Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii ili niweze kutoa mchango wangu wa mawazo kwenye hotuba ya Wizara hii ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, kwanza nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa nafasi aliyonipa, kuendelea kupumua lakini nitumie nafasi hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa utendaji kazi wake mzuri lakini na ujasiri wake mkubwa katika kufanya maamuzi na kutenda kwa maslahi ya wananchi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee nitumie nafasi hii kukupongeza sana kwa umahiri wako mkubwa katika kutuongoza Bunge hili. Nitakuwa mchoyo wa fadhila kama nisipowapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara ya Nishati, kwa kweli wanaonesha umahiri mkubwa na wanatenda mambo mengi yenye maslahi kwa Taifa letu, tuna kila sababu ya kuwatia moyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utakuwa kwenye maeneo mawili, nikitambua umuhimu wa nishati kwa sababu tafiti mbalimbali zimeonesha mahusiano ya moja kwa moja kati ya nishati ya umeme na maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwenye Jumuiya mbalimbali, umeme hasa kwa ujumla ni jambo muhimu sana na kazi kubwa iliyofanywa na Serikali yetu kusambaza nishati hii ya umeme tuna kila sababu ya kupongeza.

Mheshimiwa Spika, ninaushauri kwenye maeneo mawili, eneo la kwanza ni eneo la REA. Kazi kubwa imefanyika na kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake, tuna vitongoji zaidi ya 36,000 ambavyo havijapata umeme, bado kuna kazi kubwa inatakiwa kufanyika. Ni kweli kwamba katika usambazi vijiji vingi vimepata nishati hii ya umeme lakini tuna kila sababu ya kufanya tathmini sasa tukiangalia vitongoji lakini tuende zaidi kwa kuangalia idadi ngapi ya kaya ambazo zimepata nishati ya umeme, itatupa changamoto na kuona namna gani tuna kazi nyingine kubwa ya kufanya ili tuweze kufikisha nishati hii ya umeme, kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba REA imefanya kazi kubwa lakini bado tunahitaji tubuni vyanzo vingine kuweza kusaidia Mfuko wa REA ili angalau mfuko huu ukiweza kutuna basi nishati hii ya umeme iweze kusambaa zaidi kwenye vitongoji vyetu. Kwa hiyo, mimi kwa nafasi yangu ningeweza kupendekeza ikiwezekana hata kwenye nishati kwa mfano, kwenye mafuta ikiongezwa hata shilingi moja tuweze kuongeza vilevile kutunisha Mfuko wa Nishati hii ya umeme ili maeneo yetu yaweze kupata umeme. Kwa sababu pamoja na nishati hii kusambaa kwenye vitongoji, kwenye Jimbo kwa mfano la Ukerewe bado tuna vitongoji vingi havijapata umeme, mbaya zaidi kuna vitongoji ambavyo vimefikishiwa umeme umefika kwenye kitongoji lakini kaya nyingi bado hazipata nishati hii ya umeme. Kwenye vijiji kwa mfano kama Muruseni, Hamuyebe umeme umefika lakini bado kaya hazipata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo nilitamani nichangie ni kwenye maeneo yaliyo mbali na Gridi ya Taifa. Jimbo la Ukerewe tuna visiwa vingi ambavyo viko mbali na Gridi ya Taifa. Nikupongeze Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu, mmepata ujasiri mkaweza kututembelea Ukerewe mkaangalia changamoto zilizoko kwenye Visiwa vyetu vya Ukerewe. Bado visiwa vyetu vingi havijaweza kupata nishati hii ya umeme. Kisiwa kama cha Ukara, Mheshimiwa Waziri unakifahamu kuna watu pale Jumeme wanatoa umeme kama wanavyotoa kwenye Kisiwa cha Ilugwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nitoe ushauri kwenye Kisiwa cha Ukara, hebu kaa na wataalamu wako ikiwezekana na inawezekana angalieni, uwezekano wa kutumia sub-marine cable ili kuweza kuiunganisha Ukara na Gridi ya Taifa na kwa sababu sasa hivi mnapeleka umeme mkubwa, nikupongeze Mheshimiwa Waziri na Wizara yako, kwa mradi ambao mmeuandaa mnapeleka umeme kwenye Visiwa vya Ukerewe ambao kutoka KV 66 mpaka KV 132, umeme huo utahitaji