Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Itifaki ya Biashara ya Huduma ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2012

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge kuhusu Mapendekezo ya Kuridhia Itifaki ya Biashara ya Huduma ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika ya Mwaka 2012

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa niweze kuchangia kuhusu hii Itifaki ya Biashara ya Huduma ya SADC. Awali ya yote niwapongeze sana Wabunge wenzetu na baadhi ya Mawaziri ambao wameteuliwa na wengine wamebadilishiwa nafasi zao. Tunawatakia kila la kheri wakati wa kula kiapo chao ili waje hapa Bungeni tufanye kazi za wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia soko la SADC tunazungumzia soko ambalo nchi yetu inauza bidhaa na huduma takriban zaidi ya shilingi trilioni 4.5 kwa mwaka. Kwa mfano, mwaka 2022, mauzo yetu katika nchi za SADC tumeuza zaidi ya shilingi trilioni 4.5. Kwa hiyo, unapoliendea soko la SADC unaliendea soko ambalo ni kubwa, soko ambalo tunalitegemea na ni soko ambalo ni la pili kwa ukubwa katika masoko ambayo tunayauzia bidhaa zetu ikitanguliwa na Asia na masoko mengine kama la East Africa, Europe, AGOA na masoko mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, soko la SADC ni soko kubwa ambalo tunapofikiria kufanya jambo lolote ni lazima tulifikirie kwa umakini mkubwa na tuhakikishe kwamba tuko vizuri. Tunapozungumzia hii Itifaki ya Biashara ya Huduma (Protocol on Trade in Service, 2012), kabla hatujakubaliana kuridhia ni lazima tupewe majawabu kwenye mambo fulani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, ni lazima tujiulize kwa nini Azimio hili tangu lisainiwe na Wakuu wa nchi mwaka 2012, leo ni miaka 11 halijawahi kuridhiwa? Sababu zilizosababisha lisiridhiwe kwa miaka yote hiyo 11 ni nini? Mazingira gani yalikuwepo, Azimio hili linazaliwa tarehe 18/08/2012, sasa mpaka leo miaka 11 ndiyo linaletwa hapa Bungeni, kwa nini? Kwa nini halikuletwa kabla?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua Dkt. Stergomena Lawrence Tax ambaye anatoka Tanzania ndiye aliyekuwa Katibu Mtendaji wa SADC toka mwaka 2013 mpaka 2022 na leo ni mwaka 2023. Wakati akiwa kule Azimio hili halikuwahi kuletwa Bungeni wala halikuwahi kuidhinishwa na Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais mstaafu wa Tanzania ambaye alisaini hii Itifaki mwaka 2012, amekaa madarakani miaka minne zaidi mpaka mwaka 2015, lakini hakuwahi kuleta hili Azimio ndani ya Bunge liridhiwe. Aliyelisaini hakuwahi kulileta hapa Bungeni liridhiwe, leo kwa nini linaletwa? Sababu za kuchelewa muda wote huo ni nini? Kama kulikuwa na kasoro za kurekebishwa mbona hatujaambiwa kama zimerekebishwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaletewa hili Azimio kuridhia lakini tuna SADC Protocol for Finance and Investment, tuna SADC Protocol on Trade, hizi protokali zote zipo. Hii protocal tunayotaka kuiridhia leo inaenda kutibu nini? Inaenda kuziba changamoto gani ambayo haipo katika protocol au katika Itifaki ambazo tumeshaziridhia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma ile Ibara ya 16(2) imezungumzia kwamba tunataka huduma ya biashara kwenye hizi sekta sita. Je, tunaenda kunufaika katika muktadha gani? Tunaenda kufanyaje, kwa mfano kwenye TEHAMA tunaenda kufanya nini na TEHAMA? Kwenye ujenzi tunaenda kufanya nini na ujenzi? Haijaelezwa kwa kina. Ukisoma taarifa ya Waziri mwenyewe anayewasilisha Itifaki hii, hata taarifa ya Kamati yenyewe huoni ni kwa muktadha gani na kwa namna gani tunakwenda kufanya hizi biashara ambazo sasa hivi tunashindwa kuzifanya kwa sababu hii Itifaki haipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haijaelezwa nchi tano ambazo mpaka sasa hivi hazijaridhia hili Azimio. Haijaelezwa kwa nini nchi tano kwa muda wa miaka 11 hazijaridhia hili Azimio. Lazima kuna tatizo, kwa nini halisemwi? Kama kulikuwa na tatizo na tuliliona kwamba ni tatizo, tumefanya marekebisho gani na kwa nini leo tunataka Bunge hili lishiriki kuridhia hili Azimio bila kuelezwa matatizo yaliyopo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 6(4) inazungumzia suala la CMT, Committee of Ministers Responsible for Trade, kuanzisha utaratibu wa kinidhamu. Mawaziri wanaoshughulika na viwanda na biashara wanapewa mamlaka ya kuweka utaratibu wa kinidhamu huku tukijua chini ya WTO utaratibu wa kinidhamu wa kibiashara wa pamoja umeshawekwa katika General Agreements on Trade and Service (GATS).

