Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Itifaki ya Biashara ya Huduma ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2012

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Itifaki ya Biashara ya Huduma ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2012

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye Itifaki hii ya biashara ya huduma ya SADC. Kabla ya kuanza mchango wangu, niungane na baadhi ya Wabunge ambao wamepongeza Wabunge wenzetu ambao wameteuliwa na Mheshimiwa Rais kwa nafasi mbalimbali ili kumsaidia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara na timu yake nzima akiwemo Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jinsi wanavyofanya kazi nzuri ya kuwaunganisha wafanyabiashara wetu. Nimeona mara nyingi akikutana na wafanyabiashara ili kuwaonesha fursa zilizopo na namna ambavyo wanaweza kushirikiana na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmoja kati ya ambao wameteuliwa na Mheshimiwa Rais ni aliyekuwa Mwenyekiti wetu wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mheshimiwa David Mwakiposa Kihenzile. Ninampongeza sana kwa sababu Mheshimiwa Rais amemuamini. Mwenyekiti wewe ni shahidi, Makamu Mwenyekiti alipowasilisha wasilisho na maoni ya Kamati aliwasilisha vizuri sana na mimi nachukua nafasi hii kumpongeza, ametuwakilisha vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, nachangia maeneo machache. Itifaki hii ikiridhiwa, soko la huduma litaongezeka kutoka hii ya kwetu ya shilingi milioni 61 kwenda shillingi milioni 360. Hili ni ongezeko kubwa na nasema tu kama Mheshimiwa Shangazi alivyotangulia kusema, sisi kwenye Kamati, tumeichakata, tumeangalia na tumeona kwamba kwa kweli ni fursa ambayo tumechelewa kuichukua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashawishi Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwamba Tanzania siyo wadhaifu tunapongia kwenye mjumuiko huu wa soko letu kutanuka. Mheshimiwa Shangazi amejaribu kueleza fursa ambayo tunayo na GDP yetu ni kubwa kwa maana ya watu ambao tunaweza kuwa na mashaka nao labda ni Afrika Kusini. Pia ukiangalia kwenye sekta ya huduma naona tupo nafasi nzuri zaidi. Nawashawishi Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwamba hii Itifaki tuiridhie na muhimu sana tujiandae vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo ya sekta ambayo tunaiangalia ni sekta ya ujenzi. Kwenye sekta hii ya ujenzi fursa zilizopo ndani ya nchi bado tunazitoa kwa wageni. Fursa itaongezeka maana yake yawezekana sisi Watanzania tusinufaike sana. Naiomba Serikali kwenye eneo hili tujaribu kuangalia namna ambavyo tunaweza kuwawezesha wataalam wetu wa ujenzi, makampuni ya ujenzi ili tuweze kupata fursa hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa iliyopo kwa watu wetu ni mitaji. Kingine ambacho kipo ni namna ambavyo makampuni ya kizawa yanahudumiwa ukilinganisha na wageni. Ukiangalia kwenye tendering process watu wetu wataambiwa kwamba wafanye kazi wa-rise certificate ndiyo wanapata malipo, wakati mwingine malipo hayaendi kwa wakati, kwa mantiki hiyo tuna-drain uchumi wao na tunawachelewesha watu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukitanua soko hili tuweze kunufaika, lazima tutengeneze mechanism ya kuwasaidia Watanzania kwanza kukamata soko hili la ndani pia kukamata soko hili tunalolitanua la nchi za Kusini mwa Afrika – SADC. Ukienda kwenye benki zetu, mtu ana mkataba wa kufanya kazi hata na Serikali ya Tanzania, mlolongo ni mrefu sana, utaratibu wa kupata mkopo ni mgumu, namna ya kuwawezesha lazima itafutwe ambayo ni rahisi ili hili soko tunalolitanua tunufaike nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye sekta ya fedha kutafuta mikopo, ajenda ya kwanza watakwambia kwamba watakuwa na