kupata mzigo na ili mzigo huu uweze kupatikana ni muhimu sana visiwa kama cha Ukara ambacho kina Kata zaidi ya tatu ili kiweze kuunganishwa na Gridi ya Taifa kuongeza mzigo kwenye umeme huu mnaopeleka kwenye Visiwa vya Ukerewe. Kwa hiyo, nikushauri kaa na wataalam wako ikiwezekana muweke cable, sub-marine cable muweze kuunganisha kwenye eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile katika ukurasa wa 39 wa hotuba yako umeonyesha namna ambavyo mnajiandaa kupeleka umeme kwenye maeneo yaliyoko mbali na Gridi ya Taifa. Ninakuomba Mheshimiwa Waziri visiwa kama Gana, visiwa kama Burudi, Bwilo, Bweru, Sizu na kadhalika ambavyo kulikuwa na Wakandarasi walienda kwa ajili ya kupeleka umeme lakini wakaishia njiani, niombe sana kwa kushirikiana na halmashauri tunajitahidi kuondoa vikwazo vilivyopo ili sasa hawa wakandarasi walio tayari waende kupeleka umeme kwenye maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu ambalo nilitaka nichangie, yote haya tunawapongeza tuna wasifu kwa sababu kuna kazi inafanyika hasa kupitia Shirika letu la Umeme la TANESCO, lakini yote haya yanafanyika kwa sababu kuna watendaji, kuna watumishi, kuna wafanyakazi wanafanyakazi nzuri ndiyo maana shirika linafanya kazi nzuri. Mheshimiwa Waziri kuna minong’ono inaendelea chini kwa chini, wafanyakazi wako kwenye Shirika hili la TANESCO wanalalamika kuna mambo hayako vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mkataba wa kiutumishi waliokua nao kwa ajili ya kuboresha maslahi yao ya kiutendaji kazi, lakini katika haya moja katika malalamiko yao Mheshimiwa Waziri kuna mabadiliko yamefanyika, huko nyuma ilikuwa watumishi wakienda likizo wanalipwa mshahara wa mwezi mmoja ili waende likizo wakirudi wanaendelea na majukumu yao, lakini katika mabadiliko yaliyofanyika sasa inasemekana kwamba sasa watumishi wakiondoka kwenda likizo hawapewi pesa yoyote, anatakiwa aende kwa nauli yake, akishalipa nauli yake atunze risiti, akirudi ndiyo aanze kudai alipwe fidia kwa zile risiti kutokana na namna ambavyo amesafiri.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri jambo hili litawakatisha tamaa watumishi, liangalieni upya ikiwezekana mliondoe urudishwe utaratibu wa zamani ili watumishi hawa wafanye kazi wakiwa na morale, wakiwa na moyo kwa ajili ya kuleta sifa kwa shirika na tija kwa Taifa letu ili wananchi wetu waweze kupata huduma wanayoitarajia. Vilevile, Mheshimiwa Waziri wamekuwa hawana uhakika na mambo yao, wamekuwa na hofu kwamba inasemekana kwamba mnatarajia kupunguza watumishi kwenye shirika hili, mbaya zaidi taratibu hizi zinaendelea bila kuhusisha Chama cha Wafanyakazi, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri, kama kweli haya yapo Mheshimiwa Waziri ninaomba uyafanyie kazi ili changamoto hizi ziondoke, watumishi wetu katika Shirika la Umeme la TANESCO wafanyekazi wakiwa na moyo, wakiwa na morale ili tija ile tunayoitarajia kutoka kwenye shirika letu hili iweze kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia nikushukuru sana kwa nafasi hii, lakini ninakuomba tena Mheshimiwa Waziri Ukerewe tunakupenda tunakuhitaji na niwapongeze tena kwa ujasiri wenu kuja kututembela na kuona changamoto tulizonazo. Mtusaidie sana Visiwa vyetu vya Ukerewe ili waweza kufikia maendeleo tunayoyatarajia nishati ya umeme ni jambo muhimu sana, tusaidie sana, zaidi ya yote kwenye eneo la kisiwa cha Ukara kama nilivyoshauri, tafadhali kaa na wataalamu wako, wekeni sub - marine cable pale, muweze kuunganisha Kisiwa cha Ukara na Gridi ya Taifa. Vile Visiwa vingine vidogo ambavyo vina changamoto, changamoto zake mnazifahamu, tafuteni ufumbuzi wa haraka ili wananchi wetu waweze kwenda na kasi ya maendeleo na hasa kwa tija na kasi anayoionesha Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi, Mwenyezi Mungu akubariki sana. (Makofi)