivyoidhinisha kukopa katika mwaka husika wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mikopo kama hii ikiendelea kuruhusiwa, Bunge hili likiendelea kuruhusu mambo kama haya yafanyike na mikopo hii ya ECF pamoja na LTP ambayo hata Bunge hili liliagiza ikajadiliwe kule na nimeona majadiliano mliyoyafanya inaonekana mmeshindana. Liletwe jedwali zima la fedha hizi trilioni 2.75 zinaenda kwenye maeneo gani na Waziri wa Fedha amepata wapi kibali cha kwenda kuidhinisha mikopo ya matumizi ya kawaida wakati msimamo wa nchi fedha zote zinakopwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Waziri wa Fedha yeye amepata wapi mamlaka ya kuruhusu fedha ya kwenda ku–negotiate mkopo ambao unaenda kwenye matumizi ya kawaida badala ya matumizi ya maendeleo? Lakini fedha nyingine nazungumza EPC+F. Hii EPC+F ni mfadhili anakuja na hela, anaajiri Wakandarasi yeye, anasimamia mradi yeye, anafanya design yeye, ananunua yeye. Mbona hatupewi maelezo ya kina Taifa linapata faida gani? Tutasimamiaje gharama? Tutasimamiaje ubora kwa Wakandarasi ambao hatuwalipi sisi? Lakini pia mikopo hii ni ndani ya mikopo yetu ile tunayokopa hapa nchini au ni mikopo mingine? (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Luhaga, muda wako umeisha.