Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Grace Sindato Kiwelu

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia bajeti hii ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Utawala Bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, Utawala Bora ni pamoja na watu kupata habari na kujua wawakilishi wao waliowachagua wanawawakilisha vipi ndani ya Bunge, lakini Bunge letu leo limekuwa ni Bunge la kujifungia ndani, tumefunga milango, tumefunga madirisha, hatutaki wananchi ambao tuliwaomba kura kwa unyenyekevu mkubwa, wengine walipiga magoti, wengine walipiga pushapu, ili mradi tupate kura, lakini leo hamtaki kuwapa nafasi wananchi wasikie mnachokisema.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakuomba sana, Bunge letu liendelee na ule utaratibu wa zamani. Huko nje wananchi wanalalamika kwa sababu bajeti tunayoipitisha hapa ni kodi zao, lakini leo tunajifungia hatutaki wasikie, ni aibu!
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kidogo kuhusu mwenge. Kama kuna kitu kinachonikera ni suala la kukimbiza mwenge mchana. Wabunge wa Upinzani tulishasema, kuhusu sherehe zinazoadhimishwa na Serikali, lakini mlitucheka, leo zipo baadhi zimesitishwa. Namwomba Mheshimiwa Rais kama alivyoacha kusherehekea hizo sherehe nyingine ambazo ni za muhimu kama Uhuru na Muungano, tuachane na biashara ya kukimbiza mwenge mchana.
Mheshimiwa Naibu Spika, zinatengwa bajeti kwenye Halmashauri zetu, leo kila Mbunge analalamika mafuriko kwenye maeneo yake watu wanakimbiza mwenge, watu wetu wanakufa hawana maji safi na salama, hawana dawa, madaraja yamebebwa na maji, hakuna barabara, tunakimbizana na mwenge, hii ni aibu! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana kama ni kazi ya mwenge naamini imetosha, maana yake siamini kama hata hao mafisadi, hauna tija kwa sasa pamoja na kumulikwa kila mwaka, lakini ufisadi bado upo pale pale. Naomba sana hizi fedha zinazotengwa kwa ajili ya kukimbiza mwenge tuzipeleke kwenye shughuli za maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee suala la upotevu wa pesa katika Halmashauri zetu. Katika Manispaa ya Moshi Mjini kulitokea ubadhirifu wa shilingi milioni 90 kutoka kwenye Basket Fund na suala hili TAKUKURU waliliingilia, wakachunguza na wakagundua baadhi ya watumishi waliziiba fedha hizi na wakawashauri wale watumishi warudishe fedha hizi na mpaka sasa inasemekana zimesharudishwa shilingi milioni 70.
Swali langu ni kwa nini TAKUKURU pamoja na nia njema waliyoonyesha na kazi nzuri waliyofanya, maana wamewaomba warudishe fedha na zimerudi, ni kwa nini sasa TAKUKURU hailipeleki suala hili mahakamani ili wale wote walioshiriki kwenye suala hili wakachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria na taratibu zetu za nchi?
Mheshimiwa Naibu Spika, tukiliacha hivi TAKUKURU wakiendelea kumalizana ofisini fedha za walipa kodi zitaendelea kupotea na tukizingatia zaidi ya 70% ya fedha tunazopitisha hapa zinakwenda kwenye Halmashauri. Fedha hizo zingekuwa zinafanya kazi inayotakiwa leo wananchi wetu vilio walivyonavyo vingepungua. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Simbachawene, Waziri wa TAMISEMI, suala hili mlifuatilie na wale watumishi mhakikishe wanafikishwa mahakamani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala lingine niungane na Mheshimiwa Waziri (TAMISEMI) kuhusu uongezaji wa mapato katika Halmashauri zetu. Halmashauri zetu hasa mapato ya ndani yamekuwa ni kidogo sana na hii inatokana na wale wazabuni tunaowapa tender hawawi wa kweli, wanaziibia Halmashauri zetu. Wengi wamekuwa wakitumia vitabu viwili na kuleta yale mapato madogo katika Halmashauri zetu na kusababishia Halmashauri zetu kushindwa kujiendesha na kukosa yale mapato ya ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitolee mfano Halmashauri yetu ya Siha, yupo mzabuni mmoja, niiseme hii kwa sababu watumishi wamekuwa wakianzisha kampuni zao na wamekuwa wakijipa tender wenyewe na suala hili linasababisha sana Halmashauri zetu kushindwa kuendelea. Halmashauri yetu ya Siha yupo mzabuni mmoja amepewa zaidi ya zabuni tano na mpaka sasa anadaiwa zaidi ya shilingi milioni 56 hajaweza kuzileta katika Halmashauri yetu. Nimeona kwenye magazeti juzi wanasema Halmashauri ya Siha tusipoweza kukusanya itafutwa, lakini wanaoturudisha nyuma ni wazabuni kama hawa. Niombe Mheshimiwa Waziri tufuatilie na wale watumishi wote watakaogundulika kwamba wana kampuni ambazo wamejipa bila kufuata taratibu waweze kuchukuliwa hatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la elimu. Mzungumzaji aliyemaliza kuongea alisema siku ya wanawake duniani tulitembelea maeneo mbalimbali kwenda kusherehekea sikukuu ya wanawake duniani. Mimi nilibahatika kwenda katika shule ya watoto wenye ulemavu iliyopo Njia Panda, Jimbo la Vunjo. Shule ile ina wanafunzi 69 wasiosikia, wana matatizo makubwa sana, ina walimu 11 lakini ina watumishi watatu, matroni na mlinzi hawa bado hawajaajiriwa. Ukizingatia kauli ya elimu bure, awali wazazi walikuwa wanachangia kwa kuwaandikia lakini leo mwalimu mkuu wa shule ile hawezi kuandika kwa sababu anaogopa kufukuzwa kazi. Matroni na mlinzi hawajalipwa mshahara huu ni mwezi wa nne. Hata kutoa huduma ndogo ndogo kama matengenezo ya vitasa, kununua vitabu, toka Januari mpaka sasa wamepata capitation shilingi 25,000 tu, hii ni aibu. Mheshimiwa Waziri umeonesha hapa shule tulizonazo, nilitegemea ungetuonesha tuna shule ngapi za watoto wenye ulemavu kwa sababu tunahitaji watoto wetu wapate elimu na najua shule za watoto wenye ulemavu zina mahitaji zaidi ya hawa watoto wengine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, shule ile inahitaji mambo mengi mfano na pia ukarabati haina uzio. Pia walikuwa na kilio kwamba wanahitaji kupata shule ya sekondari kwa sababu watoto wanaotoka pale wakifaulu, wakipelekwa kwenye shule hizi nyingine kuendelea na masomo hawapati walimu wenye lugha ya alama. Kwa hiyo, uelewa wao unakuwa ni mdogo wakifika form two wanarudi nyumbani. Wanasema wanalo eneo kubwa pale, wanaomba sana ile shule iendelezwe mpaka sekondari ili watoto wetu pamoja na ulemavu lakini akili wanazo, wanao uwezo wa kusoma, tukiwapa mahitaji yao na tukatekeleza mahitaji yao, naamini watakwenda kuwa viongozi wazuri katika nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine nizungumzie suala la posho za Madiwani, Wenyeviti wa Mitaa, Vijiji na Vitongoji. Leo tuko Bungeni tunayo maafa kwenye maeneo tunayotoka lakini wanaowajibika ni hawa Madiwani, Wenyeviti wa Vijiji na Mitaa. Tunaiomba sana Serikali hii ya Hapa Kazi Tu basi watazameni hawa, wanafanya kazi ngumu. Likitokea janga wa kwanza kugongewa ni Diwani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.