Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi jioni ya leo na mimi niweze kuchangia katika hotuba ya bajeti ya Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ningependa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kupeleka fedha nyingi kwenye miradi ya maendeleo iliyopo katika sekta hii ya nishati ambayo kwa sasa inakwenda kwa speed kubwa lakini inatekelezwa kwa ufanisi mkubwa sana, nampongeza sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ningependa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa namna ambavyo kwa kushirikiana na Naibu Waziri wake, Katibu Mkuu, pamoja na Viongozi wa Taasisi mbalimbali zilizo chini yake wanavyoisimamia vizuri miradi hii, kwa kweli miradi inakwenda vizuri nawapongeza sana, nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona mradi LNG umeanza kutekelezwa, unapozungumzia Mradi wa LNG kwa Mikoa ya Lindi na Mtwara ni mradi ambao ni very sensitive kwa kweli, pale katikati ulipokuwa umekwama kwa miaka saba watu wengi katika Mikoa ya Lindi na Mtwara walisononeka sana. Pia, napongeza namna ambavyo Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere unavyotekelezwa, nimefarijika sana kusikia kwamba pale Mkoani Lindi kunaenda kujengwa Chuo cha Masuala ya Umeme, Masuala ya Mafuta pamoja na Gesi tena chuo chenyewe ni chuo chenye hadhi ya Kimataifa hongera sana Mheshimiwa Waziri na timu yako kwa kazi nzuri mnayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo maeneo kadhaa ya kushauri, katika Mkoa wetu wa Lindi tuna changamoto kubwa sana ya upatikanaji wa umeme, umeme umekuwa ukikatikakatika mara kwa mara inafika wakati, kwa mfano kama katika Wilaya yangu ya Kilwa ndani ya massa 24 umeme unaweza ukakatika hata masaa nane, mara nane kwa hiyo hii ni changamoto kubwa lakini hata taarifa nilizonazo kule kwa Mheshimiwa Kuchauka - Liwale, kule kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu - Ruangwa, Nachingwea na hata Manispaa ya Lindi kwa kweli kadhia hii imekuwa kubwa sana, ninamuomba Mheshimiwa Waziri ule mwarobaini anaopeleka Mkoani Mtwara basi pia aweze kuuleta katika Mkoa wetu wa Lindi ili wananchi wetu wapate umeme wa uhakika.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili ambayo ningependa kuizungumza ambayo niliizungumza pia mwaka jana na Wabunge wengi walichangia mwaka jana, kumekuwa katika maeneo fulani ya vijiji watu wetu wananchi wetu wamekuwa wakitozwa gharama ya shilingi 320,000 kwa ajili ya kuunganishiwa umeme, hiyo kadhia bado ipo inaendelea, ningeomba wizara ichukue hatua katika kuhakikisha kwamba wananchi wetu wa vijijini wanaendelea kulipa kiasi cha shilingi 27,000 badala ya 320,000 kuna vijiji vya Somanga Kaskazini, Somanga Kusini, Masoko, Kivinje, Nangurukuru wanatozwa 320,000 kuunganishiwa umeme, kwa hiyo nikuombe Mheshimiwa Waziri tusaidie katika hili jambo ili wananchi wetu waweze kuunganishiwa umeme kwa ile ada ambayo wanatakiwa kutozwa katika level ya vijiji.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yetu ya Kilwa ilikuwa ikipata CSR kubwa tu inayozidi bilioni moja kwa mwaka kutoka taasisi ambayo inachakata gesi pale Wilayani Kilwa katika eneo letu la Somanga, Taasisi inaitwa Pan African lakini kadri miaka inavyoendelea mbele kile kiasi ambacho tulikuwa tunapatewa kama CSR kimekuwa kikipungua sana, sasa hivi tunapata chini ya nusu ya kiwango ambacho tulikuwa tunapata mwaka 2005 wakati mradi huo ulipoanza kutekelezwa. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri tunajua pale Kilwa tumepata miradi mingi tu tumetekelezewa kupitia hiyo CSR, kwa mfano pale Somanga Kituo cha Afya kimejengwa, Chumo Kituo cha Afya kimejengwa, Songosongo hivi sasa Kituo cha Afya kinajengwa, zile fedha zinatusaidia sana, kwa hiyo niombe lile fungu lile la CSR lirudi kama lilivyokuwa zamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la ulipaji wa fidia katika Kitongoji cha Cheketu, Kijiji cha Somanga Kusini. Tangu mwaka 2017 ilifanyika tathmini ili lile eneo ijengwe miundombinu ya umeme ya TANESCO, lakini mpaka leo zaidi ya milioni 300 wale wananchi wanadai hazijaweza kulipwa, mwaka jana tuliahidiwa mwaka huu wa fedha zile fedha zingelipwa, ninaomba Mheshimiwa Waziri alichukue hili na wale wananchi walipwe haki yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho ambalo ningependa kulizungumzia ni suala la umeme wa REA. Katika Wilaya yangu ya Kilwa utekelezaji wa umeme wa REA unakwenda vizuri katika vile vijiji vilivyolengwa. Tunayo shida tu kidogo katika visiwa vilivyopo kwenye Bahari ya Hindi. Kilwa Kisiwani, Songomnara, havijaainishwa katika utekelezaji wa umeme wa REA katika kipindi hiki, kwa hiyo ningeomba hilo liangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna maeneo ambayo ni umbali mrefu sana kutoka Kijiji kimoja kwenda kingine wakati kuna vijiji vya Mkoa wa Pwani kule kwa mpwa wangu Mheshimiwa Mchengerwa vyenyewe vinakaribiana na tayari vilishaletewa huduma ya umeme. Kwa mfano kuna Kijiji cha Ngalambilienga, chenyewe ni kilomita saba unakwenda kwenye Kijiji cha Wilaya ya Rufiji, kile Kijiji cha Wilaya ya Rufiji tayari kilishafikishiwa umeme katika zile awamu za awali za utekelezaji wa umeme wa REA, ningeomba badala ya kwenda kuchukua umeme Makao Makuu ya Kata ya Kandawale ambako ni kilomita 38, tutengeneze utaratibu wa kuvuta huu umeme kilomita hizi saba toka Mkoa wa Pwani ili tuweze kufanya serving ya zile kilomita 31 ambazo ningependekeza zipelekwa sasa maeneo mengine kwa mfano, kuna kitongoji ambacho kinakua kwa kasi sana katika Kijiji cha Zinga Kibaoni kilomita 22, ningependa ile ziada ya kilomita 31 ipelekwe kule ili wananchi wa kule nao waweze kupata matumaini kwani tayari walishakuwa wamekata tamaa. Kwa hiyo ningeomba hilo lifanyike lakini zile kilomita zitakazobaki basi zinaweza zikapelekwa katika Makao Makuu ya Tarafa za Kipatimu, Njinjo pamoja na Miteja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa leo sina la ziada, zaidi ya kuendelea kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri, kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri wanayofanya, naomba nihitimishe kwa kusema naunga mkono hoja kwa asilimia 100. Ahsante sana. (Makofi)