Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya katika sekta hii ya nishati, kipekee nikupongeze Waziri wa Nishati, Kaka yangu Mheshimiwa Makamba hongera sana kwa kweli unachapa kazi. Ninakupongeza Wakili Msomi Naibu Waziri, ni msikivu, unafikika na unapokea simu muda wote, niwapongeze Watendaji nikianza na Mtendaji Mkuu Engineer Mramba ambaye ni Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu Ndugu yangu Athumani Mbuttuka kwa kweli mnachapa kazi na kazi inaonekana katika Wizara hii, hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ina changamoto kubwa sana lakini jana Mheshimiwa Waziri Mkuu amesema maneno ya faraja wakati anakagua ile wiki ya nishati pale kwenye mabanda. Amesema acha wao waseme Wizara chapeni kazi. Mheshimiwa Makamba chapa kazi. Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere kulikuwa na maneno mengi sana, lakini umesema kwenye mawasilisho yako hapa tumefikia asilimia 87 sasa hivi, bado kumi na tatu tu hongera sana. Tunao mradi wa REA, mradi mkubwa na Afrika kwa sasa hivi tunaongoza coverage ni vijiji asilimia 82, tumebakiwa na asilimia 18 hongereni sana, chapeni kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nijielekeze kwenye mradi wa LNG. Ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kama wenzangu walivyosema mradi huu ulienda kwa kasi sana huko nyuma, baadae miaka saba mradi huu ulisinzia lakini kwa upendo wake Dkt. Samia Suluhu Hassan akaagiza majadiliano yaanze tena kwa kasi. Ninakupongeza Mheshimiwa Waziri Makamba kwa kusimamia hayo majadiliano na ku-fast track majadiliano na tuliona ulitualika Wabunge wa Mtwara na Lindi pale Ikulu wakati kuna signing ceremony ya makubaliano ya awali, lakini kwenye taarifa yako umesema makubaliano, majadiliano mmeshahitimisha mna-draft mkataba, hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama walivyosema wachangiaji waliopita wenzetu wa Jimbo la Cabo Delgado Msumbiji wakati tunasinzia na mazungumzo wao walianza kwa kasi mwaka 2019, hivi karibuni nafikiri watakamilisha, lakini kwa jitihada zako nafikiri kutangulia siyo kufika ili mradi sisi tumetoka nyuma lakini kwa kasi kubwa tutafanikiwa, kwa hiyo endelea hapo na tunakuombea kila la kheri hatua iliyobaki ikamilike ili wananchi wa Mtwara na Lindi kama walivyosema wenzangu na Watanzania kwa ujumla wanufaike na mradi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nina ushauri kuhusu mradi wa LNG. Wakati mradi huu ulipoanza Serikali na wale wawekezaji waliunda Kamati mbili kubwa. Kamati ya kwanza ilikuwa kwa ajili ya upatikanaji wa ardhi (Land acquisition) na Kamati ya pili ilikuwa ni kuihusisha jamii kwenye mradi (community engagement) na Kamati hizi zilifanya kazi zake kwa kushirikiana na wananchi wa maeneo husika ya mradi kule Likong’o – Lindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ardhi limekwishakamilika kama ulivyosema nikupongeze Mheshimiwa Hamida kwa kufuatilia na sasa wananchi wake wengi wamepata fidia. Suala la kuishirikisha jamii naomba Waziri Kamati hii iendelee, kuna mambo mengi ya kufanya kwenye jamii. Vijana, wanawake, wazee na makundi ya kijamii ni lazima yajulishwe hatua zinazoendelea katika mradi huu, waelezwe fursa zilizopo, waeleze jinsi watakavyonufaika na mradi huu na mipango ya Serikali kuwa – engage wao katika mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri umesema vizuri kwamba unajenga chuo kikubwa pale Lindi lakini huko nyuma tulikuwa tunawapeleka vijana wapate elimu ya kati katika Chuo cha VETA Mtwara na VETA Lindi ili wapate ujuzi na maarifa ambayo mradi ukianza wataweza kuajiriwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tu Kamati hii ina kazi ya kuwaelimisha jamii jinsi ya kuishi na mradi. Miradi hii Kwa