Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuzungumza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote na mimi niungane na wenzangu kwa dhati kabisa kuunga mkono bajeti hii kwa mipango mizuri ambayo Mheshimiwa Waziri amekuja kutuonesha hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuunga mkono nizungumzie utekelezaji wa mradi wa REA katika Jimbo la Mbinga Vijijini. Ninaipongeza Serikali kwa nia ya dhati kabisa kwamba ina lengo la kutekeleza mradi huu ifikapo mwaka wa fedha ujao, kwamba ifikapo mwaka wa fedha ujao basi vijiji vyote vitakuwa na vimefikiwa na umeme kupitia mradi huu wa REA. Ninaipongeza sana Serikali na kwa kweli imeonesha dhati hiyo kwa sababu vijiji vingi katika Majimbo mengi asilimia ya utekelezaji ni kubwa sana, lakini napata shida kubwa sana mradi huu namna unavyotekelezwa katika Jimbo la Mbinga Vijijini, na napata hofu kubwa kama lengo hili la Serikali litafikiwa kwa namna Mheshimiwa Waziri alivyolisema hapa wakati anatuhutubia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Mbinga Vijijini lina vijiji 117, vijiji 44 tu mpaka leo ndivyo vilivyofikiwa na umeme wa REA, vijiji zaidi ya 70, mahala pengine ni Majimbo mawili haya, hawajafikiwa na umeme huu. Vijiji 30 hata nguzo hazijafika, kilichofanyika katika vijiji hivyo ni survey tu. Naomba nikusomee hapa Mheshimiwa Waziri usifikirie natamka tu, vijiji 30 havijafanyiwa kazi kilichofanyika ni survey tu, hamna nguzo hamna mashimo, hamna chochote, vijiji hivyo ni Kijiji cha Mkalite, Kijiji cha Mkoa wa Asili, Kijiji cha Langiro, Kijiji cha Makonga, Kijiji cha Ndanga, Liyombo, Ukombozi, Kizota, Kitumbi, Muhilo, Matuta, Lingomba, Mkoha, Langilo Mkaoni, Mkuka, Kihongo, Kitesa, Ugano, Tunolo, Njombe, Ndembo, Ulorela, Silo, siyo wewe Mwenyekiti, hiki ni Kijiji chetu kule. Kijiji cha Mpawa, Sara, Kihumboburu, Mapipili, Liwii na Kiangimauka. Vijiji hivi hata nguzo hazijafika huko sasa napata shida sana ikiwa lengo hili linaweza kufikiwa kama alivyotamka Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu, Mheshimiwa Waziri mimi nakuamini sana wewe namuamini pia Naibu Waziri, pia na wataalam wa mradi huu REA nawaamini wako vizuri, uzuri nimefika kwako ulinikutanisha na hao wataalamu tukapanga mkakati mzuri wa namna ya utekelezaji wa huu mradi, lakini nikuambie Mheshimiwa Waziri tangu tulivyokutana naye mwaka jana mwezi wa nane amewasha vijiji viwili tu, pamoja na mpango mzuri aliousema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tuliongea na Mheshimiwa Waziri na hivyo vijiji vimewashwa baada ya mimi kuja kwako, vijiji viwili tu vya Charukalasi na Kijiji cha Lihale. Vijiji hivyo vingine vyote havijawashwa, sasa huu toka mwaka jana mpaka mwaka huu na anasubiri pengine bajeti inakuja ndiyo wanafanya fanya hizi kazi ikiisha hii bajeti kimya. Ombi langu la kwanza, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana, hebu njoo Jimbo la Mbinga Vijijini, najua kufika kwako wanasema mgeni aje mwenyeji apone, inawezekana kabisa ukifanya ziara katika Jimbo hili mabadiliko yanaweza kutokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili niombe Mtendaji wa REA amenihakikishia, hapa naipongeza Serikali kwa sababu fedha zipo shida siyo fedha, kama shida ni huyu Mkandarasi basi ifanyike namna kuliko tunakaa maeneo mengine miradi inaenda mpaka hii kilomita mbili hizi watu wametekeleza sisi kule kilomita mbili hatujaanza, hatujui tutaanza lini bado tunahangaika na ile kilomita moja hivi vijiji 70 vyote havina kitu. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri na niko chini ya miguu yako nyumba yangu inaungua moto kule njoo uizime. