Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Niungane na Wabunge wenzangu wote kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa rehema zake, baraka zake lakini kama Taifa kwa jinsi anavyotulinda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Rais kuna mambo mengi tunampongeza kwa ajili ya Serikali kutekeleza mambo mengi, ukiacha Wizara moja moja, kwa ujumla katika nchi yetu twendeni kila Mbunge kwenye Majimbo yetu tukaeleze yale mafanikio ya Serikali ili agenda hii ya kumpongeza Rais iwe agenda yenye mashiko na inayoonesha taswira nzuri kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kumpongeza kwa sehemu kidogo Mheshimiwa Waziri lakini pia nimweleze duku duku na maeneo ambayo ninadhani pengine kupitia ujumbe wangu huu yataboreshwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na eneo la Mbulu Mjini, Jimbo la Mbulu Mji ina mitaa 58, Kata sita za mji, vijiji 34 na Kata 10 ziko vijijini. Siyo kama tunavyozungumza Mbulu Mji kama Mji, Mbulu Mji una sura mbili, nianze na sura ya eneo la mji na kwa sababu hali hii ipo katika maeneo mengine hata kwa Majimbo yetu kwa Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Jimbo la Mbulu Mji wale wa pale katikati utakuta yuko ndani ya kilometa moja kutoka katikati ya mji lakini hajafungiwa umeme lakini amemaliza wiring na yuko ndani ya mita 30 ya nguzo. Hapa ushauri wangu ni kwamba niungane na mwenzangu Mheshimiwa Francis Isack alivyozungumza, twendeni tukafanye tathmini ya maeneo ya miji yetu na hali ya uhitaji wa umeme na wale waliofanya wiring, hapa tunatafutiana ajali za kisiasa kwa sababu moja kwa moja wananchi waliofanya wiring leo unapowaambia waunganishiwe umeme kwa shilingi 320,000 wakati shilingi 27,000 ingeunganisha wao wana matumizi makubwa lakini pia wako ndani ya mji kwa maana ya ndani ya kilometa moja ama mbili. Hali hii itaifanya matumizi makubwa ya umeme kupatikana lakini na uzalishaji kuja juu na kwa vyovyote wananchi wale watakuwa wamefunga umeme huu katika majumba yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tuelimishane au tuambizane na tutazame kwa sura tofauti kila Mbunge kwenye eno lake, kwa hali ya uchumi wa wananchi wetu ni mwanancni gani ana uwezo wa kulipa shilingi 320,000 akafanya wiring tena kwa shilingi 320,000 na mambo mengine, umeme wenyewe kwenye jengo hilo moja shilingi 700,000? Hii ni hali ambayo kwa vyovyote haiwezekani Mheshimiwa Waziri, utakapokuja pale toa kauli kama Serikali eneo hili la uunganishwaji wa umeme wa awali Serikali ije na njia mbadala ya kuunganisha umeme kwenye makazi ya watu kwa maeneo ya mjini na vijijini kwa sababu eneo hili la mji zamani wakati wanafanya wiring wananchi walitegemea sana kwamba eneo hili wanaunganishiwa umeme kwa shilingi 27,000 wao wanapata gharama ya kufanya wiring kwa maana ya kufanya uunganishaji wa waya kwenye majengo yao ili wapate huduma ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili la vijijini kwa Mbulu Mji utakuta kijiji cha mwisho kilometa 40, ndani ya kijiji hicho tunapopeleka kilometa mbili, kwenda kwenye vitongoji utakuta kitongoji kutoka katikati ya kijiji ni kilometa 20 ama 15 tena, kwa hiyo, nguzo za kwenda huko ni nyingi. Mimi ushauri wangu kwenye eno hili nilikuwa naangalia tunapoanza kuweka umeme kwenye maeneo ya vijijini tuangalie utaratibu ambao utashika kaya nyingi na nyumba nyingi ili ziingizwe kwenye mfumo huu wa kuunganisha umeme. Eneo hili la vijijini ndiko waliko wananchi wengi, matumizi yao siyo makubwa, wao sana sana watatumia umeme kwa taa, kuchaji simu na huduma zingine ndogo ndogo lakini mambo ya friji na mambo ya mitambo mingine haitakuwepo sana zaidi ya mashine za kusaga na vitu vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa nafikiri kama inawezekana eneo hili litazamwe na Wizara. Mheshimiwa Waziri timu yako imepita mara nyingi na mara nyingi umetuletea mipango hii ya vipaumbele kwenye vikao vyetu vya bajeti, kwa bahati nzuri baadhi ya maeneo mengi Serikali imejitahidi kuangalia ni namna gani umeme unakwenda. Kwa hiyo Jimbo langu la Mbulu Mji, vijiji vyote umeweka nguzo, vingine vina miezi miwili, vingine miezi mitatu, vingine sita umeme haujawaka. Hali ambayo nguzo zile zinazidi kuoza, mimi nilikuwa nafikiri uwekaji wa nguzo utegemeane na waya na vifaa vingine ambapo ukisimika nguzo hizo, walau umeme unawaka kwenye hicho kijiji ili unahamia kijiji kingine kuleta sura ya matumizi lakini na pia sura ya kutoa huduma kwa wananchi kwa wakati uliosahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeruka maeneo mengi ya taasisi za umma, migodi, pampu za maji, taasisi binafsi na mashirika ya umma, nadhani kuna haja ya kufanya tathmini upya ili hayo maeneo ya taasisi za umma yakiwemo makanisa na taasisi zingine na shule lakini pia na visima na maeneo mengine ya muhimu kama migodi tukaona namna ya uunganishwaji wa umeme. Mimi kule kuna wachimbaji wadogo wako mwaka wa 10 nadhani wanachimba lakini umeme haujafika mpaka leo, wakisubiri umeme waunganishiwe na kule kuna uzalishaji mkubwa.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hizi zingeachwa kwanza ili tuokoe muda.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Issaay taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kuchauka.

