Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa jioni hii kuchangia Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, naomba nimshukuru Rais wetu wa Awamu ya Sita kwa busara na hekima ya kuwagawia wakulima wetu wa korosho pembejeo bure, kitu ambacho kimesababisha katika Wilaya yetu ya Tunduru kuongezeka kwa uzalishaji kutoka tani 14,000 mpaka kufika tani 25,000. Tunashukuru sana, lakini kipekee tumshukuru Waziri, tulipompa wazo hili kwa kweli alilichukua, akalibeba, akamshirikisha Rais, akakubali matokeo yake jambo hili likatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kutekelezeka kwa jambo hili, kuna jambo naomba Waziri unisikilize kwa umakini. Utaratibu wa ugawaji umekuwa tatizo katika vijiji vyetu. Ugawaji uliotumika msimu uliopita walipewa mamlaka watu wa ushirika peke yake na matokeo yake malalamiko yamekuwa mengi kwa wakulima, kwani wale waliofaa kupewa pembejeo hawakupewa. Kwa hiyo, naomba sana safari hii ugawaji huu ushirikishe Serikali za Vijiji, Serikali za Kata, muunde tume, kamati kwenye vijiji na ikiwezekana basi wale wanufaika watakaopata pembejeo zile basi wapitishwe na Mkutano Mkuu wa Vijiji ili kila mmoja ajue ni nani amenufaika na ikiwezekana mbandike wale wanufaika kwenye mbao za matangazo kila kijiji ili ionekane namna ambavyo pembejeo zile zimegaiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, jambo hili ni muhimu ili kuondoa lawama ambazo zimetapakaa katika vijiji vyetu kwa namna ambavyo hatukutenda haki katika kugawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, hili suala la pembejeo lipo kwenye jambo letu lile la Export Levy. Nakuomba Waziri, sikusikia jambo la Export Levy kulirudisha kama wadau walivyokuwa wamekubaliana. Wewe unafahamu Export Levy ilianzishwa na wadau wa zao la korosho ili kulifanya zao hili lifanye kazi vizuri, lihudumiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unafahamu mara ya mwisho tumeondoa Export Levy, uzalishaji ulipaa na ukaja kushuka baada ya kuondoka mpaka kufikia asilimia 33. Ili pembejeo tuweze kugawa bure, ni sehemu ya Export Levy. Kwa sasa Export Levy minimum ni Dola 160 kwa tani, kwa maana ya kilo moja shilingi 372/= ni Export Levy ambayo inakwenda Serikalini. Tunaomba Sheria ile ya asilimia 65 irudi kuhudumia zao la korosho. Hata wakulima sasa hawataweza kukatwa ile shilingi 50/=; shilingi 25/= ya kuhudumia Bodi ya Korosho na shilingi 25/= ya kuhudumia utafiti, itatokana na ile Export Levy na mambo mengine yatakwenda vizuri. Naomba sana hii Sheria tusiisahau, tuirudishe, tufanye kazi iliyokusudiwa na wadau kwa ajili ya kuhudumia zao la korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, Mheshimiwa Waziri nikushukuru sana kwa kumteua Mrajisi wa Ushirika ambaye ana moyo wa kuusaidia Ushirika. Ushirika ndiyo kiini pekee cha kuweza kumsaidia mkulima, lakini Ushirika huu unakwamishwa na watu wa chini, kwa maana Mrajisi na Head Office wana nia nzuri ya kuwasaidia wakulima, lakini watendaji walioko chini, kwa kweli imekuwa ni tatizo. Nadhani mara ya mwisho nilikwambia yaliyotokea Tunduru, kuna wadau walikubaliana kuchangia Timu ya Tunduru korosho kupitia tozo kwenye Vyama vya Msingi, ambapo kila Chama cha Msingi kinachangia Shilingi 2/= kwa kila uzalishaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TAMCO nao Chama Kikuu kinachangia shilingi 2/=, wasafirishaji wa korosho wanachangia shilingi 2/= lakini mtunza ghala anachangia shilingi 1/=. Kwa bahati mbaya, ndiyo maana nazungumza kwamba watendaji walioko chini, hawaisaidii Serikali kwa maana ya Tume ya Ushirika kufanya kazi vizuri kwa maendeleo ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile hesabu inayokusanywa kwenye Vyama vya Msingi, kwenye Chama Kikuu haioneshi mahali popote kwenye hesabu zao za vitabu. Kwa maana hiyo, ni kwamba kama haioneshi kwenye hesabu zao na ile hesabu haipelekwi kwa wananchi wakajua kwamba Chama chetu cha Msingi kimechangia kiasi kadhaa kwa ajili ya maendeleo ya michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri uende ukakague Vyama vile vya Msingi kuona fedha hii inakwenda wapi? Kule inakokwenda haifanyiwi hesabu ya aina yoyote. Sasa hivi huu ni msimu wa nne, wamekusanya lakini haioneshi kwenye vitabu vyao, wala hawasomi hesabu kwa wanachama wao kuonesha fedha hii inachangwa na imepelekwa kwenye michezo. Naomba sana jambo hili limekuwa ni kero kwa wananchi wa Tunduru, hawaelewi ni kwa nini hawataki kuonesha hesabu hii kwenye Vyama vya Msingi na kutoa ripoti kwa wenye Vyama? Huko inakokwenda, anakagua nani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana jambo hili Mheshimiwa Waziri alichukulie kwa umakini zaidi kwa sababu wananchi wa Tunduru bado wana kilio na jambo hili ingawa tulianzisha wenyewe kwa mapenzi mazuri ili kuhakikisha kwamba timu yetu inasonga mbele kwa ajili ya maendeleo ya Tunduru, lakini bado hili jambo halijakaa vizuri mpaka sasa hesabu hakuna, na huko inakokwenda hiyo fedha, hesabu haioneshwi, na hakuna mtu yeyote, vikao hawafanyi. Hili jambo hili ni kero kwa wananchi wa Tunduru, naomba tuweze kuhakikisha kwamba linafanyiwa kazi. (Makofi)

