Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi ili niweze kuchangia bajeti ya mwaka 2023/2024. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uimara wake katika kukuza uchumi wa nchi yetu kwa kuendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo inaendelea kwenye nchi yetu, lakini pia kuanzisha miradi mingine kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze kwa ajili ya kuendelea kuhakikisha nchi yetu inakuwa salama na nchi yetu inaendelea kutawaliwa huku akijali sana utawala bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa kututayarishia Bajeti hii ambayo kusema ukweli kama itakwenda kutekelezwa kama ambavyo imesomwa hapa baada ya marekebisho ya Waheshimiwa Wabunge nadhani itakuwa ni Bajeti tulivu na Bajeti ambayo ninaamini itapeleka nchi yetu mbele kwa mwaka ujao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze pia Waheshimiwa Mawaziri wote chini ya Kiongozi na Jemedari wao Mkuu Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutekeleza majukumu yao ya msingi kuhakikisha nchi yetu na Watanzania kwa ujumla wanapata maendeleo kwa kusapotiwa na Serikali yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia suala moja tu siku ya leo na jambo lenyewe ninalotaka kuzungumzia ni bei za mazao hasa mazao ya kilimo. Nataka kuzungumzia jambo hili kwa sababu mazao yetu ya kilimo ni muhimu sana kwa nchi yetu, ni muhimu sana kwa wananchi, ni muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Bashe kwa ubunifu wake na namna ambavyo anaendelea kutekeleza shughuli zinazohusiana na mambo ya kilimo kweye sekta yake. Serikali imefanikiwa kutoa ruzuku kwa mbolea, tunaipongeza sana lakini Serikali imefanikiwa kutoa viuatilifu kwa ajili ya wakulima wanaohitaji viuatilifu hivyo maeneo mbalimbali. Sisi kwa upande wetu tumepata viuatilifu kwa ajili ya zao la pamba na tumepewa bure, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais lakini tunampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuongeza Bajeti ya Kilimo mwaka uliopita na hata mwaka ambao tunajadili Bajeti yake. Mwaka uliopita bajeti ilikuwa shilingi bilioni 920 hivi, mwaka huu ni shilingi bilioni 970. Tunaamini kama fedha hizi zitatolewa na Serikali zikaenda kutekeleza miradi ya maendeleo inayohusiana na kilimo tunaamini tutapiga hatua na pengine tutafikia lengo la kukuza uchumi kwa 5% badala ya 3% ambayo tumefikia sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la kufanya haya ni nini? Lengo la kufanya haya ni kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo na mimi naamini kwa hatua hizi ambazo zinachukuliwa na Serikali uwezekano mkubwa kabisa wa kuongeza uzalishaji wa mazao ya kilimo upo. Inawezekana kabisa tukaongeza kwa sehemu kubwa sana. Sasa mazao yetu haya ya kilimo ni muhimu sana kwa mambo mbalimbali. Moja; yanaendelea kuajiri Watanzania. Pili; yanaendelea kutupatia kipato kama Watanzania, asilimia kama 65 tunapata maisha yetu kutoka kwenye mazao ya kilimo, kutoka kwenye kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazao haya ya kilimo pia ni muhimu kwa sababu haya ndiyo yanayotuletea fedha za kigeni hapa nchini kwetu. Tulikuwa na nakisi ya Serikali juu ya uagizaji na uuzaji wa mazao yetu nje kiasi cha dola milioni 5,000 hivi lakini mazao ya kilimo yametusaidia sana kutuletea fedha za kigeni ili kupunguza nakisi yetu kati ya biashara na nchi zingine. Hii inatusababisha tuwe na mfumuko wa bei kidogo pia tuwe na fedha za kigeni zinazotosheleza kununua mahitaji yetu mbalimbali tunayoyahitaji kutoka kwa wenzetu nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano mwaka wa 2021 korosho imetuletea dola milioni 226.9, ongezeko kutoka dola 159 mwaka 2021. Katani mwaka 2021 imetuletea 127, mwaka wa 2022 imetuletea 178.5, pamba imetuletea dola 103.4 mwaka wa 2022 ongezeko kutoka dola milioni 81.3. Kwa hiyo, mazao haya yana umuhimu mkubwa sana kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunapokuja kwenye bei wanazolipwa wakulima wetu hapa ndani ya nchi kusema ukweli bado kwenye eneo hili hatujafanya vizuri. Malipo wanayopata wakulima wetu ni malipo kidogo ukilinganisha na nguvu wanayoiweka kwenye hicho kilimo, ukilinganisha na gharama wanayoiweka kwenye hicho kilimo, ukilinganisha na muda wanaotumia ili kuvuna hayo mazao na hii wakati mwingine inaweza kuwa ni kwa sababu zilizo nje ya uwezo wa Serikali au nje ya uwezo wa mkulima wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la bei linatatulika, mwaka 2020/2021 bei ya korosho kwa mfano, korosho mkulima aliuza kati ya shilingi 3,400 mpaka 3,600 mwaka 2020/2021 lakini 2021/2022 mkulima ameuza korosho yake bei ya shilingi 1,400 mpaka shilingi 1,800 anguko kubwa sana hili karibu linakaribia nusu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkulima wa pamba 2021/2022 bei aliyouzia pamba yake ni shilingi kati ya 1,560 mpaka 2,200 bei ilikuwa nzuri lakini msimu huu 2022/2023 bei ya pamba ni shilingi 1,060 na hatujui kama itakwenda kupanda, anguko la nusu zaidi ya nusu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii inakatisha tamaa wakulima wetu, inakatisha tamaa wasilime tena msimu ujao lakini pia inafanya wawe na kipato kidogo na inawafanya waendelee kuwa wanyonge kwenye nchi ingawa mchango wao, mchango wa mazao wanayozalisha ni mkubwa na unaisaidia na kuifaidisha nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naomba Serikali iingilie kati kwenye bei za mazao haya kwa kuanzisha price stabilization fund. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naona umewasha kinanii chako, naomba nimalizie tu nusu dakika. Ianzishe price stabilization fund ili kuwasaidia wakulima hawa bei za mazao yao zinapoanguka na hili siyo wazo geni ni wazo linalofanywa na nchi zilizoendelea na maeneo mengine. Kwa hiyo, sisi hapa tunaweza kufanya hivyo pia tena kwa kuwachaji wakulima wakati bei za mazao haya zinapokuwa ziko juu lakini pia Serikali inaweza ikaweka ruzuku ili kufidia bei zinapoanguka. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana.

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)