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu huu ulishawekwa, sasa hii duplication ya kuweka utaratibu mwingine inatoka wapi? Kama Mawaziri wakiruhusiwa wakaenda kutengeneza mkanganyiko, hatuoni kwamba tunaweza kusababisha Nchi za SADC kuwa kwenye migogoro muda wote, kusuluhisha matatizo kila leo? Kwa nini tusitumie zile general rules, zile general disciplines zilizowekwa kwenye GATS badala ya hao Mawaziri kupewa fursa ya kwenda kuandaa na kutengeneza utaratibu wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 8(2) imeweka sharti la mabadiliko yote ya sheria, kanuni na miongozo inayoathiri biashara ya huduma ya Nchi Wanachama kupeleka taarifa TNF Services yaani Trade Negotiation Forum Services. Takwa hili linaweza kutuletea matatizo makubwa, tunapotunga sheria zetu hasa zile domestic physical legislations ambazo katika nchi yetu hazitabiriki, mara nyingi tumekuwa tukianzisha tozo, faini, ada na ushuru mpya kila mwaka. Unaanzisha baadaye unafuta, baadaye unapunguza, baadaye unaondoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukifanya hivyo kila Mwaka wa Fedha ukifika, tunabadilisha sheria, tunaongeza tozo hii, tunapunguza tozo hii, tunasamehe ipi? Haya yote yamekuwa yanafanyika bila utafiti wowote na bila tathmini yoyote. Sasa kama kila mwaka tunaripoti kwa nchi zetu wanachama ambazo tunategemea soko kubwa sana kutoka kule SADC, tukiwa tunafanya hayo marekebisho kila mwaka, tunaweza kutengeneza mkanganyiko mkubwa sana na nchi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 16(2), tunaposema tunaenda kuingia kwenye huduma katika maeneo ya mawasiliano, fedha, ujenzi na usafirishaji tumejiandaaje ndani ya nchi? Mbona miradi mingi tuliyonayo sasa hivi hatuwapi wenzetu wa SADC? Hata miradi ambayo inaweza ikatekelezwa na wenzetu wa SADC mbona hatuwapi? Miradi ya TEHAMA mingapi tumeingia hapa na mikataba ya nchi za nje? Kwa mfano, Mradi wa CISCA ambao tungeweza kuutekeleza ndani ya Nchi zetu za SADC, Mradi wa TEHEMA wa TANESCO unatekelezwa na Mahindra Tech kazi ambayo ingeweza kufanywa na vijana wetu wa e-GA waka-develop huo mfumo, lakini tumewapa watu wa nje ya ukanda wa SADC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa leo tunapozungumza, tunaji-limit kabisa, tunaandika hapa, tunaruhusu mpaka kanuni za nidhamu ziwekwe. Mpaka tunaenda kuweka namna ya utatuzi wa migogoro kwa maana ya ile Annex one iliyowekwa katika Itifaki hii. Hivi tuna maandalizi gani wakati hata shughuli tulizonazo hivi sasa zote tunawapa watu wa nje ya ukanda? Tunafanya hivi kumfurahisha nani? Mbona hata maandalizi ya ndani ya kuridhia Itifaki hii hayapo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye ujenzi na uchukuzi, hata barabara fupi tu, za hela ndogo consultant anatoka Ulaya, consultant anatoka Asia. Hata kwa mambo ambayo tungeyafanya sisi ndani ya ukanda. Leo tunajifurahisha nini kusema kwamba tunaingia mkataba huu wakati hata miradi ambayo naizungumza tumefunga mikataba nje ya ukanda, wakati Itifaki hii Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete alisaini toka mwaka 2012, kuna marekebisho gani toka kusainiwa kwa Itifaki hii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia ushirikiano wa fedha wa sekta ya fedha. Sekta ya fedha nchini hapa na hata SADC wote tunategemea Dola. Sasa hivi Dola hakuna, Dola zimeadimika, wafanyabiashara hawapati Dola, hivyo hawawezi kuagiza mizigo, tunafanyaje? Maelezo yanayotolewa na Serikali, uwekezaji umeongezeka ndani ya nchi maradufu, watalii wameongezeka nchini maradufu, Dola zimeenda wapi kama uwekezaji, utalii na mauzo ya nje yameongezeka?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Luhaga Mpina, malizia sentensi moja ya mwisho.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nahitimisha kwa kusema kwamba, Serikali ni lazima itatue tatizo la kuadimika kwa dola na hasa ninavyoona sababu ambayo haizungumzwi ni suala la ufisadi mkubwa ulioripotiwa na FIU kwa kuonyesha miamala shuku ya zaidi ya shilingi trilioni 280. Inawekana dola zetu zimetoroshwa kupitia mipakani na kwenye benki na leo nchi haina dola.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, kwa maelezo haya niliyoyatoa ambayo sikuweza kuyasema yote, nasema kwamba siwezi kuridhia Azimio hili na nalishauri Bunge kwamba lisiridhie hii Itifaki kwanza unless tupate maelezo ya kina ya Waziri nini kilichosababisha miaka 11 Itifaki hii haikuridhiwa.