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa. Ndiyo Mheshimiwa.

T A A R I F A

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji anayeongea, amezungumza vizuri, lakini taarifa ama mapato ya timu ya mpira yoyote, hayasomwi kwa wananchi ama wakulima isipokuwa yanapelekwa kwa Wajumbe wa Timu ama management, kwa timu zote Tanzania nzima, ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mpakate, unapokea taarifa hiyo?

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni sahihi, taarifa ya timu inakwenda kwa wadau, lakini fedha hii inachangiwa kutokana na zao la korosho ambalo wananchi wanachangia.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Pamoja na kwamba muda wako umekwisha, nimekuongeza dakika nyingine ili uweze kuweka hoja yako vizuri.

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba aelewe kwamba, ninachokisema, Vyama vya Msingi vina wanachama wake ambao ni Wajumbe halali wa Mkutano Mkuu; hawajaambiwa mapato yao, sehemu ya ushuru ya shilingi 65 inakwenda kuchangia mpira, na watoe hesabu kwamba mwaka huu tumetoa shilingi fulani. Ndiyo tunayotoa hii bajeti kwamba mwakani tutachangia shilingi fulani kutokana na makisio yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo makisio hayaonekani kwenye vitabu vyovyote vya Vyama vya Msingi. Kwa maana hiyo, wanachama ambao ni wananchi wa kawaida wanapata mashaka, fedha hii inakusanywa kwenye Vyama vya Msingi, wale wakulima hawaambiwi. Hatutaki hesabu ya mpira, tunataka hesabu kwenye Chama cha Msingi ioneshe, Chama cha Msingi kinachangia Shilingi ngapi kwenye maendeleo ya michezo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. (Makofi)