Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu huyu aliyenijalia afya na nguvu kuweza kusimama katika jengo lako hili Tukufu. Pia niwashukuru wananchi wangu wa Lushoto kwa kuniamini ili nije niwawakilishe katika jengo lako hili tukufu. Niendelee kumpongeza Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na timu yake ya Mawaziri, aendelee kutumbua majipu na sisi Wabunge tutaendelea kuyapaka spirit ili yakauke haraka siku ya siku tuyapeleke mahakamani majibu haya ili wakome kuita nchi hii ni shamba la bibi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuwashukuru Mawaziri wangu wawili Mheshimiwa Angellah Kairuki na Mheshimiwa George Simbachawene. Pia niendelee kuwapongeza ndugu zangu wapinzani maana leo naona wameanza kuchangia hoja, wamebakisha tu kusema naunga mkono hoja, lakini kwa uwezo wa Mungu naamini itafikia hatua hiyo sasa naona roho mtakatifu amewashukia leo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mchangiaji mmoja dada yangu Mheshimiwa Grace Kiwelu alisema kwamba tufute mbio za mwenge. Kufuta mbio za mwenge ni sawasawa na kufuta historia ya nchi, hiyo haitawezekana. Kama isivyowezekana kwa CHADEMA kufuta historia ya Edwin Mtei ndani ya CHADEMA. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuchangia hoja sasa. Niishauri Serikali iendelee kuanzisha vijiji, kata, Halmashauri, wilaya hadi mikoa kwani hii inapelekea kupeleka huduma karibu na wananchi. Historia ya Jimbo la Lushoto au Wilaya ya Lushoto kwa kweli ni kubwa sana na Rais wetu Mstaafu wa Awamu ya Nne alivyotembelea Lushoto alituahidi Halmashauri ya Mji wa Lushoto na Mlalo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, unapoongea juu juu hivi mtu huwezi ukaamini kwamba Wilaya ya Lushoto ni kubwa sana. Nataka niseme ili ujue uhondo wa ngoma uingie ucheze, namuomba Mheshimiwa Waziri wangu Simbachawene atembelee Lushoto ili tunapoongea maneno haya tuwe tunamaanisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Lushoto inapakana na Kenya. Kuna watu wanatoka kwa miguu kufuata huduma Wilayani Lushoto inashindikana wanatumia siku mbili. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu sasa ituangalie kwa jicho la huruma ili kwenye bajeti hii ya 2016/2017 iweze kutupatia Halmashauri ya Mji na iweze kutupatia Halmashauri ya Mlalo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye afya. Suala la vituo vya afya ni tatizo la nchi nzima na naamini Serikali yangu sikivu imejiandaa vyema kuweza kujenga vituo hivi vya afya. Pamoja na hayo kwenye mpango huo naomba sasa Waziri, Mheshimiwa Simbachawene tuangalie Lushoto kwa sababu Jimbo la Lushoto lina kituo cha afya kimoja na zahanati nane. Kwa hiyo, huduma hii ya watu wa Lushoto kwa kweli imekuwa na hali ngumu kiasi kwamba kwa kweli inatia masikitiko. Kituo hiki kiko sehemu moja inaitwa Mlola, kutoka sehemu moja wanaita Makanya kwenda Mlola kwanza hata miundombinu ya barabara hakuna, wananchi wa kule wanapata taabu sana.
Hawa wananchi ni wapiga kura wetu tunawategemea, hawa hawayumbi wala hawayumbishwi, hawajui CHADEMA wanajua tu CCM. Kwa hiyo, nikuombe Waziri wangu katika bajeti ya mwaka 2016/2017 hebu liangalie hilo tuweze kuongeza vituo vya afya. (Makofi)
MHE. JAMES K. MILLYA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa....
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, naomba unilindie muda wangu kwani mtoa taarifa, taarifa hiyo nadhani hajajielewa aipeleke Simanjiro lakini Lushoto ni kijani tupu. (Makofi)
MBUNGE FULANI: Ulipata asilimia mia?
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Ndiyo ni asilimia mia.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naongelea suala zima la afya. Kwa kuwa Serikali yetu ina mpango mzuri wa kujenga vituo vya afya katika Jimbo la Lushoto, niiombe sasa isimamie hawa watu wa MSD kwani dawa hazifiki kwa wakati. Nimechunguza kweli hawa watu wa MSD ni majipu kwani DMO anapeleka pesa za kununulia dawa labda shilingi milioni tano lakini akifika anapewa dawa za shilingi milioni mbili. Kwa hiyo, hili ni jipu naomba lifuatiliwe. Sisi tunalalamikia madaktari wetu kumbe kuna kidudu mtu hapa katikati anakwamisha huduma nzima ya wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye suala la kilimo. Uti wa mgongo wa Taifa hili ni kilimo lakini huachi kuongelea pia na miundombinu. Miundombinu ya barabara ndani ya Jimbo la Lushoto hasa za vijijini ni tatizo. Wananchi walio wengi hususan wakulima wanakwamisha na miundombinu ya barabara. Kwa hiyo, niishauri Serikali yangu tukufu kwamba katika bajeti hii ya 2016/2017 ipeleke pesa za ruzuku za kutosha katika Halmashauri ili barabara hizi ziweze kutengenezwa kiwango cha kupitika ndani ya mwaka mzima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hayo kuna barabara za vijiji ambazo ni tegemezi hata katika Jiji la Dar es Salaam, barabara hii ni ya Mshizihii - Boheloi, inatoa mazao mengi sana. Barabara nyingine ni ya Kwemakame - Ntambwe - Mazumbai - Baga kwa Mheshimiwa January.
Kwa hiyo, hizi ni barabara ambazo zinatoa matunda na mazao mengi sana. Pia kuna barabara inatoka Malibwi – Kwekanga - Kilole - Ngwelo ni ya muhimu sana kwani inachangia pato kubwa la Taifa hili.
Barabara nyingine ni ile inayoingilia sehemu moja wanaita Kwaikileti – Dindira – Bandi – Kwaboli – Migambo. Barabara hii inatoa matunda mengi mno kiasi kwamba hata tukielezea uchumi wa matunda ya Lushoto basi chanzo chake kinatoka maeneo hayo niliyotaja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuzungumzia suala zima la redio ya Taifa (TBC). Nimuombe Mheshimiwa kaka yangu Mheshimiwa Nape, kule kwetu tunasikiliza redio za Kenya tu. Kwa hiyo, ifikie hatua sasa kwenye bajeti hii ya mwaka 2016/2017 basi watutengee mafungu ili wananchi wale waweze kupata taarifa mbalimbali za Taifa lao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naona muda wangu umeisha, naunga mkono hoja asilimia mia.