Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami nianze moja kwa moja kwa kumpongeza sana Waziri wetu wa Kilimo Mheshimiwa Hussein Bashe na Naibu Waziri Mheshimiwa Antony Mavunde pamoja na Watendaji wote wa Wizara ya Kilimo kwa kazi nzuri wanayoifanya. Watendaji hawa ni watu wenye busara kubwa sana wamekwenda kwenye meza ya majadiliano, wamekaa na Wizara ya fedha na wadau wengine wa maendeleo, wakashawishi mpaka bajeti ya kilimo ikaongezeka kutoka Shilingi 294,000,000,000 hadi Shilingi 751,000,000,000 sawa na ongezeko la takribani asilimia 155 na hii ni 1.8 percent ya bajeti yote ya Taifa, hongereni sana Waziri na wenzako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza Wabunge wote, Wabunge wote huku ndani tulipiga kelele kwamba bajeti iongezeke na kwa namna ya pekee pia nimpongeze na kumshukuru Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kwa kusikiliza kilio cha Wabunge wote na kwa sababu tumeona kabisa alikuwa na nia nzuri na bajeti imeongezeka, tunashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado naendelea kuishauri Serikali kwamba tukienda na Azimio la Malabo tulitakiwa tuwe na angalau asilimia 10 ya Bajeti ya Taifa iende kwenye kilimo lakini hii 1.8 ni bado tungefurahi sana 4.1 trillion ambayo ndiyo asilimia 10 kufuatana na Azimio la Malabo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninaendelea kusema kwamba bado ni muhimu Serikali iongeze hii bajeti kwasababu Kilimo kinaajiri asilimia 65 ya Watanzania wote, kilimo kinachangia asilimia 27 kwenye Pato la Taifa, kilimo kinachangia asilimia 25 ya fedha za kigeni, kilimo kinatulisha watu wote nchi hii. Kwa hiyo naomba sana Serikali ifikirie kuongeza hii bajeti kama walivyokubaliana Marais kwenye lile Azimio la Malabo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utakuwa kwenye maeneo matatu ambayo ni suala la mbolea, maparachichi na nitaongelea changamoto za Jimboni kwangu ikishindikana nitaishia nitakapoishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyofahamu kitunguu na nyanya ilivyo ni muhimu sana katika kukaanga chakula na kuandaa chakula kizuri, mbolea ni component muhimu sana kwenye kuongeza tija uzalishaji kwenye Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika msimu uliopita wote tumeona kwamba bei za mbolea zilikuwa kubwa kidogo, Wabunge wengi wamesema zilipanda kutoka Shilingi 50,000 kwa mfuko wa kilo 50 hadi kufikia Shilingi 150,000 kwenye baadhi ya maeneo, hili lilikuwa ongezeka kubwa kusema kweli karibia asilimia 200 ya nyongeza ya bei ya mbolea. Wakulima wengi walishindwa kununua mbolea na msimu huu hali ya kilimo sidhani kama itakuwa kama tulivyozoea kwasababu ya wakulima wengi watakuwa wamekwazika kwenye bei ya mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu zipo sababu ni nyingi ambazo zimesababisha mbolea ikapanda bei, tunaona kule China waliweka lock down na Urusi wana vikwazo vya uchumi kwasababu ya vita wanavyopigana na Ukraine kwa hiyo vitu vingine ni nje ya uwezo wetu na hii imesababishia bei ya mbolea katika soko la dunia ikapanda na hata hapa Tanzania sisi hatujawa insolated tuna-face the same problem. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo pamoja na kwamba tuna matatizo lakini kama nchi ninashauri Serikali lazima ifanye vitu fulani ili tuondokane na hii changamoto. Ushauri wangu wa kwanza kwa Serikali Waziri katika hotuba yake amesema wana-plan kuwasiliana na Wizara ya Nishati ili kile kiwanda cha kutengeneza urea kiwepo, hili ni jambo muhimu sana. Kama intercom wame-invest Dola Bilioni 180 wakaweka kiwanda, jamani mbolea ni suala la usalama wa Taifa letu. Kama hakuna chakula hakuna usalama hapa, mimi ninaishauri Serikali kabisa kwa nia nzuri wakae chini waangalie namna ya ku-invest, gesi yetu ya asili tunayo tutumie ile gesi tutengeneze mbolea yetu wenyewe ili tujihakikishie usalama wa chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi kama China huwa zina-plan wanaweza wakawekeza hapa au tukanunua kutoka China tukatengeneza mbolea yetu wenyewe, kwa hiyo ushauri wangu wa kwanza kwa Serikali ni kuwekeza kwenye kutengeneza mbolea yetu wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa pili, ninaishauri Serikali ihamasishe Vyama vya Ushirika wanunue mbolea kwa pamoja, (bulk procurement) kwa kufanya hivyo tutapunguza gharama za kuingiza mbolea nchini na bei inaweza ikashuka ikawa afadhali kidogo, tunaona kule kwenye Tumbaku wanafanya hivyo na mambo yanakwenda vizuri. Ushauri wangu wa tatu ni kuishauri Serikali ikiwezekana watoe bei elekezi ya mbolea ili kila mtu asiwe anajipangia tu bei ya mbolea lakini tuwe na bei elekezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa Nne ni kuishauri Serikali ikiwezekana kupitia utafiti tuwahamasishe wakulima wetu watumie mbolea za asili ili wale ambao hawataweza kununua mbolea watumie mbolea za samadi, mboji na kadhalika. Na ushauri wa mwisho kwenye hili suala la mbolea ni…