TAARIFA

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mchangiaji amesema kwamba kweli kunatakiwa umeme ufikishwe kwenye baadhi ya taasisi, kwa mfano kwenye nguzo na hii minara ya simu, minara ya simu mingi inaendeshwa kwa ma-generator kwa hiyo mimi nilifikiri kwamba ingetoka sera kabisa kwamba, pamoja na kwamba unapozungumzia taasisi tuzungumzie vilevile kwenye minara ya simu kote kufikiwe na umeme.

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Zacharia taarifa unaipokea.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea ni ufinyu wa muda tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia eneo hili la kukatia kwa umeme na migao ya umeme. Hili ni janga na hii ni ajali ya kisiasa pia. Wabunge Majimboni hatukai, umeme unakatika wananchi wanatulalamikia, umeme unakuwa wa mgao, wananchi wanatulalamikia, tuangalie mgao huu namna ambavyo tutaupunguza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Mbulu Mji linaongoza kwa mgao wa umeme na kukatika kwa umeme, nafikiri kama inawezekana sababu zitolewe mapema na wananchi wajiandae kwa sababu umeme ni uchumi, umeme ni huduma, umeme pia unaleta mafanikio kwa wananchi kufanya shughuli zao kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili litazamwe ili ukataji wa umeme na mgao upungue, tumekuwa na matatizo makubwa kwenye eneo hili hasa kwa mwaka huu tulionao pengine ni umeme ulikuwa mdogo kutokana na mabadiliko ya tabianchi lakini pia na hali ya maji kwenye mabwawa, tuangalie pia utaratibu wa kuzalisha umeme kwa njia ya upepo. Eneo hili la Kanda ya Kati tunao uwezo wa kuzalisha umeme wa upepo. Tafiti zilishafanyika, Serikali iangalie utaratibu sasa wa kuzalisha huo umeme ili uweze kunufaisha wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuangalie utaratibu huu wa nauli. Mheshimiwa Waziri ruzuku ya Serikali tumeweka kwenye mafuta, Serikali tunaishukuru kwa kuweka ruzuku ya fedha kwenye ununuzi wa mafuta, hali hii haijapunguza mpaka leo. Wakati tunaweka ruzuku lita ya mafuta ilikuwa shilingi 3,350 saa hizi lita ya mafuta ni shilingi 2,930. Kuna tofauti ya karibu shilingi 500 kwa lita lakini nauli haijapungua. Tutazame eneo hili kama sababu zinatosha za gharama za nauli kubaki pale halafu huku tumeweka ruzuku ya Serikali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine ni eneo ambalo tunapenda kuishauri sana Serikali itoe fedha za Wizara hii kadri ambavyo zimeombwa na Mheshimiwa Waziri na Wizara yake ili walau mgongano huu wa kulia umeme na kuomba umeme mara kwa mara upungue, kwa sababu yale yaliyowekwa kwenye vipaumbele hivi na Mheshimiwa Waziri viweze kutekelezwa na ili vitekelezwe ni fedha tulizoomba Serikali ijitahidi namna ya kutoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ingawa siyo kwa umuhimu, ninaomba basi hali hii ya baadhi ya maeneo kwenye mji, Mheshimiwa Waziri tuma timu, fanya ziara mahususi na wewe kwenye maeneo ya Miji kama Mbulu na vijiji vyake. Ninawapongeza Waheshimiwa Mawaziri tuliyowaambia Mbulu Mji una maeneo mawili na maeneo hayo mawili kwa ujumla yameweza kutembelewa na kila Wizara iliona jitihada zake na kuongeza fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naunga hoja mkono kwa asilimia mia moja. (Makofi)