Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

Hon. Hawa Abdulrahiman Ghasia

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa Mwaka wa Fedha wa 2016/2017.

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nichukue fursa hii kukushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika hoja iliyopo mbele yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenijalia afya na uzima na kuweza kupata nguvu ya kuweza kuwawakilisha wananchi wangu wa Jimbo Mtwara Vijijini na Mkoa wa Mtwara kwa ujumla na Watanzania.
Napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayoifanya kwa sababu Wizara hii ni zaidi ya Wizara tatu kama tulivyozoea kuziona, lakini nina imani kabisa kwamba ataweza kuzimudu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri, kile kitendawili chetu cha wananchi wa mkoa wa Mtwara kuhusu barabara yetu ya uchumi angalau mwaka huu tunaziona kilometa 50 zikiwa zimetengewa pesa. Ametuhakikishia kwamba kilometa hizo 50 kutoka Mtwara mpaka Mnivata ujenzi utaanza katika mwaka wa fedha 2016/2017. Mheshimiwa Waziri tunakushukuru sana kwa hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, isipokuwa ningependa tu kusisitiza, Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli wakati anaomba kura alituahidi akishinda zile kilometa 159 zinazobaki kutoka Mtwara - Newala - Masasi watagaiwa wakandarasi kilometa zote ili ujenzi uweze kukamilika kwa wakati. Mheshimiwa Waziri nitapenda wakati unatoa ufafanuzi utuelezee utaratibu uliopo kwa zile kilometa ambazo zimebaki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo napenda pia nilizungumzie ni kuunganisha barabara zetu za mkoa na mkoa lakini pia kuunganisha nchi na nchi. Mheshimiwa Waziri tunazo barabra zetu zinazotuunganisha Mtwara na majirani zetu wa Msumbiji, kutoka Mtwara - Kilambo na kutoka Mtwara - Msimbati kimekuwa kilio cha muda mrefu, tumekuwa tukiomba zijengwe kwa kiwango cha lami kama ambavyo mipaka mingine yote inaungwanishwa. Kwa hiyo, nitataka kusikia ni lini mkoa wa Mtwara utaunganishwa na Msumbiji kupitia kivuko cha Kilambo na Msimbati kwa kujengwa kwa kiwango cha lami hasa ukizingatia kwamba Msimbati ndiko ambako gesi inatoka na tuna vitega uchumi vyetu vingi kule vya thamani ambavyo kwa kweli lazima tujenge barabara ya uhakika ambapo tutaweza tukaenda wakati wowote bila kujali mvua au jua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda kulizungumzia ni bandari. Katika bajeti ya mwaka 2015/2016 tuliambiwa kwamba majadiliano na wawekezaji upande wa Mtwara yamekamilika kwa ajili ya kujenga gati nne katika bandari ya Mtwara, leo Mheshimiwa Waziri anatuambia kwamba majadiliano yale ambayo tuliambiwa yamekamilika hayakufanikiwa na badala yake inataka kujengwa gati moja yenye mita 350, hatukatai sawa lakini lengo lilikuwa ni gati nne.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na utafiti wa gesi unaoendelea kule; zao letu la korosho na viwanda vingi ambavyo vinakwenda kule ikiwemo vya mbolea na hivyo vya kina Dangote kwa bandari iliyopo sasa hivi haitoshelezi na wakati mwingine inaleta usumbufu mkubwa sana hasa katika kusafirisha zao letu la korosho. Kwa hiyo, napenda Mheshimiwa Waziri atuambie gati zingine tatu zilizobaki mpango ukoje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo tunalo eneo la Kisiwa na Mgau ambapo eneo lingine tumempa Mheshimiwa Aliko Dangote ili ajenge bandari kwa ajili ya kusafirishia saruji na eneo lingine bandari yenyewe iliamua kuchukua kwa ajili ya kujenga bandari yake. Tathmini imeshafanyika, sasa hivi imebaki ni hadithi kesho, kesho kutwa. Amekuja Mheshimiwa Waziri Mkuu kule tuliambiwa baada ya siku tano fidia awamu ya pili italipwa. Lile eneo ambalo Dangote amepewa fidia ilishalipwa imekamilika, eneo ambalo bandari wamechukua kwa nini hamlipi? Dangote ameshalipa, wananchi wameshatumia pesa zao lakini wale ambao wanapaswa kulipwa na Mamlaka ya Bandari imebaki danadana. Sasa mnawagombanisha, kwa nini upande wa Dangote walipwe na upande wa bandari hamtaki kuwalipa?
Kwa hiyo, ningependa Mheshimiwa Waziri aje aseme ni lini watalipwa kwa sababu kila siku maelezo ni kwamba wanasubiri Bodi ya Bandari iundwe ili iweze kuridhia zile pesa kwa sababu pesa za kulipa fidia zipo shilingi bilioni 13, hiyo Bodi ya Bandari inaundwa lini ili mambo yaende? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda kulichangia ni kuhusu reli ya kutoka Mtwara - Songea - Mbamba Bay. Nimeona katika hotuba kwamba upembuzi yakinifu na usanifu umekamilika Februari 2016. Napenda kufahamu ujenzi wa reli hiyo ya kutoka Mtwara - Mbamba Bay na matawi yake ya kwenda Liganga na Mchuchuma utaanza lini? Kwa sababu uwekezaji unaofanyika kule Liganga na Mchuchuma, makaa ya mawe yaliyoko Ngaka bila kuwa na reli mradi ule Mheshimiwa Waziri itakuwa ni hadithi. Naomba Mheshimiwa Waziri aje atuambie ujenzi wa reli kutoka Mtwara - Mbamba Bay na matawi yake yanayokwenda Liganga na Mchuchuma utakamilika lini kwa Mtwara huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni ukarabati wa uwanja wa ndege wa Mtwara. Iliwekwa katika bajeti lakini mpaka sasa hivi hakuna fedha iliyotoka hata kidogo. Pia tuliambiwa uwanja ule utawekewa taa, mpaka sasa hivi taa hakuna. Tunachofanya pale ni kuazima taa za muda za wenzetu wa BG, hivi siku BG wakitukakatalia tunafanya nini? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutonana na utafiti na uchimbaji wa gesi na mambo yanayoendelea kule Mtwara, kwa kweli ni lazima ule uwanja upate taa na ukarabatiwe. Uwanja ule ulijengwa mwaka 1965, hata mimi sijazaliwa na nimeshafikia mahali ambapo kama ni umri naweza nikasema zaidi ya nusu labda au nusu nimeshamaliza uwanja ule haujakarabatiwa. Tunaomba Mheshimiwa Waziri anapokuja aje atuambie uwanja unakarabatiwa lini na unawekewa taa lini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho, tunayo makampuni ya mitandao ya simu na kila mara wamekuwa wakidai kwamba wanalipa kodi ya huduma (service levy) katika Halmashauri, lakini Halmashauri zetu nyingi hazipati ushuru huu na badala yake unalipwa katika Halmashauri chache. Niiombe Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia taasisi zake ikusanye ushuru huu makao makuu na ugawanywe katika Halmashauri zote bila kujali ukubwa wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.