Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Khatib Said Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Konde

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Namshukuru Mwenyezi Mungu pekee kwanza dakika zenyewe ni tano.
MWENYEKITI: Mheshimiwa khatib dakika tano.
MHE. KHATIB SAID HAJI: Ahsante.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa haya yanayotukuta hapa Bungeni, nimshukuru Mungu kwa kila linalotukuta. Leo nimesikitishwa sana na kilichotokea kwa njia yote ile iliyosababisha hotuba yetu ya Kambi ya Upinzani kufanya isisomwe hapa ndani ya Bunge imenisikitisha sana. Lakini nataka nikuambie tu kwamba, mmejaribu kufunga banda farasi ameshatoka. Watanzania wanaelewa kila kilichomo kwenye hotuba ile, taarifa ziko na wote wanajua ni nini, ujumbe gani umekusudia kuwafika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili niwashukuru wananchi wa Pemba hususani wa Jimbo langu la Konde kwa mapokezi makubwa waliompa kipenzi chao, Maalim Seif Sharif Hamad, jana katika ziara yake aliyofanya kule Pemba. Sasa mapokezi yale ni ishara tosha kwamba, hakika Wazanzibari nyoyo zao ziko na Maalim Seif. Kilicho chema ni chema hakibadili tabia, ni bure mngekisema na mengi kukizulia, Mungu hukipa baraka na amani kukitia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo baada ya tukio la kuzuiliwa hotuba, nilimuuliza, ninaye mtabiri wangu wa nyota na mtabiri wa ndoto, nikamuuliza hatua ya mwanzo ndani ya Bunge yamezuiliwa matangazo live ya TV, wananchi wasione tunachokisema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea, leo tayari tumezuiliwa hotuba yetu isisomwe ndani ya Bunge nikamuuliza what is next? Jibu aliloniletea muda mfupi ananiambia kinachoendelea baada ya kuweka dole mtawekewa vibakuli vya gundi wapinzani tutatia gundi ndi! Tukiingia hapa kimya. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni wajibu wetu kuona tunakoelekezwa kwenda, tuna hiari sasa kuamua kukubali kila tunalofanyiwa na wenzetu kwa sababu ya wingi wao au kuangalia ni hatua gani madhubuti tunachukua tukatae dhuluma yote ndani ya Bunge hili. Tukatae kunyamazishwa kwa namna yoyote sauti yetu hata humu ndani pia zisisikike, tukatae kabisa na tukatae. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka kuzungumzia suala moja ambalo linaendelea. Jeshi la Polisi, nimekereka sana na kitendo chao cha kuwashikilia watu zaidi ya muda wa kisheria ambao wanatakiwa kuwa-hold katika vituo vya polisi. Hili limesemewa na mimi nalisemea na linaniuma sana, kwa sababu ukiacha hilo kule Zanzibar, Jeshi la Polisi linatumika sana kisiasa, anaweza kutokea tu Mkuu wa Mkoa akasema wakamate hao weka ndani na wanafanya hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siku kumi hili linaniumiza sana, nalisema sana. Siku kumi kabla ya uchaguzi haramu wa marudio Zanzibar, wananchi wangu wa Jimbo la Konde wasiopungua 30 walizuiliwa katika vituo vya polisi katika muda usiozidi siku 14, wakapelekwa mahakamani, mahakama wakasema hatuoni kesi hawa ya kuwafungulia tulichotegemea kirudishwe vituo vya polisi watapewa dhamana, matokeo yake imetoka amri kutoka hatujui wapi, wanaambiwa endeleeni kuwashikilia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumuuliza Waziri wa Mambo ya Ndani, ni yeye, ni Naibu wake au ni nani anayesimamia amri hii haramu ifanyike kwa wananchi wangu. Leo akija hapa Mheshimiwa Waziri mimi na yeye na mshahara wake mpaka tujue nani anayetoa amri haramu ya kuwazuia wananchi zaidi ya muda wa kisheria unaotakiwa uwe nao au uwe umewapeleka mahakamani kwa hatua za mbele zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashindwa sana, hapa alinyanyuka, katika moja ya maneno mabaya aliyowahi kusema kiongozi mmoja mwandamizi wa CCM ambaye sasa hivi ni Waziri, ni pale alipotamka katika mmoja wa mkutano wake akiwa ndani ya kanisa kwamba, tatizo la Zanzibar ni Uislamu, Mheshimiwa Lukuvi, alisema hayo maneno, nataka niseme tatizo la Zanzibar sio Uislamu.