wenzetu ambao wametangulia kuna changamoto nyingi, wanaweza kuja watu wakaichonganisha jamii na Serikali yao, tujifunze yaliyotokea Nigeria kuhusu Boko haramu, lakini Jimbo la Cabo Delgado Msumbiji kuna maharamia ambao wanahujumu mradi, wamekwenda kule wakashawishi vijana kwamba Serikali inafanya mradi huu lakini ninyi hamtanufaika wakaanza kufanya zile vurugu. Kwa hiyo, sisi tuwatayarishe vijana wetu, wananchi wetu kuishi na mradi kama sehemu ya jamii ili yale yanayotokea kule Cabo Delgado Msumbiji na Boko Haram kule Nigeria yasitokee nchini kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku ya kusaini makubaliano ya awali pale Ikulu, Mheshimiwa Rais alitoa maagizo makubwa sana kwa Mheshimiwa Waziri alisema “wananchi wa maeneo husika ya mradi wasiishi kama walivyo sasa hivi” tunatarajia kwamba mradi ukianza Lindi haitakuwa kama ilivyo leo tunatarajia sasa Uwanja wa Ndege wa Lindi sasa ujengwe ili wawekezaji watumie uwanja ule wa Lindi. Tunatarajia sasa barabara za Lindi na Mtwara zitaimarishwa kwa sababu tuna kundi la watu zaidi ya 10,000 kwa ajili ya ajira rasmi na zisizo rasmi, watu hao ni wengi lazima tupanue huduma za afya huduma za elimu na huduma za kijamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuntarajia sasa hivi kwamba hata upatikanaji wa maji, wananchi wa Lindi wasitegemee mradi wa Ng’apa tu, tuwe na miradi mingine ili kuhakikisha wageni watakapokuja kusiwe na changamoto ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili utahusu changamoto za umeme Mkoani Mtwara kama walivyosema wenzangu. Mheshimiwa Waziri ninakupongeza kwa usikivu wako tulifanya kikao juzi na sina haja ya kurudia mambo tuliyokubaliana, ninakuomba sasa kayatekeleze yale, nikupongeze kwa sababu nimepata taarifa timu yako sasa iko Mtwara, kwa hiyo, yale tuliyokubaliana kwanza yale ya muda mfupi kwambab utapeleka sasa turbine kutoka Dar es salaam ili iende Mtwara ikazalishe megawatt 20 basi kazi hiyo ifanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, furaha kwetu wana Mtwara umesema kwenye hotuba yako kwamba ule mradi mkubwa wa megawatt 300 wa eneo la Naumbu pale Mtwara utaanza kutekelezwa tunakushukuru sana. Tunaomba mazungumzo na Serikali ya Japan yaendelezwe kama ulivyosema kwamba wameahidi kutoa fedha yaharakishwe, fedha zipatikane mradi ujengwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi ule umesema utajenga line ya kilometa 208 kutoka pale Mtwara hadi Somanga Fungu hapo unatudhihirishia kwamba sasa umeme wa uhakika kwa Mikoa yetu ya Mtwara na Lindi utakuwa unapatikana. Si hivyo tu, umetuthibitishia sasa kwamba ile kazi ambayo inafanywa kutoka Songea hadi Tunduru – Masasi kuiunganisha Mtwara kwenye gridi ya Taifa, basi fedha zimepatikana ili kazi iendelee kutoka Masasi hadi Mahumbika - Lindi. Ukifikisha gridi ya Taifa pale Mahumbika tuna uhakika sasa Lindi na Mtwara tutakuwa na umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkurugenzi wa TANESCO nawaombeni sasa yale ambayo tumekubaliana basi mtembee katika matamshi yenu na sisi tuna imani na ninyi na tutaendelea kuwapa support na pale tutakapohitaji kuwakumbusha tutawakumbusheni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwishoni usambazaji wa….

MWENYEKITI: Mheshimiwa Chikota, muda wako umeisha, malizia sekunde thelathini.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la langu la tatu ni usambazaji wa gesi asilia majumbani. Tumeona hapo taarifa ambayo imeandikwa kwamba Mtwara hadi sasa kuna nyumba 420 tu, Lindi kuna nyumba 209, naomba fedha zitengwe kasi iongezwe ili wananchi wa Mtwara na Lindi wanaufaike na gesi asilia pia tupunguze matumizi ya kuni majumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga hoja mkono. (Makofi)