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MWENYEKITI: Mheshimiwa Cherehani taarifa.

T A A R I F A

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ninampa taarifa mzungumzaji kwamba kwenye upande wa tumbaku tunao umoja wa wakulima wa Tumbaku unaitwa TSJE ndio maana tunanunua mbolea kwa mfumo wa Pamoja, basi tungeomba na mazao mengine waweze kuunganisha umoja wao ili waweze kuagiza mbolea kwa pamoja na bei inapungua, ahsante sana.

MWENYEKITI: Unaipokea taarifa hiyo Mheshimiwa Profesa.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea kwa moyo mmoja. Ushauri wangu wa mwisho ni kuishauri Serikali ikiwezekana wakae wapunguze tozo ambazo siyo muhimu kwa wakati huu. Kwa mfano, tozo za ushuru za usafirishaji na uingizaji wa mbolea zikipunguzwa zinaweza zikatoa nafuu kwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili ni kwenye zao la Maparachichi. Kama tulivyosikia watu wengi wanazungumzia maparachichi yanalimwa kwenye maeneo mengi hapa nchini, hii ni hanging fruits tukiitumia hii fursa vizuri ile target ya Mheshimiwa Waziri ya kuhakikisha kwamba mboga mboga na matunda yanachangia Dola Bilioni Mbili kwenye Pato la Taifa tutaifikia vizuri. Kwa hiyo ninaendelea kuishauri Serikali isimamie na isukume wahakikishe kwamba angalau tunaunda vikundi vya kupanda parachichi pamoja, wauze pamoja, tuvune pamoja ili tuweze kulijaza soko na kwa kufanya hivyo nawaomba wananchi wangu kwenye Jimbo la Moshi vijijini maeneo ya Uru, Old Moshi, Kibosho, mpaka Mabogini kule, tuingie kwenye hii biashara kwasababu Waziri ameshasema hapa kwamba kuna miche 20,000 atakayotoa ili na sisi tunufaike na hili jambo lenye heri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni changamoto kwenye Jimbo langu. Mheshimiwa Waziri tuna changamoto ya miche ya kahawa, wachaga kule sasa hivi tumechacharika tunataka kupanda kahawa tuchangie kwenye Pato la Taifa, kwa hiyo nikuombe ile miche ambayo unatoa usitusahau. Kuna maeneo yangu ya Uru, Kibosho na Old Moshi tupo tayari kulima kahawa na ndizi, ile miche utakayoleta tunaomba utusaidie ili na sisi tuchangie kwenye Pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili ni miundombinu ya …

MWENYEKITI: Mheshimiwa Profesa Ndakidemi nilikuongeza muda wako umalizie changamoto za Jimboni, naona umeshaielezea vizuri au kuna kitu unadhani umekisahau.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia.

MWENYEKITI: Sawa.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mifereji ya asili na miundombinu ya umwagiliaji tuna eneo kama hekta 4,060 kwenye eneo la Mabogini, Arusha Chini, na Mandagamnono kwa hiyo tukiboreshewa mifereji ya asili na miundombinu ya umwagiliaji tutachangia vya kutosha katika Pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)