valuer wao kama wewe una mali ambazo hazihamishiki, wa benki yenyewe. Valuers ninavyohamu huwa wanasajiliwa, valuer ambaye utapewa na benki atafanya assessment ya collateral, baada ya kufanya assessment atakuja na maneno mengi, mtaenda back and forth isiyopungua miezi minne mpaka na kuendelea. Tukienda na mwendo huu kwenye soko hili ambalo tunafungua, pamoja na strengths tulizonazo, hatutawasaidia Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara kazi yako ni kushamirisha biashara. Kazi kubwa uliyonayo mbele yako ni kukamata hili soko la watu miliono 360, ili tuweze kunufaika kwenye eneo hilo, kaa na Waziri wa Fedha ili kwenye sekta hii ya fedha, vikwazo ambavyo wanapata Watanzania viweze kuondolewa ili tuweze kunufaika na isije ikaonekana kwamba tumepata fursa lakini bado hatuna nafasi ya kuikamata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kwenye eneo la taarifa na Watanzania kujua fursa zilizopo. Kwenye eneo hili Mheshimiwa Waziri lazima ufanye kazi ya ziada, tembea na Watanzania, itazame Tanzania, angalia hali zao, kama unavyokuwa na mahitaji muhimu kwenye pochi yako, panga na hitaji la Watanzania, Serikali imuwezeshe Waziri wa Viwanda na Biashara kuwa na fedha za kufanya hamasa kwa Watanzania, kuwa na namna ya kuyafikia hayo masoko, kufanya maonesho maeneo mbalimbali kwa yale mazuri sisi tuliyonayo ili hatimaye hili soko tuweze kuliteka. Ni fursa kwetu, lazima tuchangamke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda na utendaji ule wa kawaida wa Kiserikali, haitatusaidia na tutakwama. Fursa iliyojitokeza lazima tuikamate, ni kweli tumechelewa. Ninachoomba tu, Serikali kwa maana hasa Wizara ya Viwanda na Biashara, jitoe kwenye ule mfumo wa kawaida wa urasimu wa Kiserikaliserikali. Jiweke kama wewe ni sehemu ya sekta binafsi, tembea na sekta binafsi kila sehemu ili hatimaye Watanzania tuweze kunufaika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania kwa sasa ukiangalia malalamiko mengi ambayo watu wetu wanayo si makubwa kwenye soko hili la Afrika Mashariki. Moja limeshasemwa kwamba kwenye mipaka ile zile blocks za kuwazuia watu, mfano madereva wa trucks, malalamiko yalikuwa ni mengi. Ninaamini kwa Itifaki hii tukishairidhia, yale malalamiko yote yataondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Kamati tumeona eneo hilo la sera zetu, sheria zetu, kanuni zetu za biashara lazima ziweze kufungua fursa tukimbie, tusitanguliwe na wenzetu. Lingine, kwa sababu Bunge hili ni chombo cha wananchi, niwaombe Watanzania wenzangu hii ni fursa tukimbizane nayo, tuwahi, tukichelewa tutakuta mwana si wa kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo tunapaswa tulirekebishe kabla hatujaenda mbali sana ni eneo la kodi. Kwa mfano, kwenye malori kwa sababu eneo la usafirishaji ni sehemu ya huduma, sisi Watanzania, mtu akishakuwa na lori mbili anaanza kulipia VAT, gharama zipo nyingi na kila lori ina EFD machine. Sasa tuangalie kama hizi changamoto ambazo tunazo na watu wa malori mara nyingi wamekuwa wakilalamika. Kama kwetu ipo, je, kwa wenzetu ipo hivyohivyo? Kwa sasa ukitembea barabarani utaona lori nyingi sana ambazo zimesajiliwa nchi jirani ndiyo zinazosafirisha mizigo kutoka bandarini kwetu zinaenda nchi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, hii changamoto, na wapo Watanzania ambao wameshasajili. Mtu ana lori kumi, lazima atafute jina la mtoto wake, ana Watoto wangapi, akasajili kwa marafiki ili angalau kuweza kumudu gharama. Wanalalamika sana gharama za uendeshaji, kodi ni kubwa. Tuangalie hizi changamoto na maeneo mengine, tukiweza kuyatibu na tukachangamkia, ninaamini fursa hii ni nzuri na itatusaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, niliona nichangie eneo hilo. Nakushukuru sana, ahsante. (Makofi)