Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Shanif Mansoor Jamal

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. SHANIF M. JAMAL: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie hoja ambayo iko mbele yetu. Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa pumzi, afya njema niweze kusimama hapa kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya ndani ya miaka miwili ya utawala wake, kwa kweli miradi yote ya kimkakati inatekelezwa na pia miradi mipya ameanzisha kwa kweli tumamshukuru sana na tunampongeza Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii tena kumshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kutuletea miradi mingi kwenye Jimbo la Kwimba katika kipindi hiki cha miaka miwili lakini niseme michache tu. Kwa kipindi cha mwaka mmoja huu tumepata hospitali mpya ya Wilaya, vituo vya afya viwili vipya. Kwenye masuala ya maji tumepata miradi mitatu mikubwa ya maji Hungumalwa sasa hivi tuna maji ya bilioni nne, Shibumulo pia kuna mradi wa maji unajengwa pale. Mambo haya niyaseme kwa sababu kwenye Jimbo la Kwimba tuna Kata 15 sasa hivi Kata 14 tuna maji ya Ziwa Victoria yote ni kwa sababu ya mafanikio ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Tumebakiza Kata moja tu ambayo tunategemea mwaka ujao tutapata maji, maana yake Jimbo la Kwimba wananchi wote wanapata maji safi na salama ya Ziwa Victoria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu muda hautoshi nimesema miradi michache. Naomba nichukue nafsi hii kwenda kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri ya matumaini uliyoisema hapa tunakupongeza sana. Mheshimiwa Waziri, tunakupongeza kwa kazi nzuri unayoifanya wewe, Naibu wako, Watendaji wako wote wa Wizara ya Nishati, hongereni sana kwa kazi nzuri sana mnayoifanya. Vilevile, nichukue nafasi hii kupongeza taasisi zote ambazo ziko chini ya Wizara yako, wanafanya kazi nzuri inaonekana. Kwa kweli mwaka huu Mheshimiwa Waziri umekuja hapa hakuna kelele kwenye Wizara ya Nishati lakini nakumbuka mwaka jana ulipofika hapa kulikuwa na kelele nyingi kwenye Wizara ya Nishati, mwaka huu kidogo pametulia.

Mheshimiwa Spika, pia Mheshimiwa Waziri nikupongeze kwa maonesho ya mwaka huu yaliyofanyika kwenye viwanja vya Bunge pale nje, kwenye maonesho ya nishati. Nimefika pale nimekutana na watu wa REA na maeneo mengine mbalimbali, kwa kweli maonesho ni mazuri sana. Pia, teknolojia mliyotumia kutoka viwanja vya Bunge mmenipeleka mpaka Julius Nyerere nimefika kwenye bwawa pale nashukuru sana nimepaona sina cha kusema. Niseme tu hongereni sana kwa kazi kubwa mnayoifanya kwenye bwawa, endeleeni Mungu awatangulie kuhakikisha kwamba mradi ule kama ulivyosema kwenye hotuba yako kwamba mwaka ujao mradi utakamilika nawatakia kila la kheri ule mradi ukamilike.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri nitaongea hoja mbili tu. Hoja ya kwanza nitaongelea kuhusu REA. Mimi nawapongeza sana REA wanafanya kazi nzuri. Jimbo la Kwimba mimi nimebakiza Kata mbili ambazo ni Kikubiji na Mhande ambapo sasa hivi ndiko wanakofanya kazi, wamesema mpaka Agosti mwaka huu watakuwa wamemaliza kuunganisha umeme kwenye vijiji vyote. Ninashukuru Jimbo la Kwimba mpaka Desemba tutakuwa tuna umeme kwenye vijiji vyote, nashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, changamoto tunazopata ni kwamba wanaunganisha vijiji vingi lakini tatizo liko kwenye vitongoji ambavyo vimebaki, kwa sababu watu wameshaona utamu wa kupata umeme jirani sasa wanataka na wao wapate umeme, hiyo changamoto ni kubwa Mheshimiwa Waziri kama ulivyosema kwenye hotuba yako kwamba utatuunganishia vitongoji 15 kwa mwaka ujao kwa kweli kwenye mahitaji ya Jimbo la Kwimba haitoshi nafikiri na wengine pia haitatosha, mimi ninashauri kwamba hivi vitongoji 15 havitatosha tunaomba uongeze angalau vifike hata kwenye vitongoji 50 kwa mwaka kesho kuunganisha kwa kila Jimbo angalau tutakuwa tumepunguza kero kwa wananchi. Hilo ni ombi langu kuja kwako kwamba tunaomba utusaidie kuongeza vitongoji angalau vifike 50 kwa mwaka kesho.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine Mheshimiwa Waziri ningependa kulizungumzia hapa ni kwamba Jimbo la Kwimba tuliahidiwa kuletewa taa za barabara za REA, nina Mji wa Ngudu pale nina lami kilomita nne inaelekea kilomita tano lakini hakuna taa hata moja ya barabarani.