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine niombe Wilaya ya Mbinga kunakatika sana umeme na hapa yamezungumzwa sana. Nilisema mwaka jana lakini niliuliza swali hapa, Serikali iliahidi itafanya utekelezaji bajeti inayokuja ya 2024/2025, sasa kwa sababu mipango yetu ni mizuri na inaenda vizuri, mimi niombe ule mpango muurudishe uanzie mwaka huu kwa sababu hali inavyokatika umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shida ni kwamba ile lane ni ndefu sana ukianzia Songea, ije Mbinga mpaka Nyasa lane ni moja. Kwa hiyo, ninaomba sana ile mipango ya ujenzi wa substation basi na sisi awamu hii mtufikirie tuwe na substation pale, kwa sababu ukuaji wa Mbinga ni mkubwa sana, sasa hivi tuna Uchimbaji wa makaa ya mawe watu wameongezeka sana na tuna viwanda vingi sana viko pale vya kahawa na viwanda vingine vya maji, kwa hiyo wanahitaji umeme kwa ajili ya uzalishaji. Nikuombe Mheshimiwa waziri utufikirie tupe substation ili na sisi tusahau shida hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ninampongeza sana Mheshimiwa Rais wa nchi hii, nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake kwa kufanikisha mazungumzo haya ya LNG, kwa sababu mazungumzo haya kwa kweli yalikwama muda mrefu sasa yanaonesha njia kabisa kwamba tunaenda kupata mradi huu mkubwa wa kuingizia pato kubwa nchi yetu. Hongereni sana, hongereni sana hongereni sana Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee lile suala la hofu ya mradi ule wa Songas, mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri wakati tunaenda na miradi hii mikubwa hata ile miradi midogo midogo ambayo ilikuwa inatusaidia wakati tuna crisis ya umeme tusiisahau, tusiiache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumbukumbu zangu kama niko sawa sawa mradi huu ni wa PPP na unaunda na wabia wa nchi tatu, Tanzania ikiwemo Norway na Uingereza. Sasa nikuombe Mheshimiwa Waziri, ule mkwamo uliopo wa hofu iliyopo katika kampuni hii, kwamba mkataba inawezekana Serikali haina haja ya kuendelea na mkataba, kwamba TANESCO ndio inaweza kuendesha huu mradi. Aah! mimi nikuombe Waziri fanya mambo, kama kuna vipengele katika ule mkataba havifai na mimi najua wewe uko makini pengine linaloonesha hapa kukwamakwama kidogo ni vipengele vya mikataba wa ule mkataba, ikiwemo Naibu Waziri ni Mwanasheria mzuri sana lakini najua una wanasheria wazuri sasa hivi katika Wizara yako, kaeni chini mjadili, wekeni vipengele kwa manufaa ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua huu mradi umetusaidia sana, sasa hivi pale Lindi pamechangamka sana, sasa huu mradi ukiwa unaondoka kwa kweli tutaparudisha nyuma na mimi niko eneo hilo la Mikoa ya Kusini ya Ruvuma, Lindi na Mtwara ni Mikoa inayoingiliana, kuchangamka kwa Lindi, kuchangamka kwa Mtwara ndiko kuchangamka kwa Ruvuma. Tukuombe sana Mheshimiwa Waziri endeleza mazungumzo hayo, kwamua huu mradi uendelee kuwepo, wananchi waendelee kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la mwisho nizungumzie suala la mradi huu mkubwa wa Bwawa la Nyerere. Hatua iliyofikiwa na maneno aliyotuambia hapa Mheshimiwa Waziri yamenitia faraja kubwa sana na wananchi wangu Mheshimiwa Waziri wamenipigia simu kwamba walikuwa wanasikia hadithi. Sasa maneno uliyoyasema hapa wamefarijika sana, wanakupongeza sana Mheshimiwa Waziri, pia wanampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa sababu hakurudi nyuma alikwenda mbele kutoa fedha na sasa tunaambiwa baada ya wiki moja bwawa lile lina uwezo wa kuzalisha umeme, lina uwezo wa kuanza kuzalisha umeme. Hongera sana Mheshimiwa Waziri lakini hongera sana kwa Awamu ya Sita kwa kutenda kazi hii njema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)