Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Itifaki ya Biashara ya Huduma ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2012

Hon. Khalifa Mohammed Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Mtambwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Azimio la Bunge kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Itifaki ya Biashara ya Huduma ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2012

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kutoa mchango wangu katika mjadala uliopo hapa ama Azimio lililoletwa na Serikali. Pia napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuweza kunijalia afya nikaweza kusimama kwenye Bunge letu hili kuchangia Azimio hili ambalo limeletwa kwetu leo ili kuweza kuleta mustakabali wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Azimio lililopo leo ni Protocol of Trade in Service. Protocol hii ni kwa ajili ya nchi za Kusini mwa Afrika kuweza kushirikiana katika biashara ya huduma katika nchi hizi ambazo ni wanachama. Itifaki hii inalenga kuondoa vikwazo na masharti ya taratibu za huduma ya biashara katika nchi wanachama. Kwanza ningependa kuipongeza Serikali kwa kuleta Azimio hili kwa sababu linakuja kuleta maendeleo chanya kwa wananchi wetu ambao wanatoka katika Jumuiya hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mategemeo yetu Azimio hili litakuja kuisaidia nchi yetu baada ya kuridhiwa. Kwa nini nasema hivyo? Watanzania tumekuwa tukifanya biashara hizi kabla ya kuridhiwa Azimio hili, lakini tumekuwa tukifanya biashara kwa mashaka na vikwazo vingi bila kuweza kupata njia ya kutatua vile vikwazo, sasa muarobaini wa matatizo ya wafanyabiashara ya huduma unakuja kupatikana. Biashara hizi za huduma kama vile elimu, transport na mambo mengine, nchi yetu imekuwa ikipata changamoto nyingi, kwa hiyo sasa tukiridhia Azimio hili, changamoto hizi zitakuja kuondoka. Napenda kushauri mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukipata changamoto tukitumia zile certificates za Jumuiya hii bila ya kupata huduma stahiki kwa sababu tulikuwa hatujaridhia Azimio hili. Azimio hili wenzetu nchi wanachama walianza kuridhia mwaka 2022 ingawa lilisainiwa mwaka 2012. Kiukweli hatujachelewa kuridhia Azimio hili, ni kwamba tupo katika wakati mzuri na si vizuri katika jambo ukawa mtu wa kwanza ni bora kuchunguza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipongeza Serikali kwa kuchelewa kulileta Azimio hili kwa sababu ni lazima tuangalie kwamba wale wenzetu walioingia wamekutana na changamoto gani ili na sisi tuweze kujifunza kupitia kwao. Kwa hili, naipongeza Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye hoja ambazo nahisi zinahitaji kurekebishwa. Nchi yetu ya Tanzania imeingia mikataba mingine na nchi ambazo si wanachama wa Jumuiya hizi. Napenda Wizara yetu au Serikali yetu ikaliangalia hili tusije tukaathiri ile mikataba ambayo tumeingia na nchi nyingine tukashindwa kufanya nao biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, napendekeza nchi yetu ijikite kwenye kutoa hizi National ID na siyo nchi yetu tu, nchi wanachama zote ili kusiwe na mgongano kwa raia ambao hawahusiki ndani ya nchi hizi wanachama ama wakaenda kutoa huduma wakasema kwamba wanatoka katika nchi wanachama. Kama vile watu wanaoongea Kiswahili sana katika nchi ambazo siyo wanachama, wakaenda nchi nyingine wakasema wanatokea Tanzania. Kwa hivyo, suala la National ID ni muhimu sana ili liweze ku-facilitate mambo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine kama lilivyosemwa na Kamati yetu hapa, kuhusu Sera na Sheria zilizopitwa na wakati. Ni muhimu sana hili tuweze kulipitia, tukazitengeneza ili wananchi wetu wasiwe wana vikwazo kuingia kwenye soko hili la Jumuiya hii ya Nchi za Kusini mwa Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo jema. Tufanye haraka turekebishe sheria ambazo zimepitwa na wakati ili wananchi wetu waweze kuingia kwenye soko hili vizuri. Nchi yetu itoe elimu kwa wananchi wote kulifahamu Azimio hili ili waweze kuchangamkia fursa ambazo zipo katika katika hili Azimio. Hilo ni jambo kubwa sana kwa sababu wananchi wakati mwingine kama hawana uelewa, basi inaweza ikawa fursa hizi zikatumiwa na watu wengine kuja hapa kuwekeza wakati sisi tuna uwezo wa kwenda kuwekeza katika nchi ambazo tumeridhia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nilalopenda kuchangia ni suala la leseni za biashara. Leseni za biashara ziweze kutolewa katika masharti ambayo ni nafuu na kwa haraka na ikiwezekana kusiwe na mlolongo wa leseni. Leseni ya biashara iwe moja ili kuweza ku-facilitate kwa haraka ufanyaji wa biashara wa wananchi wetu katika nchi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto nyingi ambazo wananchi wetu wanakuwa wanazipata. Mfano, madereva wanavyokwenda nchi nyingine, wanakwama mipakani kwa sababu ya logistics nyingi ambazo zinafanyika pale, ukitoka Tanzania kuingia border nyingine. Napendekeza suala hili lifanywe kwa haraka, ianzishwe one stop center kwa nchi hizi za Jumuiya ili watu wanapokwenda au wafanyabiashara hawa wa ma-truck au wasafiri, wasikutane na changamoto hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakaribia mwisho wa mchango wangu, kuhusu suala la usimamizi wa sheria. Usimamizi wa sheria zetu inakuwa ni changamoto, kwa hiyo, hili napendekeza kwamba Serikali iwe makini katika usimamizi wa sheria ili kuona kwamba hii fursa haitumiwi na watu ambao siyo wanachama. Azimio hili linakuja lakini pia nchi mwananchama itazingatia sheria zake ilizojiwekea. Siyo kwamba watu wataingia tu kiholela kwa vile tupo kwenye Azimio, napendekeza nchi yetu, watendaji wasimamie sheria tulizoziweka ili kuepuka kupoteza haki zetu kwa sababu katika nchi yetu, nataka nitoe mfano. Mfano ni upande wa Zanzibar, mtu mgeni haruhusiwi kumiliki ardhi lakini sasa hivi ukienda Zanzibar, ukifanya utafiti, basi utakuta asilimia 25 – 30 ni wageni wanamiliki ardhi bila kufuata sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili ndilo nchi tunakwama kwa hiyo tunatakiwa tusimamie zile sheria zetu tunazojiwekea na kama hazifai basi tuziondoe, kama tunavyoshauri kwamba sheria zilizopitwa na wakati. Kwa sheria ambayo tunaona ina maslahi, isimamiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nataka kuchangia suala la lugha ya Kiswahili. Lugha ya Kiswahili original ni Tanzania. Lugha hii kwa nini isiwe ni moja ya tunu yetu? na kwa nini tusiisimamie dunia ikajua kwamba original ya lugha ya Kiswahili ni Tanzania. Hili, kwa sababu tumeridhia vitu kama hivi, kuna soko la Afrika pia linakuja, kwa nini tusijidadavue kuona kwamba lugha ya Kiswahili original yake ni hapa ili kuweza kutengeneza icon ya nchi yetu kwamba lugha ya Kiswahili inatoka hapa na tukaweza kupata mambo mengi ya ndani ya Azimio letu hili na dunia kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Bunge liridhie Azimio hili. Ahsante, nakushukuru. (Makofi)