Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika hoja hii ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali kabisa, nitangulie kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri ya bajeti ambayo imejipanga vizuri kuhakikisha kwamba ulinzi na usalama katika nchi yetu unaendelea kuwekewa mkazo na msisitizo ili kuhakikisha kwamba wananchi wa Taifa hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wanaendelea na shughuli zao za maendeleo bila kubughudhiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kuyapongeza majeshi yetu ya Polisi na Magereza kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuifanya. Wanalitumikia Taifa kwa juhudi kubwa ambayo imetuwezesha sisi kuweza kufanya kazi za kila siku bila ya matatizo makubwa. Nakiri matunda ya kazi zao tunayaona, yamejionesha katika hali nyingi. Kubwa ni hali ya amani na utulivu katika nchi yetu ambayo imetuwezesha kufanya kazi vizuri. Pia udhibiti wa wimbi la ujambazi katika nchi. Ujambazi hakuna katika nchi yetu hivi kama tulivyokuwa tunaathirika huko nyuma, ambapo imepunguza hofu kubwa sana, imepunguza hofu kwa wananchi wetu na kuwawezesha kufanya kazi vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hasa kwa Jeshi la Traffic, wamejitahidi sana kutusaidia katika Majiji yetu makuu hususan Dar es Salaam, kuhakikisha kwamba msongamano wa magari nyakati za kwenda na kutoka kazini msongamano huu umekuwa nafuu sana. Tunapoteza muda mwingi sana katika kwenda kazini na kurudi kazini, lakini kwa juhudi zao ambazo tunaziona wazi wazi hivi sasa kazi kubwa ambayo wananchi wanaifanya ni kutekeleza wajibu wao ndani ya sehemu zao za kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Magereza hali kadhalika linafanya kazi kama hiyo ya kutekeleza wajibu wao. Magereza pamoja na upungufu kadhaa ambao wanao lakini wanajitahidi kuhakikisha kwamba wananchi wenzetu wale ambao wamekabidhiwa mikononi mwao wanawalea vizuri na kuwaweka katika hali ya mafunzo mpaka kipindi wanapotoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikiri kwamba kuna upungufu kadhaa ambao naiomba Serikali ijitahidi sana kuhakikisha kwamba upungufu huu unaondolewa. Suala kubwa la uchakavu wa Vituo vya Polisi ni suala ambalo linaathiri Jeshi letu, kuwanyima nafasi ya kuweza kufanya kazi zao kwa ufanisi. Vituo vingi ni chakavu, hakuna ofisi za kufanyia kazi vizuri na hata zile ambazo zipo, pamoja na udogo wake, lakini Polisi wanafikia hata kunyeshewa na mvua katika ofisi hizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri alenge juhudi zake kuhakikisha kwamba vituo hivi vinakarabatiwa kwa haraka iwezekanavyo na pia kuweza kujenga vituo vingi zaidi. Nikitoa mfano wa kule kwetu Bagamoyo, Kituo kile tumekikarabati kwa harambee, kilikuwa kinavuja sana wakati wa mvua hata Ofisi ya OCD inabidi asogeze meza huku na kule wakati wa mvua; na hivi sasa baada ya harambee hizi ndipo kinaweza kufanya kazi vizuri. Najua hali kama hiyo inawaathiri wananchi wengi na Askari wengi katika maeneo mbalimbali. Kwa hiyo, naomba Serikali yetu Tukufu iweze kuliangalia jambo hili na kuondoa kadhia hii nzito.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine katika miundombinu hii ya Vituo vyetu vya Polisi ni suala kubwa la uhaba na uchakavu wa nyumba za Polisi. Hili ni jambo zito sana. Polisi hawana makazi mazuri. Nashukuru kwamba Mheshimiwa Waziri umekuja na mpango wa ujenzi wa nyumba mpya 4100 na kidogo, lakini hizi hazitatosha kwa sababu uhaba tulionao ni mkubwa zaidi. Tunahitaji mpango mkubwa zaidi wa kuhakikisha kwamba Polisi wana mahali pazuri pa kuishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Bagamoyo tuna Askari 171, lakini chini ya robo ya Askari hawa wana nyumba za kuishi za Polisi. Wale ambao wana nyumba za kuishi za Polisi hizo chache, usiombe kuingia katika nyumba zile, kwa sababu ukiingia utatoka katika hali ya masikitiko na unyonge. Askari wetu hawa ambao wanatuwezesha sisi kuweza kufanya kazi vizuri na kulitumikia Taifa letu hili vizuri, wana haki ya kupata mazingira bora zaidi ili waweze kutumikia vizuri zaidi na sisi tupate ufanisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengi wao wanapanga uraiani, sasa unapopangisha uraiani unakaa na wananchi hao hao ambao kesho unataka uwadhibiti, anapokudai kodi na kesho huyo huyo anayekupangisha nyumba ndiye amefanya makosa, sijui yeye kama Askari anafanya kitu gani! Haya ni madhila makubwa ambayo Mheshimiwa Waziri ni muhimu sana Serikali ikajikita vizuri sana katika kuhakikisha kwamba nyumba; jambo kubwa sana, zito, muhimu katika familia yoyote ya baba mama na watoto; Askari wetu wapate nyumba ambazo ni nzuri zenye hadhi ya kazi yao na ambayo itawawezesha wao kufanya kazi vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya majumuisho ningependa kusikia mpango ambao Serikali inauleta kuhusu ukarabati mkubwa zaidi na ujenzi mpya wa nyumba; ujenzi, ametutajia zile nyumba 4,000 lakini je, katika zile zilizopo ukarabati huu ataufanya kwa kiasi gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuyataja yale ambayo yanawasibu sana na wakati mwingine kuzorotesha uwezo wa Polisi kufanya kazi. Uhaba mkubwa wa mafuta na vipuri kwa Jeshi la Polisi ni jambo ambalo halina kificho. Hawawezi kufanya kazi vizuri kama magari yao hayana mafuta; kwanza magari ni machache halafu mafuta hakuna. Wakati mwingine inabidi kuombeleza; hata safari hii nimewapiga jeki kidogo Polisi katika Jimbo langu kwa kuwapelekea pesa za kununulia mafuta. Sasa haiwezekani ikawa mafuta ni ya harambee wakati ulinzi ni jambo la muhimu sana katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali yetu Tukufu ihakikishe kwamba jambo hili inalisimamia kwa umakini. Mafungu ya mafuta yawe mazuri, vipuri vipatikane, vitendea kazi kama magari yawe angalau ya kutosha kuwawezesha Polisi wetu wafanye kazi inayotakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii pia kuzungumzia hayo hayo kama nilivyozungumzia Jeshi letu la Polisi kwa Jeshi la Magereza, nao wako katika hali ngumu. Ofisi mbovu, hawana ofisi nzuri, miundombinu ya Magereza siyo mizuri, kwa maana ya mabweni ni haba, kuna mlundikano mkubwa wa wafungwa na mahabusu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wakati sasa Serikali ikajikita kuhakikisha kwamba inafanya ujenzi mkubwa sana katika miundombinu ya Jeshi letu la Magereza ili nao waweze kufanya kazi vizuri. Pamoja na vitendea kazi lakini pia pamoja na sare. Siyo jambo ambalo linafahamika sana lakini jambo hili limeanza kunyemelea Jeshi letu la Magereza. Hata sare nayo imeanza kuwa pungufu ambayo itawakatisha moyo sana Wanajeshi wetu hawa. Ni muhimu sana Serikali ikajikita kuhakikisha kwamba hili haliwatii unyonge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Waziri ililenga kufanya Magereza yetu ni Vituo vya Uzalishaji Kilimo, lakini Magereza yetu hayana vitendea kazi vya kilimo. Gereza kubwa kama la Kigongoni lenye zaidi ya ekari 6,000 katika Jimbo la Bagamoyo halina trekta hata moja, halina lori, gari ya Mkuu wa Gereza ni mbovu. Sasa ardhi ile ni nzuri kwa kilimo inayofaa kwa mpunga, safari hii Mkuu wa Kikosi ameweza kulima ekari 50 tu katika ekari 6,000. Kwa hiyo tuweze kufanya kweli…
MHE. DKT. SHUKURU KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu muda umekwisha, nashukuru na naunga mkono hoja.