Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ili na mimi jioni hii niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nikiungana na Wabunge wenzangu waliopata fursa ya kuanza kuchangia na mimi kwa dhati kabisa nitumie fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anajitoa kuwatumikia Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu katika hotuba yake ukurasa wa kumi na mbili ametukumbusha Watanzania kwamba mradi wa kufua umeme wa Bwawa la Mwalimu Nyerere megawatt 2115 serikali imetoa bilioni 869.93 na mradi umefikia 83%; hizi ndizo kazi za Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kwamba haitoshi mradi mkubwa wa kusafirisha mafuta kutoka Uganda Hoima mpaka Tanga, kilomita 1443 Serikali imeshatoa bilioni 30.39 kwa ajili ya kulipa fidia waathirika wa maeneo ambayo bomba itapita, hizi ndizo kazi ambazo Watanzania wanafanyiwa na Mheshimiwa Rais Wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upekee wake sisi wana- Kilwa na hususani wana-Kilwa Kusini Rais Samia amefanya ambayo hayajawahi kufanyika, na kwa kweli ameacha alama ambayo kwa kweli hatutoisahau. Kulikuwa na mradi ambao umesuasua kwa muda mrefu wa maji kwenye miji 28 umeanza kutekelezwa katika kipindi hiki cha Dkt. Samia. Pia kulikuwa na ujenzi wa bandari ambao mipango yake ilikuwa ni ya muda mrefu, tulipitisha katika mpango wa miaka mitano ya maendeleo hapa Bungeni. Nitumie fursa hii kuwataarifu Watanzania kwamba mradi huu tayari umeanza pale Kilwa Masoko na unathamani ya shilingi bilioni 266.7; Kilwa hatujawahi kupata mradi mkubwa kama huu tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama kwamba haitoshi Mheshimiwa rais ameendalea kutusaidia wanakilwa katika sekta za barabara. Tumeongezewa fedha kwenye TARURA kutoka milioni 800 ambayo ilikuwa ni kwa ajili ya Wilaya nzima ya Kilwa kwa wakati ule mpaka kufikia karibu bilioni tatu kwa majimbo yote mawili kwa mwaka, Kilwa Kaskazini na Kilwa Kusini. tunamshukuru na kumpongeza sana Rais Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo sasa nije katika baaadhi ya maeneo ambayo nilidhani Serikali ikitekeleza basi tutakuwa tumemsaidia na kumfanya Rais Samia apendeze zaidi kwa Watanzania na wana Kilwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza katika eneo la ujenzi wa bandari, nitoe rai kabisa kwamba wakati Serikali inatekeleza ujenzi huu wa bandari basi ifikirie kuweka miundombinu mingine rafiki itakayoendana na uwepo wa Bandari hii ya Uvuvi pale Kilwa Masoko. Kwa mfano barabara iliyopo kutoka pale bandarini kuelekea Nangurukuru kilometa takribani 30 haiko katika viwango ambavyo vitaendana na bandari hiyo. Nitoe rai katika bajeti hii barabara hii ipanuliwe na ijengwe katika viwango. Lakini pili mundombinu rafiki na taasisi rafiki ambazo zitaendana na uwepo huu wa bandari ikiwemo viwanda vya kuchakata mazao ya Bahari na chuo cha uvuvi pale KilwaMasoko ni vitu ambavyo pia vinatakiwa vifikiriwe katika bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nieleze kwa masikitiko kidogo, kwamba pamoja na utekelezaji wa bandari ambao unaendelea pale Kilwa Masoko lakini wananchi wangu wapatao 54 bado hawajalipwa fidia kupisha upanuzi na ujenzi huu wa bandari. Nitoe rai kabisa, katika kipindi hiki kifupi ndani ya mwaka huu muda si mrefu Serikali ifikirie kuwalipa fidia wananchi wangu wapatao 54 ili masuala ya ujenzi wa bandari yasiingie migogoro ya wananchi kudai fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija katika uboreshaji na upanuzi wa viwanja vya ndege, tulipitisha katika mpango wa miaka mitano, na Kiwanja cha Ndege cha Kilwa Masoko ni miongoni mwa viwanja ambavyo vitapanuliwa na kufanyiwa maboresho. Lakini kwa masikitiko niseme tu kwamba bajeti iliyotengwa kwa mwaka uliopita ilikuwa ni ndogo sana kiasi cha kukarabati runway ile kilometa 800 tu kwa kiwango cha changarawe. nitoe rai kwamba kiwanja hiki cha ndege sasa kijengwe katika viwango vinavyotakiwa, kwa maana kuongeza mita 900 zingine za runway, kuweka uzio wa kiwanja cha ndege na pia kuboresha lile eneo la kupumzikia abiria.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nieleze tu kwamba dhana ya upanuzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kilwa Masoko ni wa miaka takribani miaka 10 iliyopita, na wananchi wangu walifanyiwa tathmini mwaka 2011/2012, na ikarudiwa tena tathmini ili walipwe fidia mwaka 2011/2012 na tathmini hii ilirudiwa tena mwaka jana mwezi wa nne. Kiasi cha wananchi wangu zaidi ya 412 wamefanyiwa tathmini hii lakini bado hawajalipwa fidia hii. Nitoe rai kabisa, Serikali ifanye hima kuwalipa fidia wananchi wangu hawa ili ujenzi utakapokuwa umeanza wa kuboresha na kupanua Kiwanja cha Ndege pale Kilwa Masoko kusiwe tena na malalamiko ya wananchi wetu kudai fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija katika eneo la maji, pamoja na kushukuru kupatiwa mradi ule wa maji kutoka Mto Mavuji kwa ajili ya Miji ya Nangurukulu Masoko na Kivinje niseme tu kwamba bado tunahitaji kupanua wigo wa upatikanaji wa maji vijijini pamoja na mijni. Hapa kwa upekee wake nizungumzie kata moja ambayo kwa kweli haijawahi kupata kunufaika na mradi wa maji wa aina yoyote ile; na hii si kata nyingine isipokuwa ni Kata ya Lihimalyao iliyopo katika Jimbo langu la Kilwa Kusini. Nitoe rai kwa kata ya Lihimalyao kwa upekee wake, hebu Serikali ione uwezekano wa kujenga mabwawa kwa ajili ya kuvuna maji ya mvua.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Kata jirani ya Pande kuna maji ya kutosha. Serikali ione uwezekano wa kutoa maji kwa utaratibu wa mtiririko kupeleka katika Kata hii ya Lihimalyao ndani ya kipindi cha mwaka huu wa bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitoe rai tu kwa Serikali; kwamba ili kupunguza kama si kuondoa kabisa tatizo la maji, si tu Kilwa lakini mikoa yote ya Kusini, kwa nini tusiwe sasa na mpango wa kupanua wigo matumizi ya maji ya Mto Rufiji? Badala ya kupeleka maji ukanda wa Dar es salaam peke yake tawi lingine lije Ukanda wa Kusini ili Mikoa ya Pwani, Lindi, Mtwara pamoja Ruvuma inufaike. Mradi huu wa Mto Rufiji kama utatekelezwa kuanzia kipindi hiki nakuhakikishia kwamba wananchi wa mikoa yote ya kusini niliyoitaja tatizo la maji au changamoto ya maji litakuwa ni baibai na hapo itakuwa kwamba kweli tumewatendea haki.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika miradi ya kimkakati. Sisi pale Kilwa tuna miradi mingi ya kimkakati lakini kwa muktadha wa mchango wangu leo niuzungumzie mradi mmoja tu ambao ni mradi wa kimkakati wa ujenzi wa Stendi ya Nangurukuru. Tunaomba kupitia halmashauri miaka mitatu katika bajeti yetu kama maombi maalum; lakini niombe mwaka huu maombi yetu yale maalum ya bajeti ya kupanua ujenzi wa stendi ya nangurukuru kama mradi wetu mkakati uweze kuidhinishwa na Bunge hili na hatimaye wana-Kilwa waweze kunufaika na stendi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikumbushe pia Bunge lako kwamba katika mpango wa miaka mitano wa maendeleo tulioupitisha hapa bungeni tulipitisha ujenzi wa kiwango cha lami Barabara ya Kiranjeranje Nanjirinji mpaka Ruangwa, lakini pia Barabara ya kutoka Nangurukuru mpaka Liwale. Ninayo furaha kusema kwamba kazi za upembuzi yakinifu na usanifu zimekamilika. Ni wakati muafaka sasa barabara hizi zianze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipendekeze barabara ya Nangurukuru mpaka Liwale ambayo kimsingi inahudumia majimbo matatu, Jimbo la Kilwa Kusini, Kilwa Kaskazini pamoja na Jimbo la mtani wangu Kuchauka kule, Liwale ianze kutekelezwa ndani ya mwaka huu angalau kilometa 50 kutoka pale Nangurukuru. Tukifanya hivyo tutakuwa tumeyatendea haki majimbo hayo matatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho niseme tu kwamba tunaendelea kupongeza na kushukuru juhudi za Mheshimiwa Rais Samia katika kuboresha miundombinu katika sekta za huduma ikiwemo afya na elimu. Katika elimu tumepata madarasa ya kutosha. Hata hivyo, nitoe rai, bado tuna tatizo kubwa la nyumba za walimu lakini pia bado tuna tatizo kubwa la madawati katika maeneo yetu ya halmashauri zetu. Niombe katika bajeti hii kwamba tatizo la nyumba za walimu pamoja na madawati liwekewe kipaumbele ili tatizo la ujumla la miundombinula shule zetu za msingi na za sekondari tuweze kulipunguza kwa kiwango kikubwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuzungumza haya naomba kuunga mkono hoja.(Makofi)