Mheshimiwa Spika, tunaomba angalau tuliahidiwa taa 200 tutaletewa ili angalau na miji yetu ipendeze kidogo kwa sababu sasa umeme uko vijijini, umeme uko kwenye miji, kwenye nyumba za watu lakini barabara ni giza. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ningeomba wakati wa majumuisho basi unisaidie angalau kunipatia hata taa hizo 200 za barabara angalau miji yangu ya Hungumalwa, Shilima, Ngudu, Gojiro, Malege na Milama angalau vipate taa za barabara. Mheshimiwa Waziri naomba utusaidie kwenye taa za barabara.

Mheshimiwa Spika, lingine Mheshimiwa Waziri ningependa kulizungumzia sasa hivi hapa ni suala la EWURA. EWURA wanafanya kazi nzuri sana lakini Mheshimiwa Waziri Sheria na Kanuni za EWURA zimepitwa na wakati. EWURA ilianzishwa na Sheria na Kanuni ambazo wakati ule tulikuwa hatuna bulk procurement system.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kwa sasa hivi Kanuni na Sheria wanazozitumia EWURA zimepitwa na wakati kwa sababu kwa mfano, ukienda mimi naomba ni-declare kwamba ni mdau wa Wizara, hii naji-declare kwamba EWURA wanapofanya vipimo vya vinasaba kwenye vituo, wamakuta wanaenda tofauti na sera za sasa hivi za Mheshimiwa Rais kwamba kazi iendelee wao wakifika wakikuta kuna tatizo kwenye kisima kimoja cha tenki wanafunga kituo kizima maana yake hawaendani na sera ya Mheshimiwa Rais ya kazi iendelee wao wanafanya kazi ifungwe.

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri hivi vituo kufungwa ni kero na wakati unakuta Mheshimiwa Waziri ni kwamba kwenye kituo umekuta kuna mafuta aina tatu, unakuta tatizo lipo kwenye tenki moja lakini unafunga kituo kizima, sasa kile kituo ukikifunga maana yake mfanyabiashara yule amewekeza, ana madeni ya benki ana wafanyakazi wanafanya kazi halafu zile faini ni kubwa. Zile faini ni kubwa sana kwa hiyo, mimi ningeshauri hizi Sheria na Kanuni ziangaliwe upya kwamba zitatusaidiaje.

Mheshimiwa Spika, jingine Mheshimiwa Waziri niseme kwenye suala la EWURA kuna suala la ki-technical wanafanyafaga kukagua Research Octane Number (RON) inatengenezwa kwenye refinery haitengenezwi kwenye depo wa la kwenye kituo RON inatoka kwenye kiwanda so wanakuja wanapima RON wakipima RON ni neno la kitaalamu unakuta RON haiko sawa, isipokuwa sawa unapigwa penati ya milioni saba, milioni 20, unafungiwa kituo.

Mheshimiwa Spika, hili suala la RON linatengenezwa kwenye refinery haitengenezwi Tanzania, sasa mtu mwenye kituo ana makosa gani kama RON iko tofauti? Maana yake wakati meli au wakati shehena imetoka kwenye refinery imekuja Dar es Salaam watu wa TBS wanaopima mafuta hayo wana makosa hawakufanya ukaguzi vizuri pale, yale mafuta yameshuka mpaka kwenye vituo, kwa hiyo mwenye depo hawezi kubadilisha RON, mwenye kituo hawezi kubadilisha RON.

Mheshimiwa Spika, RON inatengenezwa kwenye kiwanda, kwenye refinery. Kwa hiyo, mimi ningeshauri hizi kanuni na sheria za EWURA mziangalie upya zilianzishwa wakati hakuna bulk procurement, kazi wanafanya nzuri lakini sheria hizi ndiyo zimewabana.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu ndiyo huu tu ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nichangie hoja, ahsante sana. Naunga mkono hoja asilimia mia, ahsante. (Makofi)