Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Hotuba au Bajeti ya Waziri Mkuu. Nianze kama wenzangu kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, lakini Makamu wa Rais Dkt. Philip Isidor Mpango na Waziri Mkuu kwa kazi nzuri ambayo inafanyika katika kutekeleza maendeleo ya nchi yetu na ushahidi unaonekana kwamba kazi kubwa inafanyika katika utekelezaji wa miradi mikubwa; hasa mradi wa reli ambako maeneo mbalimbali kazi kubwa tunaiona ikifanyika, lakini Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ambako umeshafikia asilimia 83 na ni mategemeo kwamba baada ya mradi huo kukamilika Watanzania wataisahau shida ya umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu pia inapiga hatua kubwa chini ya usimamizi mahiri wa Daktari Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni kazi kubwa inafanyika kwenye eneo la elimu, kwenye umeme usiseme lakini miundombinu tunaenda nayo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kwa niaba ya Wananchi wa Hanang’ kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwa miradi mingi ya maendeleo ambayo imeelekezwa ndani ya Jimbo la Hanang’. Kwenye upande wa barabara tulikuwa na changamoto kubwa hasa upande wa TARURA, bajeti yetu ilikuwa milioni 800 na hamsini na kitu tu, lakini mpaka sasa tuna barabara nyingi ambazo tumefungua. Nitaje barabara chache tu ambazo wananchi sasa hivi wanafurahia matunda ya Daktari Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa na barabara yetu mbovu kabisa ambayo iliyokuwa inatusumbua barabara ya Masqaroda - Lambo – Masakta kwa sasa wananchi wanateleza maendeleo yanaenda sawa sawa. Tulikuwa na barabara mpya nayo imefunguliwa kuunganisha Kata za Bassodesh na Mulbadaw tumefungua barabara mpya kuunganisha Hilbadaw na Mwanga hicho ni kijiji ambako kilikuwa na changamoto kubwa na tuliwaahidi wakati wa uchaguzi, utekelezaji unaenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, upande wa maji, kazi kubwa pia imefanyika, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. Tulikuwa na changamoto kubwa ya maji, nilivyoanza kuja tu hapa Bungeni nilianza kulia kwa Mji wa Katesh, mji mkubwa, maji tunateka kwa mikokoteni ya punda, lakini kwa sasa Wanakatesh wanapata maji ya kutosheleza. Naamini kuna maeneo ya kuboresha ambako tutaendelea kuboresha lakini Mradi mkubwa wa Maji kutoka Mogitu, Gehandu, mradi wa zaidi ya bilioni sita karibu umefika asilimia 80 ya utekelezaji wake ambako utaenda kutekelezwa ndani ya bajeti hii inayokuja. Ni kazi kubwa ambayo imefanyika, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. Tumechimbiwa visima zaidi ya 40 ndani ya Jimbo langu la Hanang’.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa na miradi mbalimbali ambayo ilikuwa kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji nayo imeendelea kukamilika. Tunashukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kweli ametuwezesha na changamoto ya maji inaendelea kupungua ndani ya Jimbo la Hanang’. Tunalo ombi kwenye visima ambavyo tumechimbiwa visima 24 lakini tunaenda kuchimbiwa visima 16, vile visima ambavyo tayari vimeshachimbwa tunaomba maji yale yasambazwe kwa wananchi. Bajeti tunayotengewa kwa sasa kwa visima hivyo hatuwezi kusambaza kwa wakati, tunaomba tuongezewe fedha ili tuweze kusambaza kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunashukuru kwamba kwenye bajeti hizi zinazokuja tutapeleka maji Gawal, tutapeleka maji Gehandu, tutapeleka maji Mureru lakini Gijetamuhog ambako hawajawahi kupata maji nao wataenda kupata maji, lakini Mureru nao wataenda kupata maji. Tunaomba kasi hio iongezeke ili maeneo yote yaweze kupata maji, changamoto ya maji iweze kuondoka. Kwa visima vile 16 naomba maeneo ya Dajameda na Wandela yapewe kipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, tulitarajia wakati fulani Waziri Mkuu kututembelea kwenye Jimbo letu la Hanang’ akiwa Mgeni Rasmi akamtuma Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Daktari Mwigulu Nchemba. Alipofika pale mbele ya Wanahanang’ nilimwomba kwa sababu amebeba pochi ya Mama aifungue aiangalie barabara yetu ya Mogitu – Haydom na yeye kwa kuwa ni mtoto wetu, jirani yetu, aliahidi kwamba pochi ya Mama ataifungua, mpaka sasa sioni dalili ya hiyo barabara kuanza. Naomba hiyo pochi ifunguke barabara ya Mogitu – Haydom ianze kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ile barabara inategemewa na wananchi wa Hanang’. Ukanda ule wa juu ndio unakolimwa ngano nyingi na nchi yetu ina changamoto kubwa ya upatikanaji wa ngano, lakini ukanda ule ndiko kunapolimwa shahiri na mazao mbalimbali, ni ardhi ya kilimo, vitunguu tunalima mpaka tunasafirisha katika nchi mbalimbali. Tunaomba tusaidiwe hii barabara ni barabara ya kimkakati. Barabara ambayo itasaidia wananchi wetu pia kupata huduma za afya. Kwa maana ya kurahisisha kuunganisha usafiri kutoka maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Hanang’ na Wilaya ya Mbulu hasa Hospitali ya Haydom.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba hii barabara kwenye bajeti hii isikose fedha. Jana niliuliza swali la nyongeza hapa kwamba barabara hii itaanza lini, nikaambiwa upembuzi na nini kwamba swali hilo lilishajibiwa, tunachotaka sisi Wanahanang’ na Wanambulu tuone barabara inajengwa na hatimaye barabara inapitika ili kurahisha usafiri kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilishawahi kuongelea suala la ugonjwa wa malaria kwenye Bunge hili. Ni ugonjwa ambao unaongoza katika kupoteza maisha ya watu wetu lakini tuna kiwanda kimejengwa cha viua wadudu ambacho kitatokomeza viluwiluwi vya mbu. Mbu ni kero katika makazi yetu katika maeneo yetu, tuna kiwanda ambacho kina uwezo wa kuzalisha lita milioni sita kwa mwaka. Kiwanda hiki kimejengwa toka mwaka 2016. Kiko nchini mwetu mpaka sasa sisi tunahangaika na malaria, tunapoteza watu wetu kwa sababu ya malaria, lakini kiwanda tunacho, hakina soko, ilivyofanyika feasibility study wateja wakubwa walikuwa ni Wizara ya Afya kwa sababu ya kudhibiti malaria, lakini TAMISEMI kwa sababu nao wanashughulika na suala la afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi ninavyoongea kiwanda hicho kimeweza tu kuzalisha lita 916,747 kwa miaka yote ambayo imefanya kazi toka mwaka 2016, lakini tunaendelea kupoteza watu. Kiwanda hicho kinaendelea kufanya kazi kwa hasara, kiwanda cha kwetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri kuna sababu ya sisi akili zetu kuanza kufanya kazi. Kiwanda ni cha kwetu tumekitengeneza, kinapata hasara hakina soko, lakini sisi tunaugua, tunakufa kwa ajili ya malaria. Hii haikubaliki, kila Ripoti ya Wizara ya Afya utaambiwa tu kwamba ugonjwa unaongoza kuua watu Tanzania ni malaria. Tunao mfano Zanzibar, wenzetu malaria wamepunguza kwa asilimia kubwa sana, lakini Tanzania Bara mpaka sasa malaria bado ni changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda kinaendeshwa kwa hasara, tuchukue hatua sasa, Mheshimwa Waziri Mkuu tunaomba awasimamie hawa watu wake. Wizara ya Afya, Wizara ya Viwanda na Biashara kwa sababu, Viwanda na Biashara wanayo dawa, Wizara ya Afya wanapaswa kununua dawa ili kudhibiti malaria, lakini hilo halifanyiki. Tunaomba eneo hilo lisimamiwe vizuri. TAMISEMI kwenye halmashauri zetu wasimamie kuhakikisha kwamba tunadhibiti mbu wanaoambukiza malaria kwa sababu dawa tunayo hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ingekuwa ni teknolojia tunayotafuta kwa mbali tungekuwa tunahangaika kila siku tunarudia jambo hilo hilo hatusogei, tuchukue hatua sasa tusogee kwenye eneo hilo. Niseme tu, kama changamoto yetu ni kwamba tukiwa na taasisi ikawa ya umma umma hivi watu hawaoni hizi fursa na kuunganisha mazingira yaliyopo ili kuhakikisha kwamba tunachukua hatua na tufanye kazi kwa ufanisi. Tuangalie watu tunaowaweka kwenye maeneo hayo. Taasisi zetu zimekuwa zinajisahau kufanya kazi Kiserikaliserikali, wakati kuna taasisi kama zenyewe zinafanya kazi za binafsi, zinafanya kazi vizuri. Tuchukue hatua tuweke watu ambao tutawawekea vigezo hasa tuangalie performance base za wale ambao tunawapa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani una kiwanda kimesimama, wateja wapo, hakuna kinachoendelea na hii imekuwa kila sehemu kwenye nchi yetu. Ukiangalia TTCL wenzao kina Vodacom kina Tigo na wengineo wanaenda vizuri na unawasikia matangazo kila sehemu, TTCL anza kutafuta vocha utazunguka mji mzima, kupata vocha ni shida. Tuangalie kama kweli bado tunahitaji kuwa na taasisi zinazofanya biashara kwenye nchi yetu ambazo zinamilikiwa na Serikali. Tukishafanya tathmini hiyo, kama kweli tunahitaji, tuweke watu ambao wanaweza kufanya kazi ya uzalishaji wakashindana sokoni, wakaleta tija. Kama hilo haliwezekani tuwezeshe sekta binafsi iendeshe hivi vitu, sisi tuvisimane. Vile ambavyo vina maslahi ya umma tuweke usimamizi uwe imara zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nayasema haya kwa sababu udhaifu umekuwa mwingi katika maeneo mengi. Nikirudi kwenye NDC…

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, wamekopesha matrekta kwa wakulima…

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nataka nimpe taarifa mzungumzaji Mheshimiwa Hhayuma kwamba ukitaka kutafuta vocha ya TTCL ukiwa kule kijijini ni mpaka utafute namna ya kuweka M-pesa vinginevyo vocha hakuna. Minara ipo kila kitu lakini vocha ni tatizo.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Samweli, endelea.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo taarifa naipokea na naomba nisisitize tu kama Serikali kwenye taasisi zile ambazo zinafanya biashara inamaanisha biashara basi waweke watu ambao kweli watasimamia biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa najaribu kuongelea suala la NDC wamekopesha matrekta ya URSUS kwa wakulima. Kilichofanyika tu matrekta yale yamekabidhiwa kwa wakulima, walitakiwa wawe na kipindi cha warrant, walitakiwa watembelee na kufanya services, lakini toka wamekabidhi wameyatupa huko. Wanachofanya kwa juhudi kwa sasa hivi, mara ya wapite kupitia TAKUKURU, kupitia kwa nani kuwakamata wakulima hawa. Wenyewe hawajatekeleza wajibu wao wa kibiashara, lakini wanataka haki, haki yeyote inapaswa kwenda na wajibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)