Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuungana na Waheshimiwa Wabunge katika kuchangia hoja ya bajeti ya Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kuwapongeza Wizara kwa uwasilishaji wa taarifa yao ya bajeti ambayo imepunguza maswali mengi ya Waheshimiwa Wabunge na imetupa matumaini makubwa kwamba bajeti hii sasa inakwenda kutekeleza miradi mingi katika nchi yetu na kuendelea kuleta mapinduzi makubwa ya nishati katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri, January Makamba, kwa kuweka Wiki ya Nishati. Imetusaidia sana kwa sababu tumepata elimu tosha na imeweza kutupunguzia maswali mengi ambayo tungeweza kuyauliza ama kuchangia hoja katika Bunge letu hili. Kwa hiyo, nikupongeze lakini niendelee kukutakia heri katika mipango mizuri ya utekelezaji ambayo tunategemea 2023/2024 tunakwenda sasa kuleta mapinduzi ya ukweli katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipongeza Serikali kwa kuendeleza Gridi ya Taifa. Mkoa wa Lindi kwa maana ya Lindi tunategemea sana umeme kutoka Somanga, umeme kutoka Mtwara, pia Mtwara panapotokea changamoto ya mashine zao kufeli, maana yake Lindi tunapata umeme wa mgao kwa hiyo inakua ni changamoto kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunafarijika kuona kwamba mradi wa Gridi ya Taifa unaotoka Makambako – Songea – Masasi – Maumbika kwenye power extension, maana yake tutakuwa sasa na umeme wa uhakika na sasa tutakaribisha uwekezaji katika Mkoa wetu wa Lindi kama ambavyo tumejipanga kuhakikisha kwamba fursa za uwekezaji Lindi ziko nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme huu wa Gridi ya Taifa ambao tunautegemea kutoka Makambako pia utakwenda kutoka Masasi kuelekea Nachingwea – Liwale, lakini kutoka Nachingwea kuelekea Ruangwa. Kwa hiyo, tunausubiri kwa hamu sana. Lakini tunaona kwamba mradi huu umechukua muda mrefu, ni mpango wa zaidi ya miaka mitatu, nikuombe kuhakikisha kwamba mradi huu unakwenda kwa haraka na sisi Wanalindi na Mtwara tuendelee kufaidika na Gridi ya Taifa ili uwekezaji wetu uweze kuwa rahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana kwa dhati ya moyo wangu Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na niwapongeze, Waheshimiwa Wabunge leo waliochangia mradi wa LNG maana kila mmoja amehamasika kuchangia mradi huo wa LNG nakuona sasa tunakwenda ukingoni katika utekelezaji wa mradi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa LNG ulianza karibia miaka saba iliyopita lakini tunashukuru kwamba Serikali yetu imekuwa Sikivu, imepitia hatua mbalimbali na hatimaye wananchi wetu wameweza kulipwa fidia katika eneo la mradi na hatua mbalimbali shirika la TPDC wameweza kuchukua. Katika eneo wameanzisha barabara za ndani kwa ndani tunashukuru vijana wa Lindi wameweza kupata ajira, lakini tulichokuwa tunategemea sasa katika eneo lile TPDC waje kufanya usafi wa mazingira pale kuhakikisha kwamba eneo linakuwa safi. Walianza kwa hatua nzuri lakini ghafla wakasimama hatuelewi sababu ya kusimama kwao ni nini lakini tunategemea kwamba eneo lile liwe safi kwa ajili ya maandalizi ya utekelezaji wa mradi huu wa LNG.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mradi huu tumeendelea kupata fursa mbalimbali, tumewapokea EPZA wamekuja Lindi na tumewaonesha maeneo mbalimbali ya uwekezaji, kwa hiyo tunategemea sasa fursa nyingi kuja Lindi kuongeza mzunguko na uchumi mkubwa lakini kuongeza ajira katika Mikoa yetu ya Lindi na Mtwara na hatimae nchi nzima ya Tanzania. Kwa hiyo, sisi kwetu ni maendeleo makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninaipongeza Wizara ya Nishati kwa kusimamia uwekezaji wa ujenzi wa chuo cha masuala ya umeme pale Lindi katika eneo la Kata ya Mbanja, Kata ambayo unakwenda kutekelezwa mradi wa LNG na Mtaa wa Makasialeo ndipo ambapo Chuo hiki kitajengwa na hatua mbalimbali wameanza kutekeleza katika ujenzi wa chuo hiki. Sisi kwetu ni mapinduzi makubwa na ni faraja kubwa kwa sababu watakao faidika wa kwanza na mradi huu wa LNG ni sisi wana Lindi. Tunashukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita kuhakikisha kwamba inakwenda mbio katika kuhakikisha mradi huu unakwenda kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la REA. Tunashukuru mradi wa REA umetekelezwa kwa kiwango kikubwa na sasa hivi tunaona kwamba vijiji vingi vinapata umeme, vijiji vilivyobakia ni hatua ndogo na Mungu akijalia mpaka 2024 itakuwa vijiji hivi vimeweza kukamilika na wananchi watanzania tutakuwa tumepata umeme kila kona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikushukuru sana nilikuletea kilio kutoka Lindi Manispaa, ipo mitaa ambayio ilikuwa haijapata umeme. Tunajua kwamba mradi wa Peri-urban ilibidi utufikie pale Lindi Manispaa lakini kutokana na changamoto mbalimbali maana yake mradi ule umechelewa na wala hatutegemei kuja Lindi kutekeleza mradi wa Peri-urban. Ninakushukuru sana umekuwa msikivu, tulipoleta maombi yetu ya mitaa kadhaa itekelezwe mradi huu wa REA ulitukubalia. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ametutengea fedha bilioni tano katika kutekeleza mradi huu wa REA katika eneo la Lindi Manispaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu utatekeleza kilomita 26.4 njia kubwa lakini njia ndogo ni kilomita 13.7, kwa hiyo ninategemea kwamba baada ya bajetii kukamilika Mkandarasi ataanza kazi kwa sababu mkandarasi tayari ameshakuja kuripoti na maeneo tayari yameshafanyiwa kazi, tunasubiri tu fedha itoke ili Mkandarasi aingie kazini aweze kutekeleza mradi huu wa REA. Watakao nufaika na mradi huu ni ndugu zetu wa Mtaa wa Jangwani, Nyange, Chikonjwi, Ruaha Mnazi Mmoja pamoja na maeneo mengine. Mheshimiwa Waziri kwa hiyo nakushukuru sana Mungu akubariki na tuendelee kukuombea ili Watanzania tuweze kupata huduma kutoka Wizara hii ya Nishati na Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la mradi wa matumizi ya gesi majumbani. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wetu wa Nishati kwa kampeni hii mahsusi ya kumtua mama kuni kichwani, kwa kweli tunaiunga mkono Waheshimiwa Wabunge maana yake sasa tunakwenda kwenye kampeni maalum ya kuhakikisha kwamba wananchi wanaondokana na matumizi ya kuni na mkaa lakini wanakwenda kutumia nishati iliyo safi. Hili ni jambo jema kwetu kwa sababu matumizi ya kuni na mkaa yana athiri afya ya mwanadamu na tunajua ya kwamba matumizi ya gesi yanarahisha katika matumizi ya kupika pamoja na mambo mengine badala ya kutumia muda mrefu unatumia muda mfupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Lindi Manispaa Mnazi Mmoja tuna power extension ya matumizi ya gesi majumbani, Serikali ilituahidi nyumba mia mbili mtatufungia lakini mpaka leo hatujaona utekelezaji wa nyumba mia mbili kufungiwa matumizi ya gesi majumbani. Mheshimiwa Waziri kwa hiyo ningeomba utakapokuja ku-wind up utuambie ni lini utakuja kutekeleza na kukamlisha mradi huu wa nyumba mia mbili kuweza kufungiwa gesi majumbani ili wananchi waendelee kutumia kadri wanavyoweza kutumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi ya gesi ni muhimu sana kwetu na mimi niendelee kuiomba Serikali kwa sababu wananchi wanapenda kutumia gesi, wanapenda kutumia umeme lakini vifaa vya matumizi hayo kwa mfano majiko ya umeme, majiko ya gesi yamekuwa ya gharama kubwa. Wananchi wetu hawawezi kumudu kununua majiko ya gesi na majiko ya umeme. Niombe sana Serikali kupitia Wizara ya Fedha katika bajeti hii inayokuja kuona namna gani wanapunguza kodi ili Watanzania walio wengi waweze kumudu kununua majiko ya gesi ili tuendeleze kampeni hii ya kumtua mama kuni kichwani tuone tumefikia kwa kiwango gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hilo ni jambo jema litatuletea tija na Watanzania wengi wataondokana na matumizi ya kuni na mkaa majumbani kwa sababu tunaona uharibifu wa mazingira unaendelea kukua kwa kasi kubwa sana na tunaona hali ya mabadiliko ya tabianchi, joto limekuwa kali mvua hazipatikani kadri tunavyotumaini. Kwa hiyo, tuone namna bora ya kuhakikisha kwamba wananchi wa Tanzania wanaondokana na matumizi ya kuni na mkaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninaunga mkono kwa asilimia mia, ahsante sana